Aliyekuwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Kodi Tanzania (TRA), Rished Bade
..................................
Kuanzia mwishoni mwa wiki, serikali ya awamu ya tano chini ya Rais
Dk. John Magufuli imekuwa ikichukua hatua kadhaa za kukomesha ukwepaji
kodi katika Bandari hiyo inayotegemewa zaidi kwa mapato nchini. Hadi
sasa, Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Kodi Tanzania (TRA), Rished Bade,
amesimamishwa kazi na kushikiliwa polisi kuhusiana na taarifa za
serikali kukosa mapato takriban Sh. bilioni 80 kutokana na makontena
hayo (349) kupitishwa bila ya kulipiwa kodi. Kadhalika, vigogo wengine
kadhaa wa TRA wamesimamishwa kazi pia na kushikiliwa na polisi wakati
uchunguzi zaidi kuhusiana na kashfa hiyo ukiendelea.
Hata hivyo, wakati serikali ya Rais Magufuli na Waziri Mkuu wake,
Kassim Majaliwa, ikiendelea kutafuta suluhu ya kudumu kuhusiana na
ukwepaji kodi, Nipashe imebaini kuwa kazi hiyo siyo lelemama kwani zipo
njia zaidi ya tisa zinazotumiwa kukwepa kodi katika Bandari ya Dar es
Salaam.
Uchunguzi wa Nipashe uliohusisha mahojiano na vyanzo mbalimbali
umebaini kuwa wanaofanikisha ukwepaji wa kodi hushirikiana kupitia
mtandao mpana unaohusisha wafanyabiashara wasio waaminifu, maafisa wa
TRA, watumishi wa Bandari, wamiliki wa kampuni za usafirishaji na
uondoaji mizigo, maafisa wa bandari kavu, maafisa wa benki zinazopokea
malipo na pia baadhi ya askari.
Chanzo kimeiambia Nipashe kuwa viongozi wa juu wa taasisi
mbalimbali zinazoshughulikia uondoaji mizigo bandarini jijini Dar es
Salaam wamejiundia mitandao mipana inayoingiza mamilioni kila uchao na
hivyo vita iliyoanzishwa na serikali ya Dk. Magufuli inapaswa kuwa
endelevu ili kuleta mafanikio.
“Zipo njia nyingi zinazotumiwa na watu hawa kufanikisha hujuma hizi
kwa manufaa binafsi. Baadhi ya wale wanaoshiriki mchezo huu ni watu
wazito na kwa muda mrefu wamejijengea ushawishi mkubwa serikalini na
hivyo vita hii iliyoanzishwa na Dk. Magufuli na Waziri Mkuu wake siyo
ndogo… ni kazi kubwa na kila mmoja anapaswa kuwaunga mkono, “chanzo
kingine kimeiambia Nipashe.
NJIA 9 ZA UKWEPAJI KODI BANDARINI DAR
Vyanzo vimeiambia Nipashe kuwa maeneo yanayotumiwa kufanikisha
ukwepaji wa kodi yapo mengi, lakini makubwa yanayofahamika zaidi
bandarini hapo ni tisa.
Mosi, ni kupitia mwanya utokanao na mfumo wa zamani wa malipo
usiohusisha ule wa sasa wa kielektroniki, maarufu kama ‘E-Payment’.
Kwamba, wafanyabiashara wengi hutumia mfumo huo wa zamani unaohusisha
matumizi ya karatasi zilizojazwa kwa mkono na hivyo kuwezesha ujanja wa
kubadili taarifa kwa manufaa ya mitandao ya wakwepaji wa kodi.
“Tatizo lililopo ni kwamba mfumo wa E-Payment ni mpya (umeanza
Julai) na umefungwa kwenye benki moja tu iliyopo ndani ya eneo la
Bandari… ule wa zamani unaendelea kutumiwa na wajanja hucheza na
maandishi ya kujaza kwa mkono kuhujumu mapato ya serikali,” chanzo
kimeeleza.
Njia ya pili ya kuhujumu mapato bandarini hapo, imetajwa kuwa ni ya
kushirikiana na maafisa wa benki. Hii ina uhusiano mkubwa na njia ya
kwanza inayohusisha matumizi ya mfumo wa malipo wa zamani usiokuwa wa
kielektroniki. Mfanyabiashara anaweza kuandikiwa kodi sahihi anayotakiwa
kulipa, lakini anashirikiana na wafanyakazi wa benki anayokwenda kuweka
fedha kwa kuhakikisha kuwa baada ya kufanikiwa kuondoa kontena
bandarini, maafisa wa benki husika husitisha malipo hayo kwa kuondoa
fedha husika kwa madai kuwa fedha ziliingizwa kwenye akaunti husika
kimakosa.
“Huwa kuna ushirikiano wa karibu kati ya maafisa wa benki na
mfanyabiashara husika. Baada ya kontena kutolewa bandarini, hamisho la
fedha (transaction) huondolewa katika mfumo kwa maelezo kuwa halikuwa
sahihi,” chanzo kimedai, huku kikisisitiza kuwa ushirikiano huo
huhusisha pia watu wa Bandari na TRA ambao mwishowe hugawana malipo
kadri wanavyokubaliana.
Tatu, ni mwanya wa uvushaji wa makontena yenyewe yasiyolipiwa
ushuru kupitia mageti maalum yanayofahamika kwa kazi hiyo, hasa geti
Namba 3 ambalo chanzo kimedai ndilo linaongoza kupitisha mizigo ya
‘dili’.
“Kwa ujumla yapo mageti matano ya kupitisha bidhaa mbalimbali,
baadhi yakiwa ni ya kupitihia mafuta, nafaka na magari. Hili Namba 3
ndiyo hutumika kupitisha makontena ya bidhaa zenye thamani kubwa na
wengi wasiolipa kodi hulitumia hili,” chanzo kilieleza kabla ya
kufafanua kuwa awali, hilo geti Namba 3 halikuwa na mfumo wowote wa
kuangalia kama kontena husika limelipiwa au la na ndiyo maana lilikuwa
likitumika zaidi kupitisha makontena yasiyolipiwa kodi.
Njia ya nne ya kuhujumu kodi ya mapato ni ya kuwatumia watu
wanaoendesha bandari kavu (ICD’s). Inaelezwa kuwa hivi sasa kuna bandari
kavu 12, ambazo kila meli inapoingia hujulikana kila mzigo husika
unapelekwa kwenye bandari ipi kati ya hizo. Hata hivyo, inaelezwa kuwa
kinachofanyika ni kwa baadhi ya makontena yanayotolewa bandarini ili
yapelekwe bandari kavu kabla ya kukombolewa na wahusika huishia
kupelekwa kwa wafanyabiashara wenye makontena na hivyo kuikosesha mapato
serikali.
“Awali kwenye ICD’s kulikuwa na askari wa mmiliki wa ICD’s na siyo
wa TPA… huyu alikuwa akiangalia malipo ya bosi wake tu ambayo ni gharama
za kuhifadhi mzigo na hivyo TPA na TRA huambulia patupu,” chanzi
kimeeleza, kikiongeza kuwa hivi sasa walau kuna nafuu kwani kwenye ICD’s
kuna walinzi wa TPA lakini hilo limefanyika baada ya watu kuwa tayari
wameshaiba sana.
Njia ya tano inayotumiwa kukwepa kodi ni ya kubadili taarifa, hasa
kupitia watu wenye wajibu wa kufanya tathmini. Kwamba, badala ya mzigo
kukadirwaa kodi kwa kiwango sahihi, wahusika ambao zaidi huwa ni watu wa
TRA hukadiria fedha kidogo baada ya kujihakikishia kuwa nao wanapewa
mgawo na wafanyabiashara.
“Hapo utakuta kontena la kodi ya milioni 80, mteja anaambiwa alipe
milioni 40 tu … na wakati mwingine kiasi hicho pia hakiandikwi balki
huandikwa cha chini zaidi kama milioni 5 tu…hii ni njia nyingine
inayoligharimu taifa mabilioni ya fedha,” chanzo kimeeleza.
Chanzo kimeeleza zaidi kuwa njia ya sita inayofanikisha ukwepaji
kodi ni mtandao mpana wa baadhi ya vigogo wa maeneo mbalimbali Bandarini
na TRA, ambao hawa huhakikisha kuwa wanakuwa na timu ya vijana wao wa
kazi karibu katika kila eneo ili kufanikisha mipango yao.
“Hii ndiyo njia kubwa ya hujuma. Kama utakumbuka aliyekuwa Waziri
wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe, alisambaratisha baadhi ya mitandao
kwa kuwagusa vigogo 27… ile ilikuwa kuvunja mtandao uliokuwapo. Hilo
lilisaidia kiasi, lakini sasa ipo pia mitandao mingine ambayo uchunguzi
ukifanyika utabaini kuwa mambo yameanza kurudi kama zamani,” imeelezwa.
Njia ya saba ya ukwepaji kodi ni kwa baadhi ya vigogo wa Bandari na
TRA kuanzisha kampuni zao za uondoaji mizigo bandarini. Inaelezwa kuwa
hizi hutumiwa sana kufanikisha ‘dili’ za ukwepaji kodi na ndiyo maana
haishangazi kusikia kuwa kuna makontena zaidi ya 300 hayaonekani kwenye
kumbukumbu za TRA.
Chanzo kimeeleza zaidi kuwa njia ya nane ya ukwepaji kodi ni
kuonyesha kuwa kontena linapelekwa nje ya nchi, kwa mfano Malawi, wakati
ukweli ni kwamba huishia hapahapa nchini.
“Utakuta kontena linadaiwa kupelekwa Malawi, lakini linachukuliwa
na gari kukuu linaloonekana wazi kuwa haliwezi kufika hata Kibaha… njia
hii pia hutumiwa sana kuikosesha serikali mapato,” chanzo kingine
kiliiambia Nipashe.
Kadhalika, chanzo kiliitaja njia ya nane ya ukwepaji kodi kuwa ni
ucheleweshaji wa makusudi wa utoaji makontena. Kwamba, mteja anapotaka
kutoa mzigo wake kwa kufuata njia halali zilizopo, huishia kuzungushwa
kila uchao ili akubali kutoa rushwa na mwishowe kulipishwa kiwango
pungufu cha kodi au kulipa fedha zisizoingia kabisa kwenye mikono ya
TRA.
Njia ya tisa, kwa mujibu wa chanzo chetu, ni ubabaishaji
unaofanyika katika kuorodhesha idadi ya makontena inayotolewa bandarini
kwenda kwenye bandari kavu. Hapa, kama makontena yanayotolewa ni 12,
basi huandikwa kuwa ni 10 na mengine mawili huishia kunodolewa bila ya
kuwa na kumbukumbu zake kwa ajili ya kulipiwa kodi.
Pamoja na kuwapo kwa njia zote hizo, chanzo kimedai kuwa sababu
kubwa ya kufanikiwa kwa ukwepaji kodi ni mtandao mpana unaoundwa na
vigogo mbalimbali na ndiyo maana taarifa mbalimbali za wakaguzi wa ndani
na wa nje katika Bandari ya Dar es Salaam huishia kubaki kwenye
makabrasha bila ya kuwapo kwa utekelezaji wowote wa vitendo juu ya yale
yanayopendekezwa na wataalamu.
WAFANYABIASHARA WAFICHUA ZAIDI
Mwenyekiti wa Umoja wa Wafanyabishara Tanzania, Johnson Minja,
alisema suala la serikali kupoteza mapato makubwa bandarini lilikuwa
kilio chao cha muda mrefu na hivyo wanafurahi kuona kuwa sasa, chini ya
Rais Magufuli, serikali imeanza kushughulikia tatizo la hujuma ya mapato
ya serikali kwenye Bandari ya Dar es Salaam.
Alisema kilio chao kikubwa kilikuwa ni kuiomba serikali kuweka bei
elekezi ya kutoa kontena bandarini kulingana na bidhaa badala ya kuwa na
bei holela ambayo mwishowe wakubwa wengi walitumia mitandao yao kulipa
kidogo huku wengi walio na mitaji midogo wakiumia kwa kutozwa kodi kubwa
ili kufidia kiwango kisicholipwa na wakubwa.
BEI ELEKEZI YA SASA
Minja alisema waliamua kwa pamoja kila kontena la futi 40 la mzigo
wa nguo litozwe kodi ya Sh. milioni 25 bandarini huku kwa vifaa vya
ujenzi walipitisha bei elekezi kuwa ni Sh. milioni 27 kwa kontena moja.
“Kontena la vifaa vya umeme lenye ukubwa wa futi 40 ni Sh. milioni
30 huku kontena la vitenge la futi 40 likitozwa kodi ya Sh. milioni 40,”
alisema, akiongeza kuwa bei hiyo elekezi imeanza Novemba baada ya
Magufuli kushinda urais Oktoba 25.
Minja alisema awali vigogo na maofisa wa TRA walikuwa wakihusika
kupitisha mizigo bila kutoza kodi au kutoza kidogo kwa baadhi ya watu.
POLISI
Idadi ya watu waliokamatwa kutokana na kuhusishwa na hujuma ya
ukwepaji kodi kutokana na makontena 349 yaliyopitishwa bandarini
kinyemela imezidi kuongezeka baada ya watu wengine kadhaa kukamatwa jana
na kuwekwa mbaroni.
Inaelezwa kuwa kati ya wale waliokamatwa jana, ni pamoja na baadhi ya wafanyabiashara na pia vigogo zaidi wa TRA.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Ilala, Luca Mkondya, alisema kuwa suala
hilo ni nyeti na linahitaji upelelezi wa kina na hivyo, licha ya kukiri
kuwa wamewakamata watu wengine zaidi jana, lakini hakuwa tayari kutaja
idadi ya watuhumiwa hao waliowaweka mbaroni wala majina yao.
Badala yake, Kamanda Mkondya alisema alisema kumalizika kwa
upepelezi kunategemeana na jinsi watakavyopokea ushahidi kwa wakati na
baada ya hapo hatua zaidi za kisheria zitachukuliwa.
Aidha, Kamanda Mkondya hakutaka pia kuzungumzia kuhusu kuwapo kwa dhamana kwa watu hao waliowashikilia, wakiwamo vigogo wa TRA.
Alipioulizwa, Kamanda wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Sulemain
Kova, alisema atatoa ufafanuzi zaidi kuhusiana na watu waliokamatwa juu
ya makontena yasiyolipiwa kodi bandarini leo.
“Kila kitu ni kesho (leo)… nitaitisha press conference na kueleza kwa kina,” alisema Kamanda Kova .
CHANZO:
NIPASHE
Post a Comment