Rais John Magufuli.
..............
Na Gwamaka Alipipi
Uchunguzi uliofanywa na Nipashe ukihusisha pia mahojiano na baadhi
ya wachambuzi wa masuala ya siasa, umebaini kuwa, mwenendo wa serikali
ya Rais Magufuli ambayo hadi sasa bado haijawa na Baraza lake la
Mawaziri umekuwa ukiwapa matumaini makubwa Watanzania wengi kutokana na
hatua mbalimbali zinazochukuliwa kwa nia ya kumaliza kero mbalimbali
katika siku 32 tu za kuwapo madarakani na kuzidi maradufu kasi ya
serikali kamili ya Rais Kikwete iliyokuwa na jumla ya mawaziri 55 na
kudumu madarakani kwa miaka mitano, sawa na siku 1,825 (mwaka mmoja ni
siku 365).
“Hii kasi ya Serikali ya Rais Magufuli inaibua mambo mengi sana.
Kwanza inawapa matumaini makubwa Watanzania kwa kuamini kuwa miaka
mitano ijayo, kama kasi hii itadumishwa, maana yake taifa litapiga hatua
kubwa za maendeleo,” mmoja wa wachambuzi wa masuala ya siasa aliiambia
Nipashe.
“Hata hivyo, kasi hii inaibua maswali mazito kuhusiana na kile
kilichofanywa na serikali kamili ya awamu ya nne katika kipindi chake
cha mwisho ikiwa na mawaziri 30 na naibu mawaziri 25… kwa nini
ilishindwa kushughulikia baadhi ya mambo yaliyokuwa wazi kabisa na
ambayo Magufuli na wenzake watatu wamefanikiwa kuyafanya katika kipindi
kifupi cha mwezi mmoja?. Kwakweli kuna mengi ya kujiuliza,” mchambuzi
huyo alihoji wakati akizungumza na Nipashe.
Mchambuzi mwingine aliiambia Nipashe kuwa, utendaji wa serikali ya
Magufuli inayoundwa na viongozi wakuu watatu tu, yaani Rais mwenyewe
(Magufuli), makamu wake Samia Suluhu na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa,
tena katika siku 32 tu za kuwa madarakani, unaibua maswali mengi mazito
kuhusiana na ufanisi wa serikali ya iliyokuwa na mawaziri 55, huku
ikitumikia wananchi kwa miaka mitano.
“Yapo mengi yanayoibua maswali haya, kwa mfano, Magufuli na
wenzake wawili wamefanikiwa kufichua mianya ya ukwepaji kodi mkubwa
katika Bandari ya Dar es Salaam. Kulikuwa na matumizi makubwa holela ya
fedha za umma kupitia sherehe zisizo na idadi, semina, makongamano,
posho za vikao visivyo na tija, utitiri wa safari na mambo mengi
yaliyoshughulikiwa na Magufuli na wenzake ndani ya mwezi mmoja tu wakati
mawaziri wa Rais Kikwete walishindwa kuyashughulikia kwa miaka yote
mitano ya mwisho. Yapo mengi ya kujiuliza, kwamba je, ni kweli wote
walikuwa wakifanya kazi kwa maslahi ya umma au ya kwao binafsi?”.
“Na je, ni kweli baadhi yao walizidiwa nguvu ya fedha za baadhi ya
wafanyabiashara wasio waaminifu au na wao wenyewe walikuwa ni sehemu ya
mtandao wa hujuma dhidi ya mali za umma?. Kwakweli maswali ni mengi na
mazito dhidi ya wasimamizi wa ofisi mbalimbali za umma katika serikali
iliyomaliza muda wake,” mchambuzi mwingine aliongeza.
Aidha, katika uchunguzi wake, Nipashe imebaini kuwapo kwa mambo 10
makubwa ambayo Serikali ya Magufuli isiyokuwa na Baraza la Mawaziri
imefanikiwa kuyatekeleza kwa mafanikio makubwa licha ya kuonekana kuwa
yalishindikana katika kipindi chote cha miaka mitano iliyopita na
kuigharimu serikali mabilioni ya fedha.
Baada ya ushindi wake wa asilimia 58.46 ya kura zote halali
zilizopigwa katika uchaguzi mkuu Oktoba 25, 2015, Magufuli aliapishwa
Novemba 5, mwaka huu na kuanza kazi siku hiyohiyo kwa kumteua George
Masaju kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
ALIYOFANYA MAGUFULI KWA SIKU 32
1.SAFARI ZA NJE
Mara baada ya kuingia madarakani, Rais Magufuli alifutilia mbali
safari holela za nje alizodai zimekuwa zikiligharimu taifa mabilioni ya
fedha kila uchao. Hili alilitolea uamuzi Novemba 6. Akaagiza kuwa safari
zote muhimu ughaibuni ni lazima zipate ruhusa yake au ya Katibu Mkuu
Kiongozi Ikulu, lengo ikiwa ni kuokoa fedha zinazoweza kutumiwa kwa
shughuli nyingine za maendeleo kwa taifa. Akitolea mfano, alisema katika
mwaka wa fedha wa 2013/2014 na 2014/2015, taifa lilitumia zaidi ya Sh.
bilioni 356 kugharimia safari za nje; jambo ambalo yeye hayuko tayari
kulishuhudia.
Hadi sasa, Magufuli ameshaonyesha mfano kwa kuamuru watu wanne tu
kusafiri wakitokea ofisi ya ubalozi wa Tanzania Uingereza kwenda
kumuwakilisha katika mkutano wa wakuu wa nchi za Jumuiya ya Madola
kwenye visiwa vya Malta, badala ya watu zaidi ya 50 waliozoea kusafiri
katika safari kama hii ya Rais.
Katika serikali iliyokuwa na jumla ya mawaziri na naibu mawaziri
55, jambo hili halikuwezekana hata kidogo, licha ya kelele nyingi
zilizokuwa zikipigwa na wananchi mbalimbali akiwamo Mwenyekiti wa
NCCR-Mageuzi, James Mbatia aliyedai hali ni mbaya na kwamba, Rais
Kikwete peke yake alishatumia muda mwingi wa kuwapo madarakani akiwa nje
ya nchi na kuligharimu taifa wastani wa zaidi ya Sh. trilioni 4.5
katika miaka 10 ya kuwapo kwake madarakani.
2. UKWEPAJI KODI BANDARINI, TRA
Hili ni eneo mojawapo kati ya mengi yaliyofanywa kwa umahiri mkubwa
na ‘jeshi la watu watatu’ la serikali ya Rais Magufuli. Kwa kurejea
ahadi yake ya kuhakikisha kuwa Mamlaka ya Kodi Tanzania (TRA) inaongeza
mapato na pia kukomesha vitendo vya ufisadi, tayari Magufuli na serikali
yake wameibua gumzo kubwa baada ya kufichua ukwepaji kodi uliobaini
kuwapo kwa makontenda 2,431 yaliyopitishwa katika Bandari ya Dar es
Salaam bila kulipiwa kodi. Awali, yalinaswa makontena 349 yasiyolipiwa
kodi na kulikosesha taifa takriban Sh. bilioni 80, hivyo wastani wa
mapato yaliyokuwa yamepotea kwa makontena 2,431 ni zaidi ya Sh. Bilioni
557.
Hadi sasa, tayari watu 47 wamekamatwa na Polisi kuhusiana na tuhuma
za kuhusika na ukwepaji kodi huo huku baadhi yao wakiwa tayari
wamefikishwa mahakamani kukabiliana na mashtaka ya uhujumu uchumi,
miongoni mwao wakiwa Ni maafisa wa vyeo vya juu TRA. Hatua kama hizi
zilizochukuliwa na serikali ya Magufuli ndani ya siku 32 hazikuwahi
kuonekana katika kipindi chote cha siku 1,825 (miaka mitano) ya serikali
iliyomaliza muda wake ikiwa na jumla ya mawaziri 55.
3. VIPIMO CT-SCAN, MRI MUHIMBILI
Licha ya serikali iliyokuwa na mawaziri 55 ya Rais Kikwete kufanya
kazi kubwa ya kununua mashine za vipimo vya CT-Scan na MRI, bado
havikuwa vikitimiza malengo ya kutumikia wananchi kwa asilimia mia moja
kwani muda mwingi zilikuwa mbovu. Hata hivyo, muda mfupi tu baada ya
kuingia madarakani, Rais Magufuli alivamia Muhimbili na kutangaza
maamuzi mazito ikiwa ni pamoja na kumuondoa Kaimu Mkurugenzi na kisha
kuamuru mashine hizo zitengenezwe. Hadi kufikia jana, vipimo vyote
viwili vilikuwa vikifanya kazi Muhimbili na kuwaondolea kero wananchi,
jambo lililokuwa likionekana kuwa haliwezekani kufanyika katika serikali
ya awamu iliyopita kwani licha ya ahadi kadhaa kuwahi kutolewa, bado
hakukuwa na mabadiliko makubwa.
4.POSHO KAMATI ZA BUNGE
Kwa uda mrefu kumekuwa na malalamiko juu ya matumizi mabaya ya
fedha za umma kwa kuwalipa posho wabunge hata katika vikao vya kazi zao
za kila siku, vikiwamo vya kamati kuhusiana na mashirika mbalimbali ya
umma. Katika siku zake 32, tayari Rais Magufuli kupitia Msajili wa
Hazina, Lawrance Mafuru, ameshatangaza kufutwa kwa posho za vikao vya
kamati za Bunge na hivyo kuokoa fedha ambazo sasa zinaweza kuelekezwa
katika maeneo mengine ya maendeleo. Hili lilishindikana katika serikali
ya awamu ya nne iliyokuwa na mawaziri 55.
5.GHARAMA SIKU YA UKIMWI, UHURU
Miongoni mwa maeneo yanayoligharimu taifa fedha nyingi ni sherehe, maadhimisho na pia sikukuu mbalimbali za mwaka.
Serikali ya Magufuli imeepuka gharama hizi baada ya kufutilia mbali
gharama za zaidi ya Sh. milioni 200 zilizokuwa zitumike katika
maadhimisho ya Siku ya Ukimwi mkoani Singida, zaidi ya Sh. bilioni
zikaokolewa kutoka katika madhimisho ya Siku ya Uhuru na kuelekezwa
katika kujenga barabara ya lami kutoka Mwenge hadi Morocco jijini Dar es
Salaam, fedha nyingine Sh. milioni 215 zikaokolewa kutoka katika
tafrija ya wabunge kujipongeza baada ya kuapishwa na kupelekwa kununulia
vitanda 300 vya wagonjwa Hospitali ya Muhimbili na pia mamilioni
mengine ya fedha yameokolewa na Rais Magufuli baada ya kufuta kadi za
krismasi na mwaka mpya za mwaka huu kwa fedha za umma. Hatua zote hizi
hazikuwahi kufanyika katika miaka mitano ya mawaziri 55 wa serikali
iliyomaliza muda wake Novemba 5.
6. SAFARI ZA NDANI
Mbali na kudhibiti safari za nje, Rais Magufuli na serikali yake
pia amedhibiti safari za ndani baada ya kuagiza kuwa vikao vyote vya
kikazi baina ya viongozi wa mikoa vifanywe kupitia teknolojia ya video
(video conference) na siyo kusafiri kutoka mkoa mmoja hadi mwingine au
kukodi kumbi za mikutano. Hili halikuonekana katika serikali iliyomaliza
muda wake.
7. MICHANGO SHULENI MARUFUKU
Hii ni moja ya ahadi za Rais Magufuli. Katika siku zake 32 akiwa
madarakani, tayari ameshaagiza utekelezaji wa jambo hili na sasa
wanafunzi wa darasa la kwanza watakaoanza mwezi ujao hawatakumbana na
rundo la michango na pia wa sekondari pia watasalimika dhidi ya ada na
michango. Kero hii ya michango kama ya ulinzi, jembe, madawati, kwanja,
uji, na mingineyo ilikuwa sugu katika serikali ya mawaziri 55
iliyomaliza muda wake.
WASOMI WANENA
Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma wa Chuo Cha Kumbukumbu ya Mtakatifu
Stefano Moshi (SMMUCo), Dk. Gasper Mpehongwa, anasema katika utawala wa
Rais Kikwete, ripoti zilikuwa zinatolewa kwa watendaji wa serikali
lakini haamini kwamba walikuwa wakizitendea haki.
Anasema utawala uliopita ulikuwa na baadhi ya viongozi ambao
walikuwa hawachukui maamuzi ya haraka na hilo lilikuwa na athari kubwa
katika utendaji.
“Mimi naamini Rais alikuwa akipewa summary (muhtasari) wa utendaji
kazi katika kila wizara, ila watendaji wake walikuwa wanamuangusha. Hata
hili suala la Kamishna wa TRA lingetokea enzi za utawala uliopita
lingechukua muda mrefu kuchukuliwa maamuzi. Hii ndiyo tofauti iliyopo,”
alisema Dk. Mpehongwa, akisisitiza kuwa aina ya utendaji kazi wa Rais
Magufuli na Kikwete ni tofauti na kueleza kuwa katika nchi kama
Tanzania, anachofanya Magufuli kwa kuchukua uamuzi wa haraka ndiyo
inayohitajika.
Alisema hata Rais Kikwete alipokuwa madarakani alikuwa anasema ana
majina ya wafanyabiashara wakubwa wa dawa za kulevya lakini hadi
anaondoka madarakani hakuwahi kuwataja wala kutangaza kuwa amewachukulia
hatua.
Mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Iringa (IUCo), Essau Ntabindi,
alisema kuna mambo mawili ambayo ana amini yanaweza kuwa yalitokea
katika utawala wa mawaziri 55 wa Rais Kikwete.
Anasema jambo la kwanza uwezekano kuwa mambo ambayo Rais Magufuli
anayafanya sasa, utawala uliopita wa Rais Kikwete ulikuwa hauyaoni ama
ulikuwa unayaona lakini ulishindwa kuchukua hatua za haraka.
Anasema Rais Magufuli ameweza kufanya kazi kubwa kwa kipindi kifupi
lakini ni lazima awe na Baraza la Mawaziri makini kwani hawezi kufanya
mambo yote peke yake.
“Kwa mfano Rais hawezi kujua wizi wa chaki shuleni unavyofanyika
au madudu katika halmashauri, lazima atahitaji wasaidizi,” alisema
Ntabindi.
Mkurugenzi Mkuu wa Sikika, Irenei Kiria, alisema mambo anayofanya
Rais Magufuli kwa sasa hayajawahi kutokea wala kufanywa hapo kabla.
Anasema Rais Magufuli amefanya kazi iliyowashinda mawaziri
waliokuwapo katika utawala wa Rais Kikwete na kwamba, hayo yanayofanyika
sasa ndiyo waliyokuwa wakiyataka wananchi.
“Kwakweli anayoyafanya sasa Rais Magufuli yameshitua hadi baadhi ya
watu wa chama chake kwa sababu sidhani kama walitarajia angeyafanya
haya,” alisema Kiria.
Anasema maouvu anayoyafichua Rais Magufuli kwa sasa yalikuwapo kwa
muda mrefu na viongozi walikuwa wanayaona lakini walikuwa hawayachukulii
hatua, mfano ni ufisadi na ukwepaji kodi bandarini ambao haukuwa jambo
la siri.
Mwenyekiti wa Wafanyabishara, Johnson Minja, alikuwa anawaeleza
wakuu wa TRA, Bandari na hata mawaziri wa serikali ya Rais Kikwete juu
ya namna wafanyabishara wakubwa wanavyokwepa kodi bandarini, lakini mara
zote alikuwa akipuuzwa.
CHANZO:
NIPASHE
Post a Comment