Bi.
Kasiga na Bw. Asante Melita kutoka Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro
wakiwa katika picha ya pamoja na Mtangazaji maarufu wa kipindi cha Good
Morning America Bi. Amy Robach.
===================================================
Shirika la Utangazaji la ABC News la nchini Marekani limefanikiwa
kurusha matangazo yake ya moja kwa moja
(live) kutokea Ngorongoro Crater kupitia kipindi chake maarufu cha “Good
Morning America.”
Matangazo hayo ambayo yamerushwa tarehe 23 Februari, 2016
yanatarajiwa kutazamwa na watu milioni 5 Jijini New York na zaidi ya watu
milioni 50 katika Marekani yote yanalenga kutangaza vivutio vya Utalii hapa
nchini hususan Bonde la Ngorongoro pamoja na kuelezea jitihada za Serikali ya
Tanzania katika uhifadhi wa mazingira na maliasili.
Akizungumza na Waandishi wa Habari kutokea Bonde la
Ngorongoro mara baada ya matangazo hayo kurushwa, Mwakilishi wa Serikali kutoka Wizara ya Maliasili na Utalii, Bw. Herman
Keraryo alisema kuwa kuna faida kubwa
kwa matangazo hayo kurushwa nchini Marekani kwani ni miongoni mwa nchi
zinazoongoza kwa kuleta Watalii hapa nchini. Pia matangazo hayo ni moja ya
jitihada za Serikali katika kukabiliana na changamoto za kutangaza utalii ambapo njia hii iliyotumiwa
na Shirika la ABC News ni nzuri kwani imefanikiwa kuwafikia watu wengi na kwa
muda mfupi.
Bw. Keraryo ambaye pia ni Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Wanyamapori, alisisitiza
umuhimu wa kuendelea kutunza mazingira na Wanyamapori ambao wameendelea kuwa
kivutio kikubwa cha utalii nchini.
“Kama mnavyojua utalii wa Tanzania bado unategemea wanyamapori kwa
kiasi kikubwa pamoja na kuwa na vivutio vingine Kama vile mambo ya kale lakini
bado wanyamapori wanatangaza zaidi utalii wetu hivyo ni wajibu wetu kuendelea
kuwatunza” alisema Bw. Keraryo.
Mbali na Bw. Keraryo wajumbe wengine kutoka Serikalini walioshuhudia
urushwaji wa matangazo hayo ni Dkt.
Freddy Manongi, Mhifadhi Mkuu wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, Bi. Mindi
Kasiga, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali na Msemaji wa Wizara
ya Mambo ya Nje, Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Kikanda na Kimataifa na Bi.
Devotha Mdachi, Mkurugenzi wa Masoko kutoka Bodi ya Utalii Tanzania (TTB).
Kwa upande wake, Mhifadhi Mkuu, Dkt. Manongi alisema kuwa anaishukuru
na kuipongeza Wizara ya Mambo ya Nje kupitia Ubalozi wake wa New York, Marekani
kwa jitihada za kulishawishi na kufanikisha shirika hilo la utangazaji kuja
nchini na kwamba ana imani utalii utaongezeka kufuatia matangazo hayo. Alisema kuwa Tanzania imepata fursa nzuri ya kujitangaza
bure kwa vile imekuwa ikutumia fedha nyingi kwa ajili ya kazi hiyo.
“Kitendo cha kuleta shirika la ABC News nchini kwa ajili ya kutangaza
utalii ni cha kujivunia na pia ni fursa kubwa sana kwetu Watanzania. Hivyo
napenda kuushukuru Ubalozi wetu New York kwani ninaamini kupitia matangazo haya
tutafaidika sana na tunatarajia baada ya miezi michache kupata watalii wengi
hususan hapa Ngorongoro” alieleza Dkt. Manongi.
Naye Bi. Kasiga, Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje
alieleza jitihada
zilizofanywa na Wizara kwa kushirikiana na Ubalozi wa Tanzania, New York pamoja
na Wizara na Taasisi mbalimbali za Serikali katika kufanikisha matangazo hayo
ya moja kwa moja. Aliongeza kwamba jitihada hizo zitaendelea ikiwemo kuzitumia Balozi zetu zilizopo nje katika kuhakikisha vivutio
vya utalii vya hapa nchini vinatangazwa duniani kote. Pia alitumia fursa hiyo
kutoa wito kwa Mashirika mengine makubwa ya utangazaji
duniani kuja nchini kutangaza vivutio hivyo.
Kwa upande wake Bi. Mdachi kutoka Bodi ya Utalii aliwaeleza waandishi wa habari kuwa Tanzania ina Mabalozi wa hiari wa
utalii watano nchini Marekani na kwamba matangazo hayo ya ABC News yatakuwa ni
nyenzo mojawapo itakayotumiwa na mabalozi hao kuendelea kuitangaza Tanzania.
Naye Mwakilishi wa Shirika la ABC News Bi. Farhoun aliishukuru Serikali ya Tanzania kwa kuwawezesha
kufanikisha matangazo hayo ambayo kwa namna moja au nyingine yataongeza
watazamaji wa kituo chao kwa vile walihakikisha ni wanyama pekee wanaooneshwa kwenye
matangazo hayo tangu mwanzo hadi mwisho.
Pia alisema kwamba wamevutiwa na hifadhi hiyo ya kipekee
duniani na kuipongeza Tanzania kwa jitihada
za utunzaji wa mazingira hususan Bonde la Ngorongoro na hawajutii uamuzi
wao wa kuichagua Ngorongoro kwa matangazo hayo.
-MWISHO-
|
Post a Comment