Mwenyekiti Freeman Mbowe akisalimiana na viongozi mbalimbali wa CHADEMA mkoa wa Mwanza waliofika kumlaki uwanja wa ndege
..................... 
Na Fredrick Katulanda, Mwanza
MWENYEKITI wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman 
Mbowe, amevunja ukimya na kusema atawasilisha jina makini la mrithi wa 
nafasi ya aliyekuwa Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Willibrod Slaa.
Akizungumza na MTANZANIA mjini hapa jana, baada ya kumalizika kikao 
cha kwanza cha Kamati Kuu, Mbowe alisema sifa za kiongozi anayepaswa 
kushika wadhifa huo zinafahamika.
Alisema wajumbe na wanachama wa Chadema watarajie kumpokea mtu makini
 ambaye jina lake atalipendekeza kisha kupigiwa kura na wajumbe wa 
Baraza Kuu kesho.
“Sifa za Katibu Mkuu zinajulikana, nawaomba wanachama na wajumbe 
kutulia, jina watakutana nalo ukumbuni muda ukifika… nina imani litakuwa
 jina la mtu makini,” alisema.
Mbowe alisema chama hicho kinakutana kwa mara ya kwanza tangu 
kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu wa Rais mwaka jana, hivyo wana mambo mengi 
ya kujadili, ikiwa ni pamoja na kupanga mikakati mipya ya kuwafikia 
wafuasi wao.
Katika hatua nyingine, chama hicho kimesema kitamtambulisha Katibu 
Mkuu mpya rasmi Jumapili wakati wa mkutano wa hadhara utakaofanyika 
viwanja wa Furahisha jijini hapa.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Ofisa Habari wa chama hicho,
 Tumaini Makene, alisema majina mawili yatawasilishwa katika Baraza Kuu 
litakalokaa usiku wa Jumamosi kwa ajili ya kupitisha jina moja.
Alisema majina yatakayowasilishwa hayatakuwa na uhusiano au urafiki wowote na Mwenyekiti Mbowe.
“Tayari viongozi wa kitaifa wamewasili Mwanza, Sekretarieti imekutana
 kwa ajili ya kuandaa ajenda ambazo zitajadiliwa na Kamati Kuu yenye 
wajumbe 36.
“Siku inayofuata Baraza Kuu litakaa usiku kwa ajili kumpata Katibu 
Mkuu, hii ni nafasi nyeti sana ndiyo maana hata wenzetu wa Chama Cha 
Mapinduzi (CCM) wanafuatilia kwa ukaribu kujua nani atapewa mikoba ya 
Dk. Willibrod Slaa.
CHANZO:MTANZANIA 

Post a Comment