Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

Je Van Persie kaharibu Arsenal

Robin Van Persie

Imeandikwa na Israel Saria

Kauli ya Robin van Persie kwamba hataongeza mkataba Arsenal haiwezi kutafsiriwa ililengwa kwa washabiki kama alivyodai, bali ni kwake mwenyewe.Ni muhimu kuweka mambo sawa; kwamba Van Persie amekwenda kinyume na matakwa ya kocha wake, mtu aliyemkuza, kumjenga na kumfikisha alipo leo.Kwa kuchapisha zile aya tano, japo fupi lakini zilizopangwa kwa kina katika tovuti yake binafsi, ni wazi kwamba Van Persie hawezi tena kubaki Arsenal.
Kwa msingi huo kuna moja tu linaloweza kufanyika. Van Persie amepata kile alichokitaka na atauzwa kipindi hiki cha kiangazi kwa atakayetoa dau kubwa zaidi, liwe linatoka Manchester City, Italia au Hispania, mwenye kisu kikali ndiye atakayekula nyama. Kwa upande wake, Robin Van Persie anaonekana amedhamiria kuondoka Arsenal haraka iwezekanavyo.
Mwendo wa saa 10.02 Julai 4 mwaka huu, thamani ya Van Persie kwenye soko la
uhamisho wa wacheza soka ambalo lina dau kubwa, alikuwa na thamani ya Pauni
milioni 25.

Lakini saa 10.03, alipojichapa kofi usoni, samahani, alipotoa kauli yake kwa
washabiki, thamani hiyo ilipungua kwa zaidi ya moja ya tano. Hakikuwa kitendo
cha mtu anayeonekana kuipenda klabu aliyomo.
Hakuna anayemwonea wivu kijana huyu wa Kiholanzi kwa kutaka kujitosa kutoka
kwenye meli aliyoiongoza vyema kwenye safari iliyokabiliwa na mawimbi na dhoruba
kali baharini msimu uliopita.
Robin yupo kwenye kilele cha uwezo wake, wakati ambao anaweza kuuzika na
kupata kitita kikubwa zaidi cha fedha katika maisha yake ya soka; na pia ni
wakati huu anapoweza kuamua aelekee wapi.
Hata hivyo, kinachogomba hapa ni njia anazotumia kupata hicho anachokitafuta
hatimaye.
Machoni mwa mashabiki wa Arsenal, hatachukuliwa kuwa na unafuu kuliko Samir
Nasri na Emmanuel Adebayor, wawili kati ya wachezaji wanne walio likimbia dimba
la Emirates na kwenda Etihad tangu mmiliki wa Manchester City, Mansour bin Zayed
Al Nahyan alipobadili sura ya soka kote barani Ulaya.
Wanasoka na mameneja wao wa masuala ya vyombo vya habari wanajua kuchagua
maneno, angalia tu mahojiano yanayofanyika baada ya mechi uone litania ya usanii
unaotumika:-
Ni kawaida kuwasikia wakisema; "suala si mimi, ni kwa ajili ya timu',
'tunajishughulisha na mechi moja kwa wakati' au 'kitu cha muhimu zaidi kilikuwa
zile pointi tatu'.
Kuna nyingine imeibuka siku hizi, ilitungwa na Wayne Rooney alipokuwa
akijaribu kujenga mazingira ya kuondoka Manchester United, ikaigwa na Luka
Modric alipoitikisa Tottenham miezi 12 iliyopita na sasa kunakshiwa na Van
Persie."Sikubaliani na mipango klabu inayojiwekea kwa ajili ya siku zijazo,"
ndiyo kauli mpya.
Tabia na utoaji kauli za aina hii si tu kwamba ni kulenga kudhoofisha klabu
na wachezaji ambao mmekuwa mkishirikiana siku zoye, bali pia ni kama njama
inayolenga kuwagonganisha washabiki na klabu yao, kucheza na hisia zao.
Inasemwa kwamba baada ya Kombe la Dunia la mwaka 2010, wakati Rafael van der
Vaart alikuwa akibezwa kote Ulaya baada ya kutofanya vyema kwenye klabu ya Real
Madrid, Mdhachi mwenzake alikuwa akigonga mlangoni mwa kocha, akimtaka achukue
hatua.
Ijapokuwa Van Persie anaweza kupongezwa kwa nia na tamaa yake, ni muhimu
kujiuliza zina athari gani kimaadili kwa wachezaji wa nafasi hiyo.
Mmoja wao ni Aaron Ramsey, ambaye bado hajajua mwelekeo wake baada ya
majeraha aliyopata baada ya kuvunjwa mguu na mlinzi wa Stoke City, Ryan
Shawcross miezi minne tu kabla.
Ama kwa upande wake, na kwa usahihi, Kocha Arsene Wenger alitazama hali ile,
lakini akaamua kutofanya lolote, hakusajili mchezaji kwenye namba hiyo, mambo
yakaonekana yameisha, kumbe bado kabisa. Van Persie tangu wakati huo ameendeleza
ndoto za ukubwa kwenye soka, akiendekeza 'umimi'.
Kipindi hiki cha majira ya joto, hajafurahishwa na kusajiliwa kwa mchezaji wa
kimataifa wa Ujerumani mwenye umri wa miaka 26, anayejivunia kucheza mechi zaidi
ya 100 na timu ya taifa lake.
Huyu ni Lukas Podolski, mmoja wa wachezaji wazuri zaidi wenye umri mdogo
katika Ulaya wanaocheza nafasi ya ushambuliaji wa kati.Hapo hujazungumzia
kuibuka kwa Alex Oxlade-Chamberlain kama mchezaji kamili wa kimataifa.
Kitu kinachoshangaza ni kwamba Van Persie mwenyewe alisajiliwa kama
Chamberlain tu.
Hebu tujiulize; kuibuliwa kwa kijana huyu wa Kidachi, enzi zile akiwa na umri
wa miaka 21 na tabia inayotia shaka kungeweza kuwashawishi akina Patrick Vieira
na wenzake kuhusu malengo ya klabu?
Endapo Iwe walikwazika na kusajiliwa kwake au la kwa sababu hizo au nyingine,
hatukusikia chochote kikisemwa hadharani.
Jambo muhimu hapa ni moja - Van Persie anataka kuondoka. Sawa. Lakini,
imekuwa tofauti kabisa na Cesc Fabregas aliyetulia kabisa wakati klabu
ikimshawishi kuhusu nia yake ya kurudi nyumbani Barcelona mwaka mmoja
uliopita.
Nahodha huyu mpya anatembeza kabali kati yake na klabu iliyomsaidia kwa kila
hali alipokabiliwa na masahibu ya majeruhi yasiyo mfano na pia akiwa kwenye
kiwango cha hovyo kabisa kisoka. Ana deni kubwa kwao kuliko aya tano alizoandika
kwenye tovuti yake.
Kaulimbiu ya Arsenal ni 'Victoria Concordia Crescit', yaani 'Ushindi Huja kwa
Amani', lakini kwa Van Persie kwa miaka kadhaa sasa amekuwa
haifuati.
Habari na http://www.bbc.co.uk/swahili
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top