na Josephat Isango
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM), kimewageuka wanachama wake
waliotumwa kufungua kesi za kupinga matokeo ya uchaguzi katika majimbo
mbalimbali nchini, Tanzania Daima Jumapili limebaini.
Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili, umebaini kuwa waliofungua kesi
kupinga ubunge wa Godbless Lema mkoani Arusha, wametoswa na sasa
wanakusudia kumwangukia mbunge huyo kumwomba radhi ili awasamehe deni la
uendeshaji wa kesi tangu mwanzo hadi juzi Mahakama ya Rufaa
ilipomrejeshea ubunge.
Baada ya Uchaguzi Mkuu mwaka 2010, CCM kupitia Katibu Mkuu wake, kwa
wakati huo, Yusuf Makamba, iliandika barua yenye kumbukumbu namba
CCM/OND/636/VOL.11/122 ya Novemba 9, 2010 kwenda kwa makatibu wake wa
mikoa na wilaya kuwaamuru wote walioshindwa katika uchaguzi wapinge
matokeo, na kwamba chama kingewasaidia gharama za uendeshaji wa kesi
hizo.
Katika barua hiyo, Makamba aliwataka wagombea wa ubunge kufungua kesi
katika Mahakama Kuu ya Tanzania, huku wagombea udiwani walioangushwa
kufungua kesi katika mahakama za mahakimu wakazi ndani ya siku 30, tangu
ulipofanyika uchaguzi huo.
Katika barua hiyo ambayo Tanzania Daima Jumapili ina nakala yake,
Makamba aliwaagiza makatibu wa CCM wa mikoa kwa kushirikiana na makatibu
wa wilaya na kata kuwasaidia wagombea walioshindwa kwenye uchaguzi
kuandaa hoja za malalamiko na vielelezo kwa ajili ya kupeleka
mahakamani, huku akisisitiza kuwa “Chama Cha Mapinduzi Makao Makuu
kitachangia gharama za mawakili kwa wagombea ambao hawana uwezo
kifedha.”
Baadhi ya wabunge wa upinzani walioshitakiwa na kesi zao kuhukumiwa na
kuibuka kidedea, hawajalipwa gharama za uendeshaji wa kesi hizo.
Mbunge wa Mbozi Magharibi, David Silinde (CHADEMA) kupitia kwa wakili
wake, Benjamin Mwakagamba wa Kampuni ya uwakili ya BM ya jijini Dar es
Salaam, alisema kuwa, mdaiwa katika kesi hiyo, Dk. Lucas Siame (CCM)
tangu aamriwe na mahakama kulipa, amekuwa haonekani mahakamani au
kuonesha dalili zozote za kulipa gharama za uendeshaji wa kesi.
Wakili huyo anasema kuwa, mdaiwa huyo ambaye alipinga matokeo, amekuwa
akiishi kwa kujificha maeneno ya Sinza, jijini Dar es Salaam.
Tanzania Daima Jumapili lilimtafuta Dk. Siyame kupitia simu yake ya
mkononi akapatikana, ila alisema hajui utaratibu kama alipaswa kulipa au
la.
“Mwandishi hizo habari za kulipa ndio nazisikia kwako,” alisema lakini
alikiri kuwa CCM haikumsaidia uendeshaji wa kesi aliyofungua dhidi ya
Silinde.
Silinde, alishinda kesi katika Mahakama Kuu ya Rufaa Kanda ya Mbeya,
baada ya kufuta shauri la kesi ya rufaa iliyopelekwa na Siame, aliyekuwa
mgombea wa CCM, Mei 2, mwaka huu.
Siame aliyekuwa amekata rufaa kupinga hukumu iliyotolewa Julai mosi,
mwaka jana dhidi ya uamuzi wa Mahakama Kuu uliompa ushindi mbunge huyo
wa CHADEMA, alilazimika kuomba mahakama kuondoa shauri hilo.
Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’
(CHADEMA) ambaye naye alishinda kesi ya pingamizi iliyofunguliwa na
Benson Mpesya (CCM), alipoulizwa endapo amelipwa fidia kama ilivyoamriwa
na mahakama, alisema kuwa amelipwa sehemu ya fedha, na nyingine bado.
Sugu alisema kuwa, hata hivyo Mpesya amekuwa akimtuma wakili wake kuonana na wa kwake ili angalau amwongezee muda wa kulipa.
“Nimekuwa mstaarabu sana, ningeweza kutafuta amri ya mahakama ili mali
zake zikamatwe, lakini alimtuma wakili wake nimvumilie,” alisema
Mbilinyi.
Wakati mzigo wa kulipa gharama ukiwaangukia wafungua kesi, waliomshtaki
Mbunge wa Singida Mjini, Tundu Lissu (CHADEMA) wanatafuta suluhu.
Walalamikaji wawili waliokata rufaa dhidi ya Lissu, ambao kesi yao bado
haijaanza kusikilizwa, tayari wameshaanza kumtafuta mbunge huyo ili
wafanye utaratibu wa kuondoa kesi Mahakama ya Rufaa.
Akizungumza kwa simu kutoka Muyanji-Makiungu, Singida, mlalamikaji wa
kwanza katika kesi hiyo, Shabani Selema alisema: “Natamani sana kuiondoa
kesi hiyo mahakamani ambayo Chama chetu Cha Mapinduzi kilishinikiza
tukate rufaa, lakini kwa sasa chama hakieleweki, sina haja tena na hiyo
kesi, sitaki na ninataka kwenda Dodoma nionane na wakili wetu angalau
nichukue hata kitambulisho changu cha mpiga kura kwani kilikuwa ni
sehemu ya vielelezo, mimi nakuahidi kuwa nakuja Dar es Salaam wakati
wowote na nitamtafuta Lissu tukafute hiyo kesi.”
Alipohojiwa inakuwaje ajitoe katika hatua hii ya rufaa, Selema alijibu:
“Mwandishi kama kuandika andika tu, mimi hii kesi sina hamu nayo,
nimekuwa naiendesha mwenyewe, hata familia yangu, rafiki zangu na wasomi
mbalimbali sasa wananishangaa, chama kimeniacha, kwanza wamenivuruga
sana.”
Kwa upande wake, Lissu alisema taarifa kwamba mlalamikaji wake
anamtafuta ili wafute kesi, amezisikia kutoka kwa wanafamilia yake.
Tanzania Daima Jumapili iliwatafuta viongozi wa CCM Makao Makuu
kuzungumzia suala hilo, lakini simu zao hazikuweza kupatikana hewani
huku simu ya Naibu Katibu Mkuu bara, ikiita muda wote bila kupokelewa.
Kwa upande wake Katibu wa CCM Mkoa wa Arusha, Mary Chatanda alipopigiwa
simu hakuweza kupokea, lakini baadaye alimpigia mwandishi na kumuuliza:
“wewe nani?”
Mwandishi alipojitambulisha kwamba anatoka Tanzania Daima Jumapili,
Chatanda alisema: “Kama wewe ni wa Tanzania Daima, nipigie sina haja ya
kukupigia.”
Baada ya kusema hayo akakata simu, na alipopigiwa tena, simu ilikuwa tayari imefungwa - haikupatikana tena.
NA TANZANIA DAIMA
Post a Comment