MWAKA 1951 nchi ya kwanza Afrika
ilipata uhuru na kufikia mwaka 1966, nchi karibu zote zilipata uhuru
isipokuwa sita tu. Kwa maana hiyo, si vibaya kusema Bara la Afrika kwa
wastani liko kwenye miaka ya 50 ya uhuru wake kutoka kwa wakoloni.
Kipindi hiki cha miaka 50 ya uhuru Afrika kinakwenda sambamba na miaka
50 ya watu wa rangi hasa weusi nchini Marekani, kuwa na haki kamili za
kiraia (civil rights) baada ya kupitishwa sheria ya haki za kiraia
(civil rights act), mwaka 1964 na ile ya haki ya kupiga kura (voting
rights act) mwaka 1965.
Sheria hizi mbili ziliondosha kabisa sheria za kibaguzi zilizojulikana
kama Jim Crow; sheria zilizokuwa zikitenganisha wazungu na jamii
nyingine hasa weusi, kwa kila nyanja za maisha yao mfano shule za weupe
na weusi, sehemu za kukaa kwenye mabasi (weusi walitakiwa kukaa nyuma na
kukaa mbele ilikuwa kosa kisheria) na pia katika makazi.
Sheria za kibaguzi za Jim Crow ndiyo zilizopingwa na Martin Luther King,
hadi kuawa kwake mwaka 1968, King alitaka watu wote bila kujali rangi
wawe na haki sawa nchini Marekani, lakini Marcus Garvey na Malcom X
walikuwa na maoni tofauti.
Ingawa Malcom X alikuwa akibadili mtazamo kulingana na mwenendo wa
wakati, yeye na Marcus Garvey kwa nyakati tofauti walitaka weusi wawe na
nchi yao, kwa maana taifa la weusi iwe kurudishwa Afrika au kupewa
sehemu ya Marekani waanzishe taifa la weusi.
Madhumuni ya Marcus Garvey na Malcom X kutaka sheria za kibaguzi ni
kuonyesha kwamba watu weusi wanavipawa au akili kama Wazungu.
Waliamini kabisa kwamba weusi wakiwa na taifa lao, wataweza kuwa na
misingi mizuri ya kidemokrasia, kujitawala, kufanya biashara na mambo
mengine mengi tu yanayohusu maisha ya mwanadamu.
Marcus Garey alizaliwa mwaka 1887 nchini Jamaica na kufariki mwaka 1940
jijini London, Uingereza. Aliendeleza harakati za kudai haki za weusi
kutoka kwa weusi waliomtangulia kama Prince Hall, Martin Delany na
Edward W. Blyden kwa kujikita zaidi kwenye falsafa ya Pan-Africanism
(umajumui wa Afrika); itikadi na vuguvugu kuhimiza umoja wa watu weusi
duniani.
Aliongoza harakati zake za ukombozi wa weusi kwa kutia hamasa ya weusi popote duniani kurudi barani Afrika liliko chimbuko lao.
Pia alihimiza uwezeshaji wa weusi kiuchumi kwa vitendo, baada ya
kuhimiza weusi kuanzisha kampuni ya meli ya weusi iliyoitwa Black Star
Line na gazeti la kila wiki lililojulikana kama Negro World lililopigwa
marufuku na wakoloni kuingizwa katika makoloni yao Afrika.
Ni katika gazeti hilo la kila wiki la Negro World, Marcus Garvey aliweza
kuandika na kuchapisha makala kuhimiza juu ya umoja wa watu weusi
popote pale duniani.
Moja ya makala aliyoandika kwenye Negro World juu ya umoja wa weusi ni
ile iliyokuwa na kichwa cha habari “African Fundamentalism”, moja ya
nukuu kutoka kwenye makala hiyo ni “Our union must know no clime,
boundary, or nationality; let us hold together under all climes and in
every country…”, kwa tafsiri isiyo rasmi; “Umoja wetu usiangalie pande
gani ya dunia, mipaka au utaifa bali tufungamane kutoka pande zote za
dunia na katika kila nchi.”
Makala nyingine alizoandika ni kama “Society and The Selfish Exploiter”,
hii ni makala iliyohusu unyonyaji na kuwaita watu wanaodhulumu wanyonge
kuwa wahalifu zaidi ya wauaji.
Vilevile katika harakati za kupinga ukoloni uliokuwa ukiendelea Afrika,
Marcus Garvey alitoa hotuba ya kusisimua kwa weusi waliojumuika kwenye
ukumbi wa Liberty (Liberty hall), New York mwaka 1921 na kuipa kichwa;
“Africa For The Africans”, nitatoa baadhi ya nukuu kutoka kwenye hotuba
hiyo sambamba na tafsiri isiyo rasmi:
“Say! Africa for the Africans,
Like America for the Americans:
This the rallying cry for a nation,
Be it in peace or revolution.
Blacks are men, no longer cringing fools;
They demand a place, not like weak tools;
But among the world of nations great
They demand a free self-governing state”.
“Sema! Afrika kwa Waafrika.
Kama Marekani kwa Wamarekani:
Hiki ni kilio cha kudai taifa,
Iwe ni kwa amani au kwa mapinduzi.
Weusi ni binadamu, sio tena wajinga;
Wanadai sehemu, wao sio dhana dhaifu;
Bali kati ya mojawapo ya mataifa duniani,
Wanadai taifa huru linalojitawala”
Ndugu zangu, hayo ni maneno ya Marcus Garvey miaka 30 kabla nchi ya
kwanza Afrika ipate uhuru na miaka 45 kabla karibu kila nchi Afrika
ipate uhuru, isipokuwa nchi sita tu.
Miaka 11 baada ya kifo chake nchi ya kwanza Afrika ilipata uhuru na
miaka 26 baada ya kifo chake, nchi karibu zote zilipata uhuru. Hivyo
harakati zake japo za kutaka weusi kuachiwa Afrika zilikamilika akiwa
tayari ameiaga dunia, kwa bahati mbaya pia alikuwa amefariki kabla ya
kukanyaga ardhi ya Afrika.
Kwa upande wa Malcom X, yeye mpaka kuawa kwake mwaka 1965, karibu nchi nyingi za Afrika zilikuwa zimepata uhuru.
Aliuawa takribani miezi sita kabla ya Wamarekani weusi kuwa na haki sawa
za kiraia kwa kupitisha sheria ya mwisho ya haki ya kupiga kura (voting
rights act). Kama nilivyosema mwanzoni, Malcom X alikuwa akibadilika
kiasi kwenye mitizamo yake kadiri muda ulivyokuwa unakwenda lakini bado
msimamo wake ulikuwa wa kuhimiza utengano wa weusi na wazungu, kwa maana
na weusi kuwa na taifa lao.
Aliendelea kudai kwamba kwa muda wa zaidi ya miaka 400 ya mateso ya
weusi nchini Marekani, basi Marekani igharimie usafiri wa watu weusi
kurudi Afrika au wapewe ardhi sehemu ya Marekani waanzishe taifa la
weusi na waweze kuonyesha uwezo wao kwamba ni binadamu kama wengine,
wanaweza kujitawala, kufanya biashara na mambo mengine.
Pia aliendelea kupinga juu ya Marekani kuingilia mambo ya nchi za Afrika
na hii inajionyesha pale baada ya kuawa Rais Kennedy, wa Marekani
wakati huo siku iliyofuata kiongozi wake mkuu wa kundi la Kiislam la
Nation of Islam, alimsihi kutozungumzia kabisa mambo yanayohusu Rais
Kennedy kesho yako kwenye mkutano.
Lakini alipoulizwa swali na mwandishi kuhusu kuawa kwa Rais Kennedy,
baada ya kumaliza hotuba yake, Malcom hakuonyesha kushangaa kwani
alisema hayo ni malipo juu ya machafuko yanayosababishwa na Marekani
duniani kote, na mnukuu hapa “Being an old farm boy myself, chickens
coming home to roost never did make me sad, they have always made me
glad.” Aliendelea kudai kwamba Rais Kennedy ndiye aliagiza kuuawa kwa
Waziri Mkuu wa Congo, Patrick Lumumba. Malcom X alisimamishwa kufanya
kazi za kundi hilo la Nation of Islam kwa siku 90, lakini hakurudi tena
na alianzisha kundi lake na kuuawa mwaka mmoja baadaye.
Wote Marcus Garvey na Malcom X walikuwa na shauku ya kuona Waafrika
wakijitawala na kuonyesha dunia kwamba weusi wanauwezo mkubwa wa
kujitawala na ni binadamu kama binadamu wengine.
Kwa sasa ni miaka zaidi ya 50 tangu Bara la Afrika lianze kujitawala na
naweza kusema itikadi za hawa magwiji kutaka Waafrika wajitawale
zimejaribiwa ila swali je, tumeweza kujitawala kwa misingi bora ya
demokrasia, utawala bora, kuondoa baa la njaa kila mara na kuacha
utegemezi?
Ni nchi gani Afrika ambayo sio tegemezi? Hata zile zenye rasilimali
zaidi ya nchi ya Italia, kama Tanzania bado zinategemea misaada kutoka
kwa wakoloni (siku hizi mnawaita wafadhili).
Swali ambalo wengi tutakuwa tunajihuliza ni; je, kweli juhudi zote
zilizofanywa na kundi hili la wapigania haki za watu weusi wakiwa na
lengo la kuhahakikisha Mwafrika anapoachiwa ajitawale ataonyesha uwezo
wake, zimefanikiwa?
Malengo yao ya kutaka mtu mweusi awe na taifa lake huru aonyeshe vipawa
vyake vyote alivyopewa na Mwenyezi Mungu, yametimia? Bara la Afrika
linatawaliwa na weusi kwa zaidi ya miaka 50, hivi kweli tumeweza
kuonyesha uwezo wa mweusi kuudhihirishia Ulimwengu wa wazungu kwamba
ndiyo tumeweza? Au ni kauli mbiu tu za kila mara kwamba tumedhubutu,
tumeweza, tunasonga mbele?
Je, leo Marcus Garvey na Malcom X wakifufuka, wataweza kuwabeza wazungu
kwamba si mnaona tuliwaambia mkiacha tujitawale tutaonyesha kwamba sisi
ni binadamu kama nyie na uwezo tunao, na tangu mtuache weusi tuwe na
nchi zetu huru haya ndiyo maendeleo tuliyonayo.
Au wazungu ndiyo watakaowabeza akina Garvey na Malcom kwamba tulijua
weusi hawawezi kujitawala, kwa miaka zaidi ya hamsini tuwape Bara lenu
bado mnatutegemea kwa kila kitu, mmeshindwa kuwalisha watu wenu,
mnagombana wenyewe kwa wenyewe.
Nikifikiria Bara la Afrika lilipo kwa sasa, ni kwamba ndoto zote za hao
magwiji wa haki za weusi hazijatimia kwa maana ya kuonyesha uwezo na
kuweka heshima kwa mweusi katika nchi huru anayoitawala.
Bara la Afrika halijaweza kuonyesha thamani halisi ya Mwafrika na kuonyesha uwezo wa Mwafrika, huo ndiyo ukweli.
Haya ndiyo yaliyokuwa malengo ya akina Garvey na Malcom na weusi wengine
waliokuwa utumwani, kujenga heshima ya mtu mweusi kwa kuonyesha uwezo
katika nchi huru anayoitawala. Mwonekano uko wazi, bado taifa ni
tegemezi.
Swala hili si kwa Marcus Garvey na Malcom X au jamii ya Wamarekani weusi
tu waliokuwa na mtizamo kama wao bali ni kwa Waafrika ndani ya Bara la
Afrika, waliokuwa na mitizamo kama hiyo, mfano, Kwame Nkrumah wa Ghana,
Mwalimu Julius Nyerere wa Tanzania, Thomas Sankara wa Burkina Faso na
Samora Machel wa Msumbiji, mlolongo ni mrefu wa Waafrika wenzetu
waliojitoa kwa ajili ya Bara letu lakini hawako nasi kuona mwelekeo wa
Bara hili na kuzidi kupotea kwa heshima ya mtu mweusi waliyokuwa
wakiipigania na kuijenga, enzi zao.
Tunabaki tu na maswali kama wakifufuka iwe kwa wale waliopata uhuru kwa
amani au mapinduzi pengine wakapewa nafasi ya mdahalo kama waliokuwa nao
kipindi wakidai uhuru kutoka kwa wakoloni ni hoja hizi zipi wataingia
nazo kutetea uhuru wa Mwafrika baada ya miaka 50? Je ni hoja kwamba
binadamu wote ni sawa?
Ndio, inawezekana tuko sawa, watasema tuliwapa nchi zenu mzitawale, na
je, uwezo wa kujitawala kwa ufanisi tumeuonyesha au bado ni mtindo ule
ule wa kuwalaumu wazungu?
Kila mwaka tarehe ya kuadhimishwa uhuru inapofika kwa kila nchi Afrika, mbwembwe ni nyingi, sambamba na sherehe za gharama.
Sina hakika kama viongozi wetu huwashirikisha wananchi kutafakari
madhumuni ya wapigania huru wetu na hadhi ya Mwaafrika ulimwenguni. Au
ni mtindo ule wa kunywa mvinyo na kuthamini kuwapo kwao madarakani,
kufurahia fursa za kukutana na marais au mawaziri wa nchi za kizungu na
kupigiwa mizinga na kuandaliwa tafrija ughaibuni katika Ikulu za
wenzetu. Je, hayo ndiyo yaliyokuwa madhumuni ya kudai uhuru?
Kwamba mtu mweusi anapigiwa mizinga ya urais Marekani na Uingereza,
inawezekana rais huyo kutoka Afrika akaona hiyo ndiyo heshima na
ukombozi kwa Mwafrika.
Ni hapo rais kutoka Afrika anapoulizwa kwa nini nchi yako ni masikini
anajibu kwamba hata yeye haelewi ni kwa nini. Sasa kama rais haelewi na
anakaa madarakani kwa miaka 10, inawezekana katika miaka 50 ya uhuru
basi toa miaka 10, jibu utapata miaka 40 ya uhuru, na kama mtangulizi
wake alikuwa haelewi basi toa tena miaka 10 unapata miaka 30 ya uhuru.
Kwa mtindo huu, kama watawala wetu hawaelewi kwa nini Bara letu bado ni
masikini, ukitoa miaka yao katika miaka 50 ya uhuru wa Afrika
inawezekana Bara letu likawa bado haliko huru; linaitaji wakombozi wapya
wanaotambua kwa nini hili Bara ni masikini mbali na kujaaliwa
rasilimali lukuki, wakombozi watakaoweza kutimiza malengo ya wapigania
uhuru na haki za mtu mweusi popote pale dunia.
Ninatambua kwamba wako watu weusi wengi walioonyesha uwezo katika
masuala mbalimbali kama uongozi, michezo, taaluma, lakini wachache hao
hawawezi kuchukuliwa kama mfano kuonyesha kwamba weusi tumethubutu na
tumeweza.
Heshima ya Mwafrika iko kwenye kuliendeleza Bara la Afrika, kukomesha
majanga ya njaa ya kila mara na vita ya wenyewe, pia kuonyesha ukomavu
wa demokrasia.
Hata hao wachache kwenye medani ya michezo wameonyesha uwezo wao nje ya
Bara la Afrika na hii inaonyesha kwamba kama Bara tumeshindwa kuwa na
mipango madhubuti kujiendeleza kimichezo, na hili si michezo tu hata
kwenye taaluma.
Kwa upande wa uongozi wale waliothubutu kuonyesha uwezo wa kiuongozi
kama Thomas Sankara wa Burkina Faso waliishia kuawa na Waafrika wenzao.
Je, kweli tumeweza kuonyesha kwamba Afrika huru imefikia au inaelekea
kufikia malengo ya kutaka kujitawala kwa miaka hamsini ya uhuru wake na
kuweka heshima ya mtu mweusi popote pale duniani?
Mwandishi wa makala haya,
Mshobozi Kamugisha, ni msomaji wa Raia Mwema aliyeko North Carolina,
Marekani. Anapatikana kwa namba ya simu; +19195368526 na baruapepe;
klmu9@yahoo.com
Post a Comment