PATA TAARIFA KAMILI:
Release No. 024
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Februari 7, 2013
MAWAKILI RUKSA RUFANI ZA UCHAGUZI TFF
WAOMBAJI uongozi kuwania nafasi
mbalimbali katika uchaguzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania
(TFF) na Bodi ya Ligi Kuu (TPL Board) waliokata rufani kupinga
kuenguliwa kwenye kinyang’anyiro hicho wanaruhusiwa kuwa na uwakilishi
wa kisheria (legal representation) wakati wa kusikilizwa rufani zao.
Uamuzi wa kuruhusu mawakili kwenye
usikilizaji wa rufani hizo mbele ya Kamati ya Rufani ya Uchaguzi ya TFF
inayoongozwa na Idd Mtiginjola ni kuhakikisha kila upande unapata haki.
Pia Kamati ya Uchaguzi ya TFF ambayo
ndiyo iliyosaili waombaji uongozi, hivyo kuwa mlalamikiwa katika rufani
hizo, nayo inaruhusiwa kuwa na Wakili wakati wa usikilizaji wa rufani
hizo.
Kamati ya Uchaguzi ya TFF iliwaengua
waombaji kumi na mbili wa uongozi kwenye nafasi mbalimbali katika
uchaguzi huo utakaofanyika Februari 24 mwaka huu jijini Dar es Salaam
kwa kutokidhi matakwa ya kikatiba. Uchaguzi wa TPL Board utafanyika
Februari 22 mwaka huu jijini Dar es Salaam.
Waombaji hao waliochujwa ni Omari Mussa
Nkwarulo aliyeomba kuwania urais na Michael Richard Wambura aliyejitosa
katika kinyang’anyiro cha nafasi ya Makamu wa Rais.
Wengine waliochujwa wakiomba kugombea
nafasi ya ujumbe wa Kamati ya Utendaji ni Abdallah Hussein Musa, Mbasha
Matutu, Charles Mugondo, Ayubu Nyaulingo, Nazarius Kilungeja, Eliud
Peter Mvella, Farid Nahdi, Omari Isack Abdulkadir na Shafii Kajuna
Dauda.
Kwa upande wa uchaguzi wa Bodi ya Ligi
Kuu aliyechujwa ni Christopher Peter Lunkombe aliyekuwa akiomba nafasi
ya ujumbe katika Kamati ya Uendeshaji.
Mwisho wa kukata rufani kwa waombaji
uongozi walioenguliwa na wale walioweka pingamizi kwa wagombea na
zikatupwa ni leo (Februari 7 mwaka huu) saa 10 kamili jioni.
MECHI YA STARS, CAMEROON YAINGIZA MIL 148/-
Pambano la kirafiki la kimataifa kati ya
Tanzania (Taifa Stars) na Cameroon (Indomitable Lions) lililochezwa
jana (Februari 6 mwaka huu) na wenyeji Stars kuibuka na ushindi wa bao
1-0 limeingiza sh. 148,144,000.
Fedha hizo zimepatikana kutokana na
watazamaji 23,092 waliokata tiketi kushuhudia mechi hiyo kwa kiingilio
cha sh. 5,000, sh. 7,000, sh. 10,000, sh. 20,000 na sh. 30,000.
Mgawanyo wa mapato hayo ulikuwa kama
ifuatavyo; asilimia 18 ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ni sh.
22,598,237.29, maandalizi ya mchezo sh. 58,000,000 wakati wa gharama za
uchapaji tiketi ni sh. 7,340,900.
Nyingine ni bonasi kwa wachezaji wa
Taifa Stars sh. 18,831,864.41, asilimia 20 ya gharama za mchezo sh.
8,274,659.66, asilimia 15 ya uwanja sh. 6,205,994.75 na asilimia 5 ya
Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) sh. 2,068,664.92.
Asilimia 60 ya Shirikisho la Mpira wa
Miguu Tanzania (TFF) sh. 24,823,978.98 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa
wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 1,241,199 ambayo ni asilimia 5 kutoka kwenye
mgawo wa TFF.
Boniface Wambura
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)
Post a Comment