MWENENDO wa mambo ndani ya Baraza la Vijana la Chama cha Demokrasia
na Maendeleo (BAVICHA) unaendelea kuwa tete, kutokana na vita ya makundi
yanayotofautiana kimsimamo na kimtizamo kuendelea kushika kasi,
Mwenyekiti wa Baraza hilo, John Heche, alipotangaza kuwatimua kundini
baadhi ya wanachama, akiwemo Makamu Mwenyekiti wake, Juliana Shonza.
Uamuzi huo uliotangazwa na Heche unapingwa na Shonza, ambaye amekuwa akieleza kuwa yeye bado ni Makamu Mwenyekiti wa BAVICHA na kwamba anaendelea na shughuli zake za kiuongozi ndani ya jumuiya hiyo kama kawaida, kwa sababu taratibu za kumtimua zilikuwa batili.
Ili kupata msimamo wa Shonza kuhusu hatma yake ya kisiasa baada ya
tangazo la kutimuliwa kwake, Mtanzania Jumatano limefanya naye mahojiano
ya ana kwa ana ambapo alisisitiza kauli yake hiyo na kutumia fursa hiyo
ya mahojiano kutangaza kuwa atawania uenyekiti wa BAVICHA katika
uchaguzi ujao wa viongozi wa Jumuiya za Chadema.
Sambamba na hilo, Shonza pia alitangaza kuwa ni mfuasi wa Zitto
kisiasa na kwamba atamuunga mkono iwapo atatekeleza uamuzi wake wa
kuomba kuteuliwa na Chadema kuwa mgombea wake wa urais katika uchaguzi
mkuu wa mwaka 2015.
Mtanzania Jumatano: Umevuliwa uongozi wa BAVICHA. Ukiwa nje ya
BAVICHA, unautizamaje mwenendo wako wa kisiasa ukilinganisha na
ulipokuwa kiongozi?
Shonza: Mimi siko nje ya Bavicha, mnakosea sana kuamini hivyo. Naomba
nieleweke vizuri kwamba mimi bado ni Makamu Mwenyekiti wa Bavicha kwa
sababu niliwekwa kwa misingi ya Katiba na misingi ya Katiba pekee ndiyo
inayoweza kuniondoa.
Kiongozi aliyechaguliwa kikatiba hawezi kuondolewa kwa matakwa ya mtu
kama Wegesa Suguta, anayetumika kama daraja la mabosi wake kutekeleza
matakwa yao na ndiyo maana hata kushinda kwake alishinda kimagumashi.
Aliwekwa hapo kwa nguvu ili awatumikie waliomuweka badala ya Jumuiya ya
vijana na chama kwa ujumla.
Mtanzania Jumatano: Jina hili la Wegesa Suguta ni geni katika safu za
uongozi wa Chadema kwa ujumla, hapa unamaanisha ni nani huyu na ana
nafasi
gani ndani ya Bavicha au Chadema?
Shonza: Ni huyo ambaye nyie mnamwita John Heche.
Mtanzania Jumatano: Hili ni jina lake halisi au umembatiza wewe?
Shonza: Mimi nadhani swali hilo aulizwe yeye mwenyewe. Muulizeni hilo
la John Heche kalipata wapi? Mimi namjua kwa jina la Wegesa Suguta
ambalo liko kwenye vyeti vyake. Nawaachia kazi hiyo.
Mtanzania Jumatano: Unasema wewe bado ni Makamu Mwenyekiti wa
Bavicha, unamaanisha Heche alikosea kutoa tamko la kukuondoa madarakani
na kukufukuza uanachama?
Shonza: Ndiyo, na hili liko wazi kabisa. Siyo siri kwamba Wegesa
(Heche) anaonekana ana sauti sana ndani ya Baraza kwa sababu kuna vinara
ndani ya chama ambao wako nyuma yake na hawa ndiyo waliomuweka hapo
alipo ili awatumikie na kutimiza matakwa yao.
Na ndiyo maana unapozungumzia udhaifu wa Wegesa (Heche) hutaacha
kumuelezea kwamba ni kiongozi aliyeshindwa kuwaunganisha vijana ndani ya
baraza na vijana ndani ya chama wanafahamu hili.
Wegesa (Heche) ana uwezo mdogo wa kiuongozi unaomfanya achukue
maamuzi yasiyofuata Katiba ya chama na mwongozo wa baraza. Katika
mazingira kama hayo, tegemea kuungwa mkono na watu wasiojitambua lakini
kwa watu wanaojitambua ni ngumu kumuunga mkono Wegesa (Heche).
Hata historia inamhukumu kwani katika uchaguzi wa mwaka 2009 wa
Bavicha aligombea akagalagazwa vibaya na David Kafulila, lakini kutokana
na ukweli kwamba Kafulila hakuwa chagua la viongozi wakuu ndani ya
chama kwa sababu misimamo yake thabiti na uwezo alionao, uchaguzi ule
ukavurugwa na Kafulila akaambulia kufukuzwa.
Uchaguzi huo baada ya kuingia ‘kidudumtu’ uliitishwa tena mwaka 2011
na Wegesa (Heche) aliyekuwa akipiganiwa na vigogo wa chama alishinda kwa
mbinde sana baada ya vijana watatu ambao ni Mtela Mwampamba, Habib
Mchange na Nyakarungu wenye uwezo kuondolewa, achana na Ben Saanane
aliyeenguliwa kimkakati, lakini bado Wegesa (Heche) alishinda kwa
asilimia 51 tu.
Mtanzania Jumatano: Kwa hiyo wewe ni kiongozi unayeongoza kundi lipi? Maana Bavicha imeshatangaza haikutambui.
Shonza: Mimi ni kiongozi, kama yupo anayesema hanitambui basi huyo ni
Wegesa (Heche) na wenzake wanaoogopa changamoto mpya ndani ya chama na
kiongozi ni yule anayetambulika kikatiba, sawa! Mimi natambulika
kikatiba, alisema nimeondolewa alikiuka misingi ya Katiba, kwa hiyo
sitishwi na maneno ya vibaraka wa aina ya Wegesa (Heche) kwamba eti mimi
Shonza si mwanachama au kiongozi. Thats nonsense.
Na ndiyo maana viongozi wenye kujua misingi ya kikatiba huko mikoani
wananitambua kama kiongozi wao, bado nashirikiana nao na sitaacha
kushirikiana nao. Tunajenga chama, hatutaki majungu sisi wala
kufukuzana, kisa hofu inayotokana na uwezo mdogo wa kiuongozi unaomfanya
mhusika kuhofia kupokwa cheo alichonacho.
Mtanzania Jumatano: Zipo tuhuma kwamba ulishiriki kuanzisha Chama cha
Ukombozi wa Umma (Chauma) na pia ni mshirika wa makundi ya Masalia na
PM7-pindua Mbowe, tuhuma hizi unazizungumziaje?
Shonza: Nilishasema tangu awali na hata kwenye tamko langu nililisema
hili kwamba mpaka sasa sizifahamu tuhuma zangu. Siwezi jibu tuhuma
zilizotolewa na kiongozi ‘kilaza’ kwenye magazeti, kwani nami
nitadhihirisha kuwa ni kilaza kama yeye au wao maana chama kina
utaratibu wake wa kuwasilishiana tuhuma kwa viongozi na wanachama wake.
Na ndiyo maana hata wao wameogopa kuniandikia hizo tuhuma maana
wanajua fika kuwa ni za uongo, uzushi na uzandiki mtupu. Hata huo
ushahidi wanaosema wanao ni uongo na kujijaza upepo tu sawa na kupiga
ngoma na kucheza mwenyewe. Wamezoea kuwadanganya Watanzania kwamba wana
ushahidi, wana ushahidi wakati hawana chochote, wanacheza na akili za
watu ili tu waaminiwe upesi.
Mimi ninawaomba waache tabia ya kuwadanganya wananchi kwamba wana
ushahidi, sijui intelijensia kumbe wanapeleka majungu na umbea tu. Ni
aibu kuwa na kiongozi mpika majungu, msikiliza majungu na anayeendesha
chama kimajungu.
Sasa kwa ufupi tu ni kwamba mimi bado ni mwana Chadema na kupitia
mahojiano haya, natangaza rasmi ili Watanzania wote wasikie, kwamba
nitagombea Uenyekiti wa BAVICHA mwaka huu. Mimi ni kamanda na kamanda
hakimbii vita hata siku moja.
Mtanzania Jumatano: Unatangaza uamuzi mzito sana huo ukiwa katika
mgogoro na viongozi wako, itakuwaje ukikataliwa kugombea. Utachukua
hatua gani, utahama chama kama ambavyo imetokea kwa wanasiasa wengine
wengi waliokutangulia au utachukua hatua gani?
Shonza: Wakifanya hivyo watakuwa wameamua ‘kubaka’ demokrasia ndani
ya chama na chama kisicho na demokrasia ni hatari kwa mustakabali wa
nchi yetu. Watanzania na wana Chadema wataona na wataamua iwapo itakuwa
hivyo. Lakini hata ikiwa hivyo, sitakaa nikahama chama, nitapambana
nikiwa ndani ya chama, nitapigania demokrasia.
Mimi ninaamini hakuna haja ya kukimbia changamoto na ndiyo maana hata
wenzangu ninaodaiwa kuvuliwa nao uanachama kwa mujibu wa tangazo la
Wegesa (Heche) walipochujwa kutogombea Uenyekiti Bavicha katikati ya
uchaguzi, hawakuondoka Chadema.
Mtanzania Jumatano: Vipi kuhusu tuhuma kwamba unatumiwa na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema, Zitto Kabwe kukihujumu chama?
Shonza: Mimi siyo mtu wa kutumiwa, bali ninajituma mwenyewe kwa
sababu ninajitambua, sishikiwi akili na mtu. Situmiwi na Zitto wala
yeyote ndani ya chama, isipokuwa nimekuwa nikishirikiana naye kwa karibu
katika shughuli za ujenzi wa chama kwa sababu nyingi, kwanza ni
kiongozi kijana ambaye ana uwezo mkubwa wa kiuongozi na amekuwa chimbuko
la vijana wengi kujiunga na upinzani, nikiwemo mimi mwenyewe.
Pili ni kiongozi aliyekaribu sana na viongozi wote wa Baraza la
Vijana bila kubagua kama baadhi ya viongozi wa chama wanavyofanya. Kwa
mfano ni kiongozi pekee aliyetoa gari lake bure litumike kwa shughuli za
ujenzi wa baraza japo Wegesa (Heche) amelifanya gari hilo la kwake,
ufisadi mwingine huu kutumia mali ya baraza kwa matumizi yake binafsi.
Pia, siku zote nimekuwa nikivutiwa na siasa za Zitto zilizojaa weledi
mkubwa katika namna ya kujenga na kusimamia hoja, kuwa na msimamo na
kutoyumbishwa.
Zitto si kiongozi wa hovyo kama ambavyo gazeti la kipropaganda la
Chadema limekuwa likimchafua, kwamba anamiliki mtandao wa vijana
wanaotaka kuharibu chama.
Tatizo ni kwamba ukiwa na uwezo na msimamo wa kusimamia kile
unachokiamini, ‘future’ yako Chadema inakuwa mashakani. Ndicho
kilichomkuta marehemu Chacha Wangwe, Kafulila, Walid Kaborou na wengine
wengi.
Pamoja na haya bado si mwisho, wako wengine watakuja kuyaongea haya
tunayoyaongea sisi sasa, maana hata sisi wanaotuita masalia hatukuwa wa
kwanza kufukuzwa bila kufuata misingi ya kikatiba.
Kwa hiyo mimi ni muumini wa siasa za Zitto, lakini hanitumii na
niweke wazi kabisa kwamba endapo akigombea Urais 2015, kama ilivyo azma
yake, nitamuunga mkono kwa asilimia 100.
Mtanzania Jumatano: Unazionaje siasa za ndani ndani ya Chadema kuelekea uchaguzi mkuu mwaka 2015.
Shonza: Bado kuna kazi kubwa ya kufanya kabla ya 2015 ili tuweze
kuchukua nchi, hasa maeneo ya vijijini, bila kuwasahau na kuwaacha
wanawake nyuma, maana ndiyo wadau wakubwa na ndiyo wapiga kura wakubwa.
Lakini jambo la muhimu ni chama ‘kirecruit’ wanawake wengi na kiwatie
moyo badala ya kuwakatisha tamaa.
Lakini jambo la muhimu zaidi ambalo ni lazima viongozi wakuu wa chama
wakubali kubadilika tunapoelekea mwaka 2015 ni hili linalohusu uadilifu
wao. Tunawatuhumu viongozi wengine kwa ufisadi, tunawatangazia
Watanzania kuwa uadilifu wa viongozi wa vyama vingine ni wa kutiliwa
shaka wakati viongozi ndani ya Chadema uadilifu wao una madoa mengi
meusi. Hili litatugharimu kama chama.
Viongozi wakubali kujisahihisha, Chadema ni chama cha siasa cha
Watanzania wote, huo ndiyo msingi wa kuanzishwa kwake, na siyo chama cha
kuwanufaisha wachache wanaojua kuteka akili za wengine kwa sababu
wamewachoka waliopo madarakani.
Siasa za ndani ya Chadema ni siasa zilizogubikwa na uviziaji wa
demokrasia, ubaguzi wa ukanda na ukabila. Hili ni tatizo ambalo siku
Watanzania na wanachama wa Chadema wakiligundua, chama hiki kitaporomoka
na kuwa kama vingine vilivyopata kuwa maarufu halafu vikaporomoka kwa
kasi ya ajabu.
Mfumo wa sasa wa uendeshwaji wa chama wa mfano wa Saccos haufai. Ni
lazima uachwe. Katibu Mkuu, Dk. Willbrod Slaa, kajikopesha Sh. milioni
140 ambayo ni michango ya wanachama na wakati huo huo analipwa donge
nono la mshahara wa zaidi ya Sh. milioni saba kwa mwezi pamoja na
marupurupu mengine. Hili haliwezekani kunyamaziwa kwa sababu fedha hizi
ni za wanachama.
Ni aibu kwa kiongozi kama Dk. Slaa kuudanganya umma wa Watanzania
kuwa amekopa Sh. milioni 20 wakati nafsi yake anajua kuwa si kweli. Wako
wapi wakaguzi wa hesabu za fedha ndani ya vyama hivi vya siasa!
Inafika mahala tunashindwa kujua kama ni kweli Dk. Slaa wa sasa ndiye
yule aliyesoma orodha ya mafisadi pale Mwembe Yanga au la! Kwa sababu
matendo yake hayaendani na mahubiri yake. Bado tuna kazi kubwa ndani ya
chama, lakini ninaamini tutajisafisha tu. Acha niwajibike bwana, siku
nyingine nihoji.
NA MTANZANIA
Post a Comment