Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

NGASSA ADAI NI FITINA ZA SOKA TU

Uongozi wa Yanga umesema utapinga uamuzi wa Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi ya Wachezaji ya TFF ya kumfungia Ngassa.
Dar. Mshambuliaji mpya wa Yanga, Mrisho Ngassa ameishangaa Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi ya Wachezaji kwa kushindwa kumtendea haki ya kumruhusu kuichezea Yanga moja kwa moja badala yake wamemfungia mechi sita na kumtaka kuilipa Simba Sh 45 milioni.
Ngassa alisema jana kuwa uamuzi wa kamati hiyo ya TFF umetokana na ‘fitina’ za soka, lakini yeye anaamini ni mchezaji halali wa Yanga.
Alisema kuwa hakusaini mkataba na Simba kutokana na ukweli kuwa alikuwa na timu hiyo kwa mkopo na kama angekuwa amesaini, kamati hiyo ingemwidhinisha kuchezea Simba ambayo aliitumikia katika mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara msimu uliopita.
“Wameniidhinisha kuichezea Yanga, eti mpaka nikae nje mechi sita na kulipa fidia, hii siyo haki na kwa nini wanipe adhabu wakati wao walitakiwa kunitetea mimi kwa mujibu wa kazi zao,” alisema Ngassa.
Alisema kuwa, “Tofauti na majukumu yao, wameniangamiza kwa staili ya ‘kuuma na kupulizia’ kwa kuogopa kufuata sheria ambayo wameitumia kuniidhinisha kuichezea Yanga.”
“Mimi napingana nao, si uamuzi wa kunitetea, ‘nitakomaa’ nao na ninaamini viongozi wangu wa Yanga nao watakuwa na msimamo huohuo,” alisema Ngassa.
Nao uongozi wa Yanga umesema kuwa utapinga uamuzi wa Kamati hiyo ya TFF wa kumfungia Ngassa kuichezea timu yao kwa mechi sita sambamba na kuilipa fidia Simba ya Sh45 milioni.
Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Yanga, Abdallah Bin Kleb alisema kuwa uamuzi wa Kamati hiyo haukulenga hali halisi ya sakata zima la usajili wa mchezaji huyo na kuhoji kwa nini amelipishwa faini huku akiidhinishwa kuichezea Yanga?
Bin Kleb alisema kuwa kama kamati imeridhika kuwa Yanga imefuata taratibu zote za usajili wa mchezaji huyo, haikupaswa kumchukulia hatua zote hizo.
Alisema kuwa cha ajabu ni kitendo cha kamati hiyo kushindwa kuiadhibu Simba ambayo inadaiwa ilimsainisha mkataba mwingine Ngassa huku wakijua kuwa anaitumikia klabu hiyo kwa mkopo na ni kinyume na utaratibu, siyo hapa Tanzania tu, bali dunia nzima.
“Kingine kamati haikuzingatia mambo aliyofanya Ngassa akiwa Simba, ameifungia mabao timu hiyo na kuiwezesha kushika nafasi ya tatu, hii leo unaamuru arejeshe fedha zote zinazodaiwa kulipwa kwa mchezaji huyo bila kujali ameifanyia nini timu hiyo,” alisema Bin Kleb.

CHANZO:Mwananchi.

author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top