Rais wa Rwanda Paul Kagame
ameshutumu vikali viongozi wa Burundi kutokana na mauaji yanayoendelea
nchini humo nakuonya kuwa huenda kukatokea mauaji ya halaiki
Bw Kagame ameshangaa ni vipi viongozi wa taifa hilo jirani "wanaweza kuruhusu wananchi wao kuuwawa kiholela".
Rais
Kagame alisema hayo Ijumaa, lakini matamshi yake hayakutangazwa hadi
mwishoni mwa wiki, akionekana sana kumlenga Rais wa Burundi Pierre
Nkurunziza.
Akizungumza kwa Kinyarwanda Rais Kagame alisema:
''Tazama nchi jirani kama Burundi, maisha yao yamesimama kabisa. Lakini
sababu ni ipi? Wana historia inayofanana na yetu.
Ila viongozi wao wapo kwa ajili ya kuua wananchi kuanzia asubuhi hadi jioni."
''Rais akajifungia sehemu isiyojulikana, hakuna
anayejua sehemu alikojificha, hakuna anayezungumza naye, huyo anaongoza
watu vipi?" alisema Bw Kagame, akihutubu katika hafla ya kuwatunuku
Wanyarwanda waliosaidia kuwaficha na kuwaokoa Watutsi wakati wa mauaji
ya kimbari 1994 pamoja na wanaharakati wanaotetea umoja na maridhiano
miongoni mwa Wanyarwanda.
''Watu wanakufa kila siku, maiti
zinabururwa barabarani. La kusikitisha ni kuwa bara la Afrika lina
ugonjwa wake lenyewe kiasi kwamba hata nitalaumiwa eti nimekosea kuitaja
nchi nyingine, eti ningecheza diplomasia au siasa. Siyo haki mimi
nitasema wazi. Viongozi wanashinda wakiua watu, maiti zinatapakaa sehemu
zote; wakimbizi wanarandaranda sehemu zote watoto, wanawake ....kisha
unasema ni siasa. Hiyo ni siasa gani?"
Uhusiano kati ya Rwanda na
Burundi umedorora sana tangu Bw Nkurunziza atangaze kuwa atawania urais
kwa muhula wa tatu, hatua iliyopingwa na wapinzani.
Mwezi uliopita,
Burundi ilimfurusha mwanabalozi mmoja kutoka Rwanda ikimtuhumu kwa kuhujumu usalama wa nchi hiyo.
"Utasema
kuwa ni nani aliyesababisha matatizo ya Burundi? hata kukiwa na mtu
anayekutakia mabaya atavutiwa na ubaya wako unaotenda...Hata kama ni mtu
kutoka Rwanda anayesababisha machafuko nchini Burundi, bila shaka
atavutiwa na maovu ya viongozi wa Burundi wanayotendea wananchi wao.
Shida ni ya Warundi wenyewe," alisema Bw Kagame.
"Tatizo ni kwamba hawakupata somo kutoka kwetu
(Rwanda), kutokana na yaliyosibu taifa letu wangepata somo hasa kutokana
na baadhi ya Warundi wenyewe kuhusika katika yale yaliyolisibu taifa
letu.
Afrika sijui tunaugua ugonjwa upi?"
Hayo yamejiri siku moja baaya watu 9 kuawa usiku na watu wenye silaha, ndani ya baa moja katika mji mkuu wa Bujumbura.
Askari
wa usalama wanafanya msako katika kila nyumba, kwenye mitaa
inayoonekana kuwa ni ngome za upinzani, baada ya muda uliowekwa na
serikali kwa watu kusalimisha silaha zao kumalizika.
Watu takriban 20 wameuwawa nchini Burundi katika juma lilopita, huku maelfu ya watu wakitoroka makwao.
SOURCE:BBC SWAHILI
Post a Comment