Dar es Salaam.Baada ya kuapishwa kushika
madaraka ya Rais, kibarua kizito cha Dk John Magufuli ni kuunda Baraza
la Mawaziri litakaloendana na kasi ya kaulimbiu yake ya ‘Hapa kazi tu’,
ambalo ni wazi litajaa sura nyingi mpya.
Kujaa kwa sura
mpya katika baraza hilo kutokana idadi ya wabunge waliokuwa mawaziri na
naibu mawaziri katika Serikali iliyomaliza muda wake kupungua kutoka 55
walioanza na Rais Jakaya Kikwete katika awamu yake ya pili hadi 23,
kati yao 20 wa majimbo na watatu wa viti maalumu waliofanikiwa kurudi
katika Bunge la 11.
Uchambuzi uliofanywa na Mwananchi
umebaini kuwa wengi wa mawaziri hao ama waliangushwa wenye majimbo yao
ya uchaguzi, hawakupitishwa na CCM kuwania tena ubunge, hawakugombea
tena ubunge au walifariki dunia.
Baadhi ya wabunge
wateule waliokuwa mawaziri katika Serikali iliyopita huenda wakawa na
nafasi ya kuteuliwa tena katika baraza jipya la mawaziri la Rais
Magufuli, huku wale walioanguka wakisubiri huruma ya rais huyo kwa
nafasi mbalimbali za uteuzi, zikiwamo 10 za wabunge wa kuteuliwa
Maoni ya wachambuzi
Akizungumzia
Baraza la Mawaziri linalotarajiwa, mchambuzi wa masuala ya kisiasa na
Mhadhiri wa Chuo Kikuu Dar es Salaam, Dk Benson Bana alisema Rais
Magufuli amekuwa waziri kwa miaka takribani 20, hivyo anajua kati ya
mawaziri waliopita nani mzembe na nani mchapakazi, jambo ambalo
litamfanya ateue watu sahihi.
“Tatizo la nchi yetu ni
mawaziri wanaoteuliwa, wengi wanajilimbikizia mali na kuwa karibu na
wafanyabiashara. Wapo wabunge walikuwa mawaziri wanaoweza kwenda na kasi
yake (Dk Magufuli).
“Kwanza amejipa muda wa kutosha,
hakutaka kuwahi kuteua, nadhani anajipanga ili kupata watu sahihi.
Watanzania watarajie mshangao katika uteuzi wake, usisahau kuwa ana
nafasi 10 za kuteua wabunge ambao anaweza kuwapa uwaziri,” alisema.
Dk
Bana alifafanua kwamba rais huyo ni lazima awe na mawaziri makini kwa
sababu Bunge la kumi na moja litakaloanza vikao vyake Novemba 17
litakuwa na mvutano mkali, hasa kutoka wa wabunge wa vyama vya upinzani
ambavyo vimetoka kujeruhiwa katika Uchaguzi Mkuu.
Hata
hivyo, Dk Bana alisema Dk Magufuli kama akishindwa kujipanga kwa awamu
yake ya kwanza ya miaka mitano atapata aibu kubwa, jambo alilodai kuwa
ni vigumu kutokea.
“Anatakiwa kujitahidi kuwa na Baraza la Mawaziri ambalo halitakumbwa na kashfa kama ile ya Escrow au Dowans,” alisisitiza.
Kwa
upande wake Profesa wa Uchumi katika Kilimo wa Chuo Kikuu cha Sokoine
(SUA), Damian Gabagambi alisema tatizo la Tanzania si sera wala sheria
mbovu, akifafanua kuwa hata Dk Magufuli alipokuwa Waziri wa Ujenzi
aliweza kufanya mambo mazuri.
“Naona tatizo ni uzembe
tu na umakini. Dk Magufuli aliwahi kusema kuwa ataingia mikataba na
mawaziri wake ili kama wakishindwa kutekeleza jambo awawajibishe.
Nadhani hili ni wazo zuri.
“Yule atakayeshindwa akae
pembeni. Pia anatakiwa kuteua watu wasio na kashfa, nadhani uzoefu wake
serikalini umempa mwanga na sasa atakuwa anawajua mawaziri wazembe na
wachapakazi,” alisema.
Alifafanua kuwa baraza hilo linapaswa kuchanganywa mawaziri wapya na wa zamani wachache, ili kuondoa “kufanya kazi kwa mazoea”.
Mawaziri wa zamani
Hadi
anaondoka madarakani, Rais Jakaya Kikwete katika baraza lake alikuwa na
mawaziri na naibu mawaziri 55, wakiwamo 16 ambao alianza nao tangu
2005.
Kati yao, mawaziri 12 walishindwa kura ya maoni
ndani ya CCM, sita waliangushwa katika Uchaguzi Mkuu, watatu walikuwa
wabunge wa kuteuliwa na rais na hawakugombea, wawili walifariki dunia na
sita hawakugombea ubunge.
Katika orodha hiyo,
aliyekuwa Waziri wa Fedha, Saada Mkuya baada ya kuteuliwa na Rais
Kikwete kuwa mbunge, amegombea ubunge katika Jimbo la Kijitoupele,
Zanzibar ambalo bado halijafanya uchaguzi.
Pia mawaziri
waliobahatika kurudi bungeni ni Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na
Watoto, Sofia Simba, Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya
Makazi, Angela Kairuki na Naibu waziri wa Katiba na sheria, Ummy
Mwalimu.
Katika orodha ya mawaziri 55 yupo Dk Magufuli na Samia Suluhu Hassan waliochaguliwa kuwa Rais na Makamu wa Rais.
Katika
uteuzi wake, Rais Magufuli anaweza kurejesha baadhi ya wabunge
waliokuwa mawaziri, pia kuchagua wabunge nje ya hao au kuteua ambao sasa
siyo wabunge, lakini vyovyoite hawatarajiwi kuwa wengi.
Pia,
Dk Magufuli anaweza kutumia utaratibu uliomwibua yeye, wakati wa Rais
mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa alipoteua sura nyingi mpya za
wabunge na kuwapa uwaziri.
Pia upo uwezekano wa kuteua
wabunge wapya kimikoa au kikanda uliokuwa unatumiwa na mtangulizi wake
ambao utakumbwa na changamoto kutokana na baadhi ya mikoa kuwa upungufu
wa wabunge wa chama chake.
Mkoa wa Kilimanjaro
mathalan, waliokuwa mawaziri watatu wameshindwa ubunge, akiwamo Anne
Kilango (Naibu-Elimu), Aggrey Mwanri (Naibu-Tamisemi) na aliyewahi kuwa
Waziri wa Viwanda, Dk Cyril Chami, huku wakibaki mawaziri wa zamani
mawili.
Endapo Dk Magufuli atafuata utaratibu wa
kimikoa, nyota inaweza kuwawakia tena Profesa Jumanne Maghembe (Mwanga)
na aliyekuwa waziri wa Uvuvi na Mifugo, Dk David Mathayo David
aliyevuliwa uwaziri katika sakata la Operesheni Tokomeza.
Wadadisi
wa masuala ya kisiasa wanajiuliza endapo pia, Rais Magufuli anaweza
kuwakumbuka mawaziri waliotoswa kutokana na kashfa ya Akaunti ya Tegeta
Escrow, Profesa Anna Tibaijuka (Ardhi) na Profesa Sospeter Muhongo
(Nishati na Madini).
Mawaziri walioshinda ubunge
Waliokuwa
mawaziri ambao kwa sasa ni wabunge wateule ni; George Simbachawene
(Nishati na Madini), Juma Nkamia ( Naibu-Habari), Lazaro Nyarandu
(Maliasili na Utalii), Mahmoud Mgimwa (Naibu-Maliasili na Utalii),
Charles Kitwanga (Naibu-Nishati na Madini).
Charles
Mwijage (Naibu-Nishati na Madini), Stephen Masele (Naibu-Muungano),
William Lukuvi (Ardhi), Mwigulu Nchemba (Naibu-Fedha), Jenista Mhagama
(Sera, Uratibu Bunge), Gerson Lwenge (Naibu-Maji).
Wengine
ni Dk Harrison Mwakyembe (Afrika Mashariki), January Makamba
(Naibu-Mawasiliano), George Mkuchika (Utawala Bora), Profesa Jumanne
Maghembe (Maji), Dk Shukuru Kawamba (Elimu), Hawa Ghasia (Tamisemi), Dk
Mary Nagu (Mahusiano na Uratibu), Dk Charles Tizeba (Naibu-Uchukuzi) na
Dk Hussein Mwinyi (Ulinzi)na Janet Mbene (Naibu-Viwanda na Biashara).
Walioanguka kura ya maoni
Waliokuwa
mawaziri ambao waliangushwa kura ya maoni Dk Binilith Mahenge
(Mazingira), Adam Malima (Naibu-Fedha), Dk Seif Rashid (Afya), Dk Pindi
Chana (Naibu-Wanawake, Jinsia na Watoto), Dk Titus Kamani (Uvuvi), Kaika
Telele Naibu-Uvuvi) na Amos Makala (Naibu-Maji).
Dk
Abdulla Juma Abdulla (Naibu-Afrika Mashariki), Mathias Chikawe (Mambo ya
Ndani), Mahadhi Juma Maalim (Naibu-Mambo ya Nje), Pereira Ame Silima
(Naibu-Mambo ya Ndani), Christopher Chiza (Uwekezaji na Uwezeshaji) na
Gaudencia Kabaka (Kazi na Ajira).
Viti maalumu
Mawaziri
waliokuwa wabunge wa viti maalumu ambao wamerudi mjengoni, Sofia Simba
(Wanawake, Jinsia na watoto), Angela Kairuki (Naibu-Ardhi) na Ummy
Mwalimu (Naibu-Katiba na Sheria).
Waliangushwa katika uchaguzi
Mawaziri
walioangushwa katika uchaguzi ni Dk Stephen Kebwe (Naibu-Afya), Anne
Kilango- Malecela (Naibu-Elimu), Dk Fenella Mukangara (Habari), Aggrey
Mwanry (Naibu-Tamisemi), Stephen Wasira (Kilimo), Godfrey Zambi
(Naibu-Kilimo).
Hawakugombea tena
Mawaziri
ambao hawakugombea kabisa ubunge ni Samuel Sitta (Uchukuzi), Profesa
Mark Mwandosya (Ofisi ya Rais-Kazi Maalumu) Bernard Membe (Mambo ya
Nje), aliyekuwa Waziri Mkuu, Mizengo Pinda na Dk Makongoro Mahanga
aliyehama CCM na kujiunga na Chadema.
Pia wapo
waliokuwa mawaziri baada ya kuteuliwa na Rais Kikwete kuwa wabunge
lakini hawakujitosa kuwania ubunge majimboni ambao ni, Dk Asha-Rose
Migiro (Katiba na Sheria), Profesa Makame Mbarawa (Mawasiliano).
Waliofariki dunia
Mawaziri
wa Serikali iliyomaliza muda waliofariki dunia ni aliyekuwa Waziri wa
Viwanda na Biashara, Dk Abdallah Kigoda na aliyekuwa Waziri wa Nchi,
Ofisi ya Rais (Utumishi), Celina Kombani.
Post a Comment