NA BASHIR YAKUB .
BIASHARA
hufanywa kwa mitindo ya aina nyingi kutegemea na mahitaji ya wahusika.
Unaweza kufanya biashara kwa mtindo wa kampuni, unaweza kufanya
biashara kwa mtindo wa mtu binafsi, lakini pia unaweza kufanya biashara
kwa mtindo wa shirika ( firm)/ubia. Mitindo hii yote inatofautiana
kiutendaji, kifaida na kiuwajibikaji (liability).
Kuhusu
kampuni tumeeleza mara nyingi faida zake, aina zake, masuala ya hisa,
mpaka namna ya kuunda kampuni, ada zinazostahili na kila kitu. Pia yapo
makala yaliyoeleza biashara binafsi hasara na faida zake. Leo katika
makala haya tutapata kuona biashara ya shirika (firm)/ubia . Tukumbuke
kuwa haya yote ni mazao ya sheria na hivyo huwa tunayatizama kwa mtazamo
wa sheria.
Sheria
imeeleza kwa mapana kabisa aina zote hizi za biashara ili kuepusha
migongano baina ya wahusika. Sura ya 345 ya sheria ya mikataba
iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002 ndiyo inayozungumzia shirika/ubia
kama tutakavyoona.
1.SHIRIKA/UBIA NI NINI.
Shirika/Ubia
ni uhusiano uliopo baina ya watu wanaofanya biashara ya faida kwa
pamoja . Kwa hiyo ili ubia uwepo ni lazima watu wawili au zaidi waungane
na waamue kufanya biashara kwa pamoja. Hii ni kwa mujibu kifungu cha
190 cha sheria ya mikataba. Kuungana huku ili kufanya biashara sio
kuunda kampuni.
Ni kuungana ambako hakuhusishi kampuni lakini kunakotambulika kisheria. Muungano wa kufanya biashara kwa pamoja ndio ubia.
Watu
walioingia ubia kwa umoja wao wanaitwa shirika ( firm). Kwa hiyo shirika
na ubia humaanisha kitu kimoja na ndio maana katika makala maneno haya
yanatumika pamoja. Na jina wanalotumia wabia linaitwa jina la shirika (
firm name).
Mifano
ni mingi ila mojawapo ni yale mashirika ya wanasheria yaitwayo law
firm, au ya wahasibu yaitwayo accountant firm na mengine mengi. Lakini
hata katika biashara za kawaida za uuzaji wa bidhaa na mengineyo nako
ubia hufanyika.
2. TOFAUTI YA SHIRIKA UBIA (PARTNERSHIP FIRM ) NA KAMPUNI (COMPANY).
Tofauti ni nyingi ila hizi ni baadhi :
( a )
Katika shirika (firm) ikiwa kuna mkopo umekopwa na shirika kwa ajili ya
biashara fulani basi wanashirika wote wanawajibika kwa deni hilo kila
mtu mmoja mmoja kwa nafasi yake. Na ikiwa shirika litashindwa kulipa
basi mali binafsi za kila mmoja ya washirika zinaweza kukamatwa kulipia
deni hilo. Hii haipo kwenye kampuni. KatIka kampuni haiwezi kutumika
mali ya mtu binafsi mwanahisa kufidia deni ambalo kampuni imeshindwa
kulipa hasa kama mali hiyo haikutumika kama rehani. Ni mali ya kampuni
tu itakayotumika.
( b )
Shirika linaposababisha hasara kwa mtu mwingine ambaye sio mwanashirika
kwa maana ya mtu wa tatu basi wanashirika(partners) wanawajibika kufidia
hasara hiyo kwa michango yao. Hii ni tofauti na kwenye kampuni ambapo
wenye kampuni hawawajibiki kufidia hasara iliyosababishwa na kampuni kwa
mtu ambaye si mhusika katika kampuni hiyo. Kampuni kama kampuni ndiyo
inayowajibika kufidia hasara hiyo na si wenye kampuni. Mali za kampuni
ndizo zitakazotumika na kama hazipo hilo ni jambo jingine. Muhimu ni
kuwa mali za wenye kampuni hazitaguswa.
( c )
Katika ubia hakuna mtu anaweza kualikwa kuwa mbia katika shirika bila
ridhaa ya wabia wote. Kila mbia ni lazima aridhie ujio wa mbia mpya.
Katika kampuni hasa makampuni ya umma (public company) haihitajiki
ridhaa ya wana hisa wote ili mtu mpya akubaliwe kuwa mwanahisa.
3. KANUNI KUU ZINAZOONGOZA SHIRIKA (FIRM).
Kanuni
kuu inayoongoza shirika ni makubaliano ya kimkataba. Kile
mnachokubaliana kimkataba ndicho kinachotakiwa kutekelezwa. Kama hakuna
makubaliano yoyote basi masharti yaliyo katika kifungu cha 194 cha
sheria ya mikataba ndiyo yatakayotumika kama makubaliano yenu. Masharti
hayo ni pamoja na kila mbia kuwa sehemu ya uongozi wa shirika, maamuzi
kufanywa kwa kura za walio wengi, haki ya kukagua vitabu vya shughuli za
shirika, kugawana faida kwa usawa, n.k.
4. SHIRIKA (FIRM) HUSAJILIWA WAPI.
Mashirika
(firm) husajiliwa kwa msajili wa makampuni na biashara BRELA. Vipo
vyeti maalum ambavyo hutolewa kwa ajili ya usajili baada ya ada ya
usajili hulipwa. Katika makala nyingine tutaona kipi bora kibiashara
kati ya shirika (firm) na kampuni ( company).
MWANDISHI
WA MAKALA HAYA NI MWANASHERIA NA MSHAURI WA SHERIA KUPITIA GAZETI LA
SERIKALI LA HABARI LEO KILA JUMANNE, GAZETI JAMHURI KILA JUMANNE NA
GAZETI NIPASHE KILA JUMATANO. 0784482959, 0714047241 bashiryakub@ymail.com
Post a Comment