Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

Aibu ni chaguzi za Zanzibar, sio wapinzani kususa Bunge

BAADA ya yaliyotokea wiki iliyopita katika shughuli ya uzinduzi wa Bunge, watu wengi, hususan wanasiasa walio upande wa chama tawala, Chama Cha Mapinduzi (CCM0, wameita kitendo cha wabunge wa vyama vya upinzani kususia kusikiliza hotuba ya Rais Dk. John Magufuli ya uzinduzi wa Bunge kuwa ni kitendo aibu.

Wabunge-wa-UKAWA-wakitoka-bungeni-
Wabunge-wa-UKAWA-wakitoka-bungeni-Njonjo Mfaume

Uamuzi wa kugomea shughuli hiyo ulitokana na uwepo wa Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein ambaye wapinzani wanadai hastahili kuendelea kuongoza Zanzibar. Wapinzani walitaka rais wao halali, Seif Sharrif Hamad, ndiye awepo.

Mmoja wa walioelezea fujo iliyotokea na kitendo cha mgomo wa wapinzani kuwa ni cha aibu ni Spika wa Bunge hilo, Job Ndugai, huku Rais Magufuli mwenyewe akiita kitendo hicho kuwa ni cha kitoto.

Mimi nakataa. Sioni kuwa kitendo kile cha wapinzani ni cha aibu wala cha kitoto. Kuna vitendo vya aibu vimefanyika nchi hii ambavyo ndio hasa vimetufedhehesha mbele ya wageni.

Kwa mfano, nchi imeingia katika aibu kwa vitendo vya hujuma dhidi ya demokrasia ambavyo vimekuwa vikitokea kila mwaka wa uchaguzi kule Zanzibar na kuingiza nchi katika migogoro ya kisiasa.

Kutokana na migogoro hii ya kisiasa ya Zanzibar watu wamekufa na wengine kupata ulemavu katika 20 iliyoita. Tanzania imetoa wakimbizi wa kisiasa kwenda Kenya na sehemu nyingine duniani. Jumuiya ya Kimataifa, hususan Commonwealth imekuja kujaribu kutupatanisha wakati sisi ndio tegemeo la majirani zetu la kupatanisha wanapogombana. Na haya ndio mambo ya aibu.

Kuanzia uchaguzi wa 1995 ambao ni wa kwanza kufanyika baada ya kurudishwa kwa mfumo wa vyama vingi mwaka 1992 hadi huu wa mwaka 2015 hakujawahi kuwa na uchaguzi uliopita bila kuzalisha migogoro mikubwa Zanzibar.

Uchaguzi wa mwaka 1995 ambao CCM ilitangazwa kuwa mshindi ulizaa mgogoro baada ya Chama cha Wananchi (CUF) kudai kuwa imeporwa ushindi na kugoma kumtambua rais aliyetangazwa. Taarifa za waangalizi wengi wa kimataifa zilieleza masikitiko yao kutokana na vitisho dhidi ya raia na udanganyifu katika kuhesabu kura, jambo ambalo waliamini huenda lilipelekea matokeo yaliyotangazwa kuwa sio sahihi. Baadhi ya nchi wafadhili kama Norway na Sweden zilisimamisha misaada kwa Zanzibar kutokana na kadhia ile na hii kwa mtazamo wangu ndio aibu.

Kutokana na mgogoro huo, Jumuiya ya Madola ilisimamia mazungumzo ya upatanishi na hatimaye kufikiwa makubaliano yaliyosainiwa Aprili 29, 1999. Yalikuwa ni makubaliano mazuri ambayo yangetekelezwa huenda migogoro isingejirudia tena. Moja kati ya vipengele vya makubalino kuwa zichukuliwe hatua za kuhakikisha kuwa chaguzi za miaka ijayo ziwe wazi, huru, za kuaminika na zisiwe na mizengwe.

Hata hivyo, uzuri wa makubaliano ni kitu kingine, na dhamira ya kisiasa ya kutekeleza makubaliano hayo, hususan kwa upande wa watawala, ni jambo jingine.

Ni wazi kuwa makubaliano yale ambayo yalilenga katika kujenga misingi ya kuimarisha demokrasia, utawala bora na utengamano hayakutekelezwa kwani mwaka 2000 kulitokea mgogoro mwingine ambao ulizalisha wakimbizi waliokimbilia Shimoni, Mombasa huko Kenya. Na hii nayo ni aibu nyingine.

Pia, kufuatia uchaguzi wa mwaka 2000, mnamo Januari 27, 2001, watu 31 waliuwawa, 48, walipata vilema vya maisha na 243 walijeruhiwa, baada ya polisi kutumia nguvu kuzuia maandamano ya kupinga matokeo ya au uchaguzi Unguja na Pemba. Hii pia ni aibu iliyotufedhehesha kama taifa. Wengi wa wahanga hao walitoka kisiwani Pemba.

Chanzo cha mgogoro wa uchaguzi wa mwaka 2000 ilikuwa ni kufutwa kwa matokeo ya uchaguzi na kuamuliwa kurudiwa katika majimbo kadhaa ambapo CUF haikukubaliana na uamuzi huo na kuamua kususia uchaguzi wa marudio. Katika uchaguzi huo wa marudio, CCM walijishindia kirahisi.

Mgogoro ukaendelea tena hata katika uchaguzi wa 2005, ambapo kwa mara nyingine tena, CUF waligoma kuitambua serikali ya Rais Amani Abeid Karume. Kutokana na kutoridhika kwa uwepo wa hali hiyo ya migogoro iliyogawanya jamii ya Wazanzibar, baadhi ya wanasiasa kutoka CUF na CCM walifanya jitihada ya kuanzisha mazungumzo ya kutafuta muafaka ambayo ndio yaliyozaa mpango wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa mwaka 2010 ambayo ilikubaliwa na Wazanzibar wengi.

Mazungumzo yaliyozaa muafaka na ambayo yalifanywa na Wazanzibar wenyewe yalianza Machi 2009 na kufikia tamati Novemba 2009 kwa mkutano wa Rais Karume na Maalim Seif Sharif Hamad na kukubaliana kufuta tofauti za kisiasa zilizoigawa jamii ya Wazanzibari kwa zaidi ya miaka 15. Labda ni kutokana na muafaka wa kisiasa uliofikiwa uchaguzi wa mwaka 2010 haukuhijiwa sana, ingawa bado kulikuwa na figisu figisu nyingi.

Hata hivyo, mwaka 2015 umekuwa ndio kilele cha migogoro yote baada ya Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC), Jecha Salim Jecha, kuamua peke yake kufuta matokeo ya uchaguzi wote, ingawa Tume ya Uchaguzi ya Tanzania, (NEC) haikufanya hivyo kwa matokeo ya Zanzibar. Inasemekana Jecha alitangaza uamuzi ule wa kufuta matokeo kwa kushinikizwa.

Jambo la kuzingatia ni kuwa kwa mara ya kwanza katika uchaguzi wa Zanzibar mwaka huu waangalizi wote wameuita huru na wa haki, huku CCM wakilalamika kuibiwa. Kitendo cha CCM kimetajwa kuwa ni sawa kutia mpira kwapani katika mechi ya soka, baada ya kuona unaelekea kushindwa! Nikimjibu Magufuli, walichofanya CCM Zanzibar si sahihi.

Kuna hoja nyingi za kitaalamu zinazotolewa kuhalalisha yaliyofanyika Zanzibar, lakini yote hayo ni katika jitihada za kuficha aibu kubwa kabisa kuliko zote. Aibu kubwa kuliko zote ni kuwa kuna maana mpya ya demokrasia imetoholewa kule Zanzibar. Demokrasia Zanzibar maana yake ni ushindi kwa CCM, na si vinginevyo.

Najua kuna sababu za baadhi ya Wazanzibar na hata wanasiasa wa Tanzania Bara kuamua kutumia maana hii mpya ya demokrasia iliyotoholewa. Kule Zanzibar, CCM wanasema walipindua na hivyo basi hawako tayari kutoa serikali kwa vipande vya karatasi. Pia wanasema wana wasiwasi CUF watarudisha Waarabu. Huku Bara tunaogopa Uislamu wa siasa kali, kama ambavyo video maarufu ya William Lukuvi akizungumza kanisani ilivyotudhihirishia.

Mimi sio mtaalamu wa yote mawili. Sijui undani wa siasa za kimatabaka za Uarabu dhidi ya Weusi, Zanzibar. Kadhalika pia sijui ajenda halisi za CUF na uhusiano wake na siasa kali za Kiislamu, ingawa nimewahi kusoma makala ya Abdulrahman Kinana katika jarida moja huko nje akigusa suala la ugaidi.

Hata hivyo, kwamba hatusemi yaliyo vifuani mwetu kwa uwazi na badala yake tunatekeleza demokrasia ya hila na ghilba ni aibu kubwa. Tunamhofia nani kusema na kutenda kile tunachoamini? Nashauri CCM waifute CUF Zanzibar ili watawale peke yao badala ya kuendelea kuulea uhizbu na siasa kali za CUF kisa wanataka kuonekana na wao ni waumini wa demokrasia. Mimi sielewi kwa nini tunashindana katika uchaguzi kama kushindwa si matokeo ambayo tutakubali hata siku moja?

Baada ya hayo niseme kuwa kitendo cha wapinzani kususia bunge sio cha aibu. Ni kitendo kizuri cha kishujaa kuiambia dunia kuwa mambo si shwari Zanzibar. Nitamshangaa balozi wa nchi ya kigeni ambaye atashangaa kitendo kile kwa kiasi cha mshangao chini ya alioupata kwa yaliyotokea Zanzibar. Sana sana wengi watatupa uzoefu wa vituko vikubwa zaidi vilivyowahi kutokea katika mabunge ya nchi zao.

CHANZO: RAIA MWEMA
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top