Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

CHADEMA YAJA KIVINGINE


  • YAELEZA mikakati ya kuzaliwa upya, Katibu Mkuu asema Watanzania wataamua kama viatu vya Dkt. Slaa vimempwaya, anahitaji vipya au vimemtosha, adai Magufuli ana mtihani....
BAADA ya kumalizika kwa Uchaguzi Mkuu Oktoba 25, mwaka jana, na Chadema kuibuka na wabunge 72 wa majimbo na viti maalumu, chama hicho ksasa imeeleza mikakati ambayo kimesema itashangaza wengi muda mfupi ujao.
Katibu Mkuu wa chadema, Dk. Vincent Mashinji.
Mikakati hiyo saba mikubwa, iliwekwa wazi na Katibu Mkuu wa chama hicho, Dk. Vincent Mashinji, alipokuwa akizungumza na gazeti hili. Alisema baada ya muda mfupi Watanzania wataamua kama viatu vya mtangulizi wake, Dk. Willibrod Slaa, vinamtosha, vinampwaya au anahitaji vipya.


Dk. Mashinji ambaye aliteuliwa kushika wadhifa huo takribani mwezi mmoja uliopita, akieleza mikakati ya kukisuka chama hicho, alisema kwa kuanza watapunguza uanaharakati na kuhakikisha halmashauri zote zilizo chini yao zinakuwa za mfano wa kuigwa.


Alisema utendaji kazi wa halmashauri hizo, baada ya muda zitakuwa ushawishi kwa wananchi kujua kwamba wanaweza kuongoza serikali kwa viwango vya hali ya juu.


Pia alisema kwa sasa wameunda timu ambayo imejichimbia kuandaa njia bora ya kupata wagombea wa ngazi mbalimbali, badala ya mfumo wa kura za maoni unaotumika sasa. Mkakati mwingine alioulize ni kuhakikisha, uongozi wa chama unarudi kwa wananchi kwenye ngazi za vijiji na mitaa na kwamba makao makuu watabaki na sera pekee.


Mbali na kujenga chama kitu ambacho ni jukumu lake kubwa, ajenda ya ufisadi alisema kamwe haiwezi kuachwa na chama hicho.


Akifafanua hoja Akieleza mikakati ya ya kujenga chama, Dk. Mashinji alisema: “Mikakati ni kupeleka chama kwa wanachama. Chama kilishashuka.


Kwa mfano, uamuzi wote wa kiutendaji unafanywa na ofisi za kanda, kwa hiyo chama kiko karibu na wanachama. Lakini M4C is for life (ni ya maisha).


Bado ipo sana mpaka tutakapohakikisha tunaleta mabadiliko. Inaweza ikawa inabadilisha tu ‘brand’ kulingana na matukio, lakini ‘our movement is still there’. 

Swali:
Kuhusu Wenyeviti na Mameya wanaotokana na Ukawa kwamba wahakikishe hawategemei ruzuku ya serikali kuu, hili linatekelezeka vipi hasa ukizingatia kuwa kuna tatizo la madawati, zahanati na huduma nyingine za kijamii?

 Jibu:
Nadhani ukiisoma sheria ya serikali za mitaa inapeleka haya majukumu kwa halmashauri husika. Na jukumu la serikali kuu ni kuingilia pale tu inapotokea kuna mkwamo, lakini kama unavyoona asiyekubali kushindwa si mshindani.


Hawa mabwana (CCM), hawajakubali kushindwa kwa hiyo wanahakikisha wanafanya figisufigisu ilimradi tu kuhakikisha ile hali ya utengamano inaondoka. Na kwa sababu wao akili yao hawashindwi.


Sasa huwezi kuendesha nchi kwa kuviziana. Tumekuwa tukitoa mawazo kueleza tatizo liko wapi, lakini ukiangalia ni kama hawa mabwana (CCM), wanatu-block kila unachotaka kufanya wanazuia.


Kwa mfano, sasa hivi wanafanya kitu cha ajabu kabisa kuhakikisha kwamba property tax (kodi za majengo) zote zinahamia serikali kuu.


Hiki kitu kilishawahi kufanyika na ukusanyaji haukufanikiwa kwa sababu serikali kuu haiko kwa watu. Wao wanachofikiria kwenye akili zao ni kuzipunguzia Halmashauri mapato kwa sababu miji mikubwa yote ukianzia Dar es Salaam, Arusha, Babati, Moshi, Mbeya, Iringa, Bukoba, Mtwara yaani karibia miji yote inaongozwa na Ukawa na hakuna Halmashauri nyingine yenye mapato makubwa.


Ukibana ukusanyaji wa mapato, hawa wanaoongoza hizi halmashauri wawe wanasubiri ruzuku. Kwa hiyo unapoona mikakati kama hii unagundua kabisa kwenye hii nchi kuna watu wanataka kujenga nchi, lakini kuna kundi lingine malengo yao siyo kujenga nchi. Malengo yao ni kulinda nafasi zao na kubomoa.


Sasa sisi tutaenda kupambana nao ndiyo maana ukiangalia sasa hivi Mkuu wa Mkoa au Mkuu wa Wilaya anatangazwa kama ndiye Mwenyekiti wa Halmashauri.


Anayefanya hivi ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), George Simbachawe, ambaye ni mwanasheria na alikuwa akizunguzma si kwa bahati mbaya.


Anawaelezea wakuu wa mikoa kwamba wanapolisi na magereza, lakini anasahau kuwa nchi inaendeshwa na wananchi siyo mapolisi na magereza.


Wananchi wanaongozwa na Halmashauri zao na wenye mamlaka ya kuamua matumizi ya rasilimali kwenye maeneo yao ni Baraza la Madiwani ambalo Mkuu wa Mkoa au Wilaya si wajumbe, kwa mujibu wa sheria.


Kuhusu majukumu ya mameya na suala la utekelezaji wa Ilani ya CCM, wao wanasema wanafanya siasa za Ujamaa na Kujitegemea, sisi tunasema tutafanya siasa za mrengo wa kati; sasa jiulize ni falsafa yao…zidumu fikra sahihi za Mwenyekiti wa chama wakati falsafa yetu ni nguvu ya umma, kwamba watu wataamua mambo yao hapa ndipo kwenye tofauti yetu.


Tutakachokifanya ni kuita watu na kujadili mambo yao na kuamua. Nikupe mfano, kuna kodi za majengo na kodi ya huduma, ambazo asilimia 0.3 zinatakiwa kurudi kwenye mtaa. Sasa muulize mtendaji wako, alishawahi kurudishiwa hizi hela? Kwa hiyo kama kwenye mtaa wako kuna kiwanda au majengo yakitozwa kodi lazima asilimia 0.3 inatakiwa irudi kwa wananchi.


Hii tutaisimamia na tutawaambia wananchi haki zao na watatakiwa kuzidai. Fedha hizi zikipatikana, unaweza kukuta tatizo la madawati likaisha.


Wao waendelee kufanyakazi kwenye vyombo vya habari, sisi tutawaeleza wananchi na tutawaita watendaji wawe wa CCM au Ukawa, kuwaeleza hili.


Swali: Umepokea chama kikiwa kinaandamwa na tuhuma za rushwa na hasa baada ya kuwakaribisha baadhi ya waliokuwa makada wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), hili likoje?

 Jibu:
Unajua chama hivi sasa kimekua sana. Unapozungumzia Chadema siyo tena kile chama tulikuwa nacho miaka 10, 15 iliyopita. Sasa hivi tunazungumzia chama chenye wabunge 72, Halmashauri 24 kwenye nchi.


Chama ambacho sasa hivi kimefanya ‘decentralization by devolution’ (ugatuaji wa madaraka), kinaongozwa katika ngazi ya kanda badala ya taifa na huku taifa imebakia kutoa miongozo ya kisera.


Kwa hiyo chama kinavyokua kinakuwa na wanachama wa aina mbalimbali. Ni kweli kumekuwa na sauti za kusema sasa hivi kuna watu wanakula rushwa kwenye chama, lakini kuna mfumo ambao uko makini, hauruhusu rushwa ndiyo maana hata waliojaribu waligundulika mapema.


Ukiangalia vizuri utaona hata viongozi waliojihusisha na rushwa kwa njia njia yoyote ile, wengi wao walisimamishwa. Ukiangalia kuna sehemu nyingi kuna nafasi ziko wazi, inawezekana ni kwa tuhuma za rushwa au nyingine, lakini inaonyesha kabisa kuwa hii (Chadema), ni taasisi inayofanyakazi kwa mfumo wa kitaasisi na siyo mfumo wa mtu. Suala la rushwa si kubwa kama watu wanavyojaribu kulipaka rangi (kulikuza).


Unajua chama kinavyokuwa kikubwa mtu anajua kabisa nikishapitishwa na Chadema kugombea nakuwa mbunge, anaanza kutumia njia mbalimbali.


Lakini tuna mfumo madhubiti sana wa kiusalama kuchagua wagombea. Kwa hiyo suala la rushwa kwenye jamii yoyote ambayo inaendelea, huwezi kusema kwamba halitakuwapo; hapa ni namna unavyojipanga kukabiliana nalo.


Chama kina mfumo wake wa kufuatilia wanachama. Swali: Vipi kuhusu tuhuma za upendeleo wa mgawanyo wa viti maalum? Jibu: Hii ni tafsiri tu ya mtu, wala haupo na imeshaelezwa kwenye Baraza Kuu na wote waliokuwa wanalalamika walikuwa wanajua, japokuwa kuwa kuna external force (shinikizo la nje ya chama), zinazoingia ndani kuja kutuvuruga.


Viti Maalum tulivyonavyo ni vichache, unatakiwa upeleke kwenye Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), majina ya watu 105. Kilichofanyika ni kwamba tuna-allocate kwa nia ya kujenga chama kwa sababu kupanga majina tu bila vigezo vingine unaweza kukuta unapeleka majina ya watu wanaotoka sehemu moja.


Tuli-allocate kiti kwa kila mkoa na sasa kila mtu alikuwa ana matarajio yake. Tulifanya hivyo kwa sababu kazi mojawapo ya hawa wabunge (Viti Maalum), ni kwenda kujenga chama.

 Swali:
Inaonekana mfumo wa kura za maoni umechangia kusababisha rushwa, huu mfumo ninyi mnauonaje? 

Jibu:
Tumefikiria kwenye Baraza Kuu na sasa hivi timu yetu ya mkakati imepewa kazi ya kufikiria njia mbadala na muafaka ya ambayo itasaidia kupata wagombea mbalimbali, kwa sababu unapokuwa na ile hali ya kushindanisha watu wapo watakaokwenda na mbinu halali na wapo watakaocheza rafu.


Katika kuchezeana rafu saa zingine unakuta mtu kacheza rafu nyie kama viongozi hamjaiona, lakini yule aliyechezewa rafu kaiona kwa hiyo unaweza kukuta saa nyingine inasababisha mipasuko ya chama. Kwa hiyo tunajaribu kutafuta njia ambayo nadhani hivi karibuni…kabla ya mwezi huu wa sita itakuwa imepatikana ambayo itakuwa ni shirikishi.


Swali: Upo tayari kuhimili matusi ya wapinzani wenu? Jibu: Wanafalsafa wanasema ukiona watu wanatukana ujue wameshindwa na wanaamua kufanya uhalifu.


Sisi chama chetu hatufanyi vurugu. Tunajua haki ya mtu huwa haipotei, bali inachelewa na tutaipata karibuni. Swali: Katiba mpya, hii ajenda imefikia wapi? 

Jibu:
Hii ndiyo ajenda yetu kuu. Maelekezo ambayo tumeyatoa kwa wabunge wetu ni kwamba popote watakapokuwa, chochote watakachofanya lazima kila kitu wanachofanya wahusishe na Katiba mpya.


Tutapiga kelele hata kama ulikuwa umelala utaamka tu maana itakukera. Magufuli alikuwa na mitihani miwili tu, Zanzibar na Katiba mpya. Zanzibar amefeli sasa amebakisha Katiba ili ama afaulu kiasi au afeli kabisa. Katiba ambayo wananchi wanaitaka ni ile rasimu ya pili iliyoandikwa na Jaji Joseph Warioba kwa sababu ni shirikishi na imebeba maoni ya wananchi. Sasa hivi Magufuli anazungumza maadili na hakuna mtu asiyetaka maadili;
yapo kwenye rasimu ya Warioba.


 Anayofanya sasa hivi yote atashindwa kwa sababu sheria nyingi hazimruhusu. Mwaka 1983, Sokoine alifanya hichi hichi anachofanya Magufuli leo, yaani ni kama unaangalia video.


Alikamata watu wengi kama wahujumu uchumi akawaweka ndani, baadaye kuna mtu mmoja Arusha alikamatwa kama mhujumu uchumi, ndugu zake wakaenda kuomba kumwekea dhamana ili atolewe kizuizi.


Aliyekuwa amemweka ni Mkuu wa Mkoa, mbele ya Jaji wakasema sheria inataka anayemweka kizuizini ni rais, na hata kama anakasimisha madaraka kwa Mkuu wa Mkoa anatakiwa amwachie kwa maandishi yake mwenyewe yakiwa na seal ya taifa na kwa mtu mahsusi si kwa kundi.


Na Mkuu wa Mkoa anatakiwa ndani ya saa 48, amwandikie jaji kwa mkono wake, ampelekee na ale kiapo; lakini hakuna anayefanya hivi.


Hawa watu wanaokamatwa na kuachiwa, wakiamua kuishtaki serikali kwa udhalilishaji, tutaingia kwenye matatizo. Kwa hiyo mwaka 1983, wanasheria walihoji na wakati huo, baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, alikuwa nje ya nchi, kaimu wake alikuwa Jumbe.


Wanasheria wakaeleza kuwa kama Jumbe ndiye anakaimu, Rais alitakiwa amwandikie kwa mkono wake na aweke muhuri. Watu wakasema alete hiyo barua, haikuwapo kwa hiyo wakamwachia.


Nyerere alivyorudi, akaandika barua ya kumkaimisha Jumbe, yule mfanyabaishara akakamatwa tena. Baada ya kumkamata wakahoji tena wanashtakiwa kwa sheria gani, hakukuwa na sheria.


Mwaka 1984 ikatungwa sheria ya uhujumu uchumi na wakasema ianze kufanyakazi mwaka 1983. Waliona kina Dk. Slaa wanapiga kelele ufisadi, wao wanao ni mtaji…wakadandia treni kwa mbele, lakini hawajui kwamba mtu anapokaa anapanga kitu chake ana namna yake ya jinsi ya kutekeleza.
Sasa hivi anakamata watu.


Nchi ina mechanism mbalimbali, mojawapo ni usalama wa taifa, polisi, jeshi na nyingine ni raia. Usalama wa Taifa inatakiwa kukusanya taarifa zote ambazo zinahatarisha usalama na ustawi wan chi na kuishauri serikali.


Unataka kuniambia kwamba makontena 300 yanapotea bandarini halafu uniambie Ikulu haikujua. Watu wamechukua hela Stanbic, siamini kwamba Ikulu haikujua. Hili ni genge la watu ambao wanatangulizana tu kwamba wewe fanya hivi, mimi nikija nitafanya hivi, lakini kuna mahali watakutana.

CHANZO IPP MEDIA
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top