Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

KUTOKA ACT-WAZALENDO:SASA NAWASHAURI WABUNGE MPUMZISHENI MAGUFULI



Nimetumia muda wa kutosha kumpa Ushauri wa Bure Ndugu John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania (JMT) juu ya Kudumisha Utawala wa Sheria na Kulinda Demokrasia iliyopelekea yeye kuwa Kiongozi wa nchi hii. Nakumbuka Msajili wa Vyama vya Siasa alijaribu kutoa Tafsiri ya Kauli ya Rais ya Kupiga Marufuku Mikutano ya Kisiasa mpaka 2020, siku moja baada ya mimi kuandika kwenye Ukurasa huu Kushangazwa kwangu na Ukimya wa Msajili wa Vyama juu ya Kauli hiyo ya Mwenyekiti Mtarajiwa wa CCM inayopingana na Kanuni za Vyama vya Siasa za Mwaka 2007 zilizotungwa chini ya Sheria ya Vyama vya Siasa. 


Hata hivyo, Kauli zilizotolewa hivi karibuni na baadhi ya Wakuu wa Mikoa juu ya Kupiga Marufuku Mikutano ya Kisiasa katika Mikoa yao zinadhihirisha wazi kwamba Msajili wa Vyama vya Siasa ndiye aliyeshindwa kumuelewa Rais Magufuli.


Ingawa Katiba ya Jamhuri ya Muungano inampa Kinga Rais kushitakiwa Mahakamani (Ibara ya 46), lakini Katiba inalipa Bunge la Jamhuri ya Muungano Mamlaka ya “Kumng’oa” Rais kwenye Kiti Chake. Kwa mujibu wa Ibara ya 46A (2), Bunge linaweza kumlazimisha Rais kuachia ngazi, naye kulazimika kufanya hivyo Kupitia Azimio la Bunge, endapo atathibitika kufanya makosa yafuatayo:

(a) Ikiwa ametenda vitendo ambavyo kwa Ujumla vinaivunja Katiba au Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma;


(b) Ikiwa ametenda vitendo ambavyo vinakiuka Maadili yanayohusu Uandikishwaji wa Vyama vya Siasa yaliyotajwa katika Ibara ya 20(2) ya Katiba; au


(c) Ikiwa amekuwa na mwenendo unaodhalilisha kiti cha Rais wa Jamhuri ya Muungano…


Ukifuatilia Mwenendo tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie Madarakani, Rais amekuwa akilalamikiwa kwa Kukandamiza Demokrasia, kutumia Lugha za kudhalilisha kwa Vijana waliotimuliwa Chuo Kikuu cha Dodoma (kwa kuwaita VILAZA) na mambo mengine yanayokwenda Kinyume na Katiba ya JMT na Lengo la Kuwepo kwa Katiba hiyo kama linavyobainishwa na Ibara ya 9 ya Katiba. Tazama 9(a), 9(f) na 9(h) kwa mfano, pia rejea Hotuba ya Ndugu Zitto Kabwe, Mbunge wa Kigoma Mjini na Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo aliyoitoa mbele ya Maelfu ya Wakaazi wa Dar es Salaam, kwenye Viwanja vya Zakhiem Mbagala 05/06/2016.


Katiba ya JMT imeeleza hatua ambazo katika Mazingira kama haya, Bunge linaweza kumfikisha Rais kwenye Kujiuzulu. Ibara ya 46A(3)(a) inaeleza kwamba Mchakato wa Kumng’oa John Pombe Magufuli (JPM) Ikulu unaweza kuanza kwa Taarifa ya Maandishi inayoungwa mkono na asilimia ishirini ya Wabunge wote Kuwasilishwa, ikieleza makosa yake. Naamini kupata asilimia ishirini ya wabunge kuanzisha huu Mchakato si suala zito, linawezekana ( Kumbuka Idadi ya Wabunge wa Upinzani).

Ingawa Mchakato huu unaweza ukapata ugumu kupitia Kamati Maalum ya Uchunguzi itakayoundwa katika mazingira haya ya Demokrasia finyu, naamini Kitendo cha Rais kulazimika kujieleza/kujitetea ni hatua muhimu sana katika Kurekebisha Nidhamu na kuwakumbusha Viongozi wa Umma kwamba HAKUNA ALIYE JUU YA SHERIA.

Kwa mujibu wa Ibara ya 46A (9):
“ Baada ya Taarifa ya Kamati Maalum ya Uchunguzi kuwasilishwa kwa mujibu wa Ibara ndogo ya 8 ( yaani 46A (8)), Bunge litaijadili taarifa hiyo na litampa fursa ya kujieleza, na kisha, kwa kura za Wabunge wasiopungua theluthi mbili za Wabunge wote, Bunge litapitisha azimio ama kuwa mashitaka dhidi ya Rais yamethibitika, na kwamba hastahili kuendelea kushika Kiti cha Rais, au kuwa mashitaka hayo hayakuthibitika”.


Nitumie fursa hii kuwaondoa hofu wabunge wa Upinzani, wasihofie idadi kubwa ya wabunge wa CCM.

Wapo wabunge wanaochukizwa na baadhi ya makosa haya kwani Ubabe huu ukiachiwa hata atakapokuwa Mwenyekiti wa Chama chao, atakandamiza Demokrasia ndani ya CCM.

Kusambaratika kwa Ukomunist zama za Vita Baridi kuliwakutanisha Mahasimu Marekani na Osama Bin Laden katika dhamira moja, japo kwa Sababu na Malengo tofauti. 

Si ajabu theluthi mbili ya Kura ikapatikana ili kulinda Maslahi mapana ya Taifa hili. 

Hivyo naamini JPM atalazimika kujiuzulu ndani ya Siku 3 tangu kupitisha Azimio (Ibara 46A(10)) na kuweka Rekodi ya kuwa Rais wa Kwanza kuondolewa na Bunge kwa kujaribu kuichezea Demokrasia tunayoijenga kwa taabu na hatimaye apoteze Malipo yoyote ya Pensheni na Haki zingine (Ibara 46A(11)).

Kwa kuwa haki hii wamepewa Wabunge wa JMT na mimi si Mbunge, natumia fursa hii kwa mujibu wa Ibara ya 18(a) ya Katiba ya JMT kuwashauri wabunge wakaweke Historia hii mpya kwenye Kikao kijacho cha Bunge.

Eng. Mohamed M. Ngulangwa
Katibu wa Uadilifu Taifa
ACT-Wazalendo(0713417707)
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top