MAHAKAMA ya
Rufani nchini, kesho inatarajia kutoa hukumu ya rufaa iliyokatwa na
aliyekuwa Mbunge wa Arusha Mjini kwa tiketi ya CHADEMA, Godbles Lema,
kupinga hukumu ya Mahakama Kuu Kanda ya Arusha iliyotengua ubunge wake.
Hukumu hiyo
inayovuta hisia za wengi nchini, inatarajiwa kuhudhuriwa na wafuasi
wengi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo
(CHADEMA).
Mamia ya
wafuasi wa Lema kutoka mjini Arusha, wakiongozwa na Katibu Mkuu wa mkoa
huo, Aman Gulugwa, wanatarajia kuongoza msafara wa magari kwenda jijini
Dar es Salaam kwa ajili ya kusikiliza rufaa hiyo ya kihistoria.
Habari za
kuaminika toka ndani ya Mahakama ya Rufani jijini Dar es Salaam,
zilisema kuwa tayari jopo la majaji watatu; Nataria Kimaro, Salum
Massati na Bernad Ruhanda, limeshamaliza kazi na kwamba uongozi wa
mahakama umepanga hukumu hiyo isomwe kesho.
“Tarehe ya hukumu ya rufaa iliyofunguliwa na Lema ni kesho, hivyo mfike bila kukosa,” kilisema chanzo chetu cha habari.
Desemba 4
mwaka huu, Mahakama ya Rufaa ilisikiliza sababu 18 zilizowasilishwa na
mawakili wa Lema, Method Kimomogoro na Tundu Lissu kupinga hukumu
iliyomvua ubunge mteja wao.
Baadhi ya
hoja za mawakili wa Lema ni pamoja na madai kwamba Jaji Gabriel
Rwakibalila wa Mahakama Kuu Kanda ya Arusha, alijielekeza vibaya katika
hukumu yake alivyosema kesi za uchaguzi hazitawaliwi na kanuni za sheria
za Uingereza wakati kuna maamuzi ya kesi mbalimbali zilizokwishatolewa
hukumu na Mahakama ya Rufaa na Mahakama Kuu nchini na kuruhusu kesi za
uchaguzi ziamuliwe kwa kanuni za sheria za Uingereza.
Mawakili wa
Lema pia walidai hakuna ushahidi unaoonesha wajibu rufaa kweli ni
walioandikishwa kupiga kura katika Jimbo la Arusha Mjini.
Mawakili hao
pia wanadai jaji alikosea kisheria kusema kuwa mtu yeyote akiwemo mpiga
kura ana haki ya kufungua kesi ya kupinga matokeo ya uchaguzi wa jimbo
ambalo yeye ni mpiga kura.
Kutokana na
hali hiyo, wanaiomba Mahakama ya Rufaa itamke kuwa wajibu rufaa (wapiga
kura wa Arusha waliofungua kesi ile), hawana haki kisheria kufungua kesi
ya kupinga ubunge wa Lema kwani mwenye haki ni Dk. Batrida Buriani
aliyekashifiwa.
Pia walidai
hukumu ile haina hadhi ya kuitwa hukumu kwani Jaji Rwakibalila alikosea
na kujielekeza vibaya kisheria katika kutoa hukumu.
Kwa upande
wa mawakili wa wajibu rufaa, Aluthe Mugwai na Modest Akida na wakili wa
Msimamizi wa Uchaguzi na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Timon Vitalis
walijibu sababu zote 18 na kusisitiza kuwa hukumu iliyovua ubunge wa
Lema, ilikuwa sahihi na ilikidhi matakwa ya sheria.
Aprili 15
mwaka huu, Mahakama Kuu Kanda ya Arusha ilitoa hukumu katika kesi ya
kupinga ubunge wa Lema iliyofunguliwa na wapiga kura watano wa Jimbo la
Arusha Mjini.
Katika
hukumu hiyo, mahakama ilimtia hatiani Lema kwa makosa ya kutoa lugha za
matusi na udhalilishaji dhidi ya mgombea wa CCM, Dk. Burian katika
kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka 2010.
Chanzo:CHADEMA BLOG
Post a Comment