Kesi ya mauaji ya kutokukusudia inayomkabili msanii wa filamu nchini,
Elizabeth Michael `Lulu’, imepokelewa katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar
es Salaam na kusajiliwa kwa namba 125 ya mwaka 2012.
Elizabeth Michael `Lulu’
Kwa mujibu wa habari zilizopatikana mahakamani hapo, kesi hiyo
imepokelewa kutoka Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na inasubiri
kupangiwa Jaji na tarehe ya kuanza kusikilizwa.
Awali Lulu alikuwa akikabiliwa na mashitaka ya kumuua msanii mwenzake,
Steven Kanumba, kwa kukusudia lakini baada ya upande wa mashitaka
kukamilisha upelelezi alibadilishiwa mashitaka na kuwa kuua bila
kukusudia.
Kesi hiyo ilifunguliwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mbele ya
Hakimu Augustina Mmbando, katika hatua za awali na Lulu hakuruhusiwa
kujibu mashitaka yanayomkabili kwa kuwa Mahakama hiyo haina mamlaka ya
kusikiliza kesi hiyo.
Kwa mujibu wa sheria, kutokana na Lulu kushitakiwa kwa kosa la kuua bila kukusudia, anaweza kupata dhamana.
Desemba 21 mwaka huu, Lulu alisomewa maelezo ya kesi na ushahidi
utakaotumika na upande wa mashitaka katika kesi hiyo, ambapo Wakili wa
Serikali Shedrack Kimaro alidai kuwa watakuwa na mashahidi tisa,
ushahidi wa nyaraka, ripoti ya uchunguzi wa hospitali na ramani ya eneo
la tukio.
Baadhi ya mashahidi watakaotoa ushahidi ni pamoja na mdogo wa marehemu,
Seth Bosco, Sofia Kassim, Daktari wa marehemu aitwaye Pancras Kageigwa,
Morris Semkwao na Esther Zephania ambaye ni askari Polisi wa kituo cha
Oysterbay, Kinondoni.
Katika kesi hiyo, inadaiwa kuwa Aprili 7, mwaka huu nyumbani kwa
Kanumba, Sinza Vatican, jijini Dar es Salaam, Lulu alimuua bila
kukusudia msanii huyo nyota wa filamu nchini.
Chanzo - HabariLeo
Post a Comment