NAIBU Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo
(CHADEMA), Zitto Kabwe, amekishutumu Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwamba
kinachonganisha viongozi wa chama chake kwa lengo la kukidhoofisha
wakati huu kinapoelekea kushika dola mwaka 2015.
Zitto alisema hayo jana alipokuwa anazungumza na viongozi wa CHADEMA
wa matawi na kata zote kutoka Jimbo la Kigoma Kaskazini ukiwa ni mkakati
wake wa kuendelea kukijenga chama na kujua matatizo ya kisiasa na
kijamii yanayowakabili wananchi wake.
Mbunge huyo ambaye ameamua kupiga kambi jimboni humo kwa lengo la
kuwazuia CCM wasipotoshe wananchi wake wakati huu wanapoadhimisha miaka
36 ya kuzaliwa chama chao, alisema kuwa licha ya maneno na uvumi kuzagaa
kwamba CHADEMA Taifa inakabiliwa na mgogoro baina ya viongozi, jambo
hilo si kweli.
Zitto alibainisha kuwa hali hiyo inakuzwa na watu waliopandikizwa na
kutumiwa na CCM kwa ajili ya kuleta mpasuko na kukigawa chama ili
kupunguza kasi yake ya kuelekea uchaguzi mkuu wa mwaka 2015.
“CHADEMA hakuna mpasuko wala migogoro kama inavyotafsiriwa na wengi,
badala yake kuna kakundi kanataka kutuhujumu kwa kutugawa kwa kutumia
itikadi za kidini, kimaeneo, kimitazamo na hata kiitikadi kama
walivyotumwa na hicho chama chao.
“Ninachoweza kusema ni kwamba ndani ya chama chetu kuna majungu,
fitina, kuoneana wivu, usaliti na hata kumalizana kisiasa, haya
tutahakikisha tunayamaliza kikatiba kwa sababu hiyo ndiyo sheria mama
inayotuongoza ili tufikie malengo tuliyojiwekea,” aliongeza Zitto.
Alidai kuwa wajibu wake ni kupigania misingi ya uwajibikaji na
demokrasia ndani ya CHADEMA ili kuondokana na vitendo vya uongozi wa
kutumia mabavu kama ilivyo kwa CCM, ambayo imekuwa ikitumia nguvu katika
kuendesha mambo yake, sambamba na serikali iliyopo madarakani.
Hata hivyo, aliwashutumu viongozi wa jimbo lake kwa kushindwa
kuwajibika ipasavyo katika kujenga chama na badala yake kila kitu
kumtegemea yeye kama mbunge ikiwa ni pamoja na vikao na mikutano ya
hadhara.
“Ili tujenge chama chenye nguvu na heshima, ni lazima viongozi wote
tushirikiane kuanzia ngazi ya matawi, kata na jimbo badala ya kila kitu
kunitegemea mimi mbunge, lazima tuweke misingi imara ya chama ili
mgombea ajaye wa CHADEMA asipate wakati mgumu wa kufanya kampeni,”
alisisitiza.
Zitto aliongeza kuwa, wakazi wa Kigoma kwa miaka mingi wamekuwa hawana
mtetezi katika ngazi za kitaifa, kiasi kwamba hoja za kuendeleza mkoa
kwa kupatiwa miradi ya maendeleo zinapata upinzani mkubwa kwenye vikao
vya uamuzi kama vile Baraza la Mawaziri na Bunge.
“Lazima sisi watu wa Kigoma tuwe na umoja kwa sababu tumekuwa wanyonge
kwa miaka mingi, na daima nguvu ya wanyonge ni umoja baina yaoNa sisi
tunapaswa kuwa na umoja kwa ajili ya maendeleo ya mkoa wetu na hata hii
miradi inayoletwa Kigoma sasa ni kutokana na kelele tunazopiga,”
alisema.
Aliongeza kuwa hata kama hatagombea nafasi yoyote ndani ya chama, bado
ataendelea kuwa mwanachama mwaminifu na ataitumikia CHADEMA kwa vile
misingi aliyoshiriki kuitengeneza kwa ajili ya ustawi wa chama hicho
bado haijakamilika na hawezi kuiacha ikiwa hivyo.
TANZANIA DAIMA
Post a Comment