Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

TUKICHOKA KUHUBIRI AMANI, TUJIANDAE NA KAZI YA KUCHIMBIANA MAKABURI (Mawazo yangu katika kutafakari neno la Maggid Mjengwa)


Kaka zangu Maggid Mjengwa na Ansbert Ngurumo, mimi pia huandika mara chache tu, nyinyi ni kati ya waandishi ambao mimi huwasoma sana.

Binafsi nakubaliana na Maggid na sitatofautiana sana na Ansbert. Kuwa, wanasiasa tusiwatumie vijana vibaya, wengi hawana elimu, hawajui lolote na wanaburuzika kirahisi.

Tufungue njia za “dialogue” zaidi kuliko mapambano ambayo hayana mwisho mwema.
Pamoja na CCM kuishika pabaya nchi hii, pana haja tunaopambana CCM iondoke tuwe “very tactical". Mara nyingi tuwekeze nguvu kubwa katika kutafuta masuluhisho ya kudumu.

Hivi karibuni nilikuwa LIWALE na Ruangwa, sikuona aibu, niliwaeleza wananchi kuwa kudai haki zao ni muhimu, lakini isifikie kuanza kuchoma majumba na magari ya walioshikilia haki zao.Tukianza hiyo michezo ya kuchomeana itapasa visasi vianze, visasi havina macho, vitatupeleka pabaya. Pamoja na mapambano ya kudai haki,amani haikwepeki kwa sababu ikikosekana ina maana hata harakati za kudai haki hazina pa kufanyikia.

Leo Tanzania ikigeuzwa kuwa uwanja wa vita na mapambano kila kona ya nchi, hatutakuwa na vyama vya siasa tena, tutakuwa na vikundi vya kupigana kwa kutumia silaha kila kona. Hatutapeperusha bendera za vyama.

Na jambo tunalosahau ni kuwa,hivi sasa tukiwafanya vijana wetu wawe "rude", "bully" and "cruel" kwa kisingizio cha kudai haki, Siku CCM itakapoondoka na ikaingia CUF, CHADEMA au mwingine, vyama hivi vipya vitarithi madaraka ya nchi na vijana hao hao RUDE,BULLY and CRUEL. Hivi sasa ndo tukijifanya machampioni wa kuwaeleza vijana kuwa ajira zinapatikana “after 3 days”. NCHI HII TUTAIPIGA KIBERITI WENYEWE....

Sera za vyama vitakavyoongoza dola zijikite katika kuwaelimisha wananchi, wajue kuwa nchi imefikishwa pabaya sana na CCM. Vijana wajipange wapambane kupiga kura na kulinda kura nchi nzima hadi CCM iondoke. Vijana wasishauriwe eti wakapambane na bunduki za CCM na kwamba liwalo na liwe! Pasiwe na liwalo kwenye maisha ya vijana wetu.

WIKI tatu zilizopita nilifika Nanyumbu kufanya mkutano wa hadhara, polisi waliuzuia kupitia zuio la waziri wa mambo ya ndani na jeshi la polisi makao makuu kuwa mikutano ya vyama isifanywe mkoa wa Mtwara isipokuwa na wabunge na madiwani tu.
Kufika Nanyumbu nikakuta vijana wapatao 1000 wakanipokea, wao na kina mama wakasema mkutano lazima ufanyike. Polisi nao walikuwa ‘Standby’ na mabomu yao na bunduki zao na vitambaa vyekundu na kabla ya hapo walishatangaza kwa vipaza sauti kuwa nisifanye mkutano.

Pamoja na presha kubwa ya umma uliokusanyika MJINI na ile presha ya viongozi wangu wa wilaya kuwa nisipolazimisha kufanya mkutano ATI tutaua chama Nanyumbu niliweka msimamo. Ukweli ni mchungu, sikuwa hata na mshauri, ilinipasa kutangaza kuwa hakuna mkutano. Niliwakumbusha wananchi kuwa pale hapatakuwa na mkutano bali mapambano ya polisi na wananchi.
Nilipowauliza wangapi wako tayari kwa mapambano wote wakanyoosha mikono hadi watoto, tena wakiwa na hasira KUU. Niliwaeleza kuwa nilikuja kwa ajili ya mkutano tu na siyo mapambano.

Nikawataka watawanyike kimyakimya kurudi majumbani. Nilizomewa sana lakini nilikubali gharama hizo, sikuwa tayari kuacha vilema na majeruhi na hata maiti za watu “just because” ntalaumiwa na viongozi na wananchi na wanachama. Nilitambua kuwa mara kadhaa nimewahi kuhutubia mahali pale na nikajua kuwa nitakuwa na fursa nyingine siku za usoni. Hasira zote zilikuwa juu yangu...kelele za msaliti nikapigiwa, nikakubali. Kazi ya kiongozi ni kuongoza na si kufuata.

Nakubaliana na Maggid Mjengwa, kuwa viongozi wa vyama vyote tujipange. CCM haitaondolewa madarakani kwa mapambano ya vijana wetu na polisi na mabomu na risasi. Tuwaandae vijana nchi nzima, tuwaandae bodaboda na wamachinga wasimamie mabadiliko makubwa ya elimu ya fikra na demokrasia pana. Tuwaeleze vijana ukweli, kwamba nchi imeharibiwa sana, kwamba tunahitaji CCM iondoke ili kiingie chama imara, kipewe muda wa kutosha wa kusimamia mabadiliko na kupanua wigo wa ajira n.k.

Kamwe wanasiasa tusizunguke nchi kuwadanganya vijana ATI wakituchagua tu, wote watakuwa na ajira. Tusiwadanganye wamachinga ATI wakituchagua tu tutawapa mikopo ya mamilioni, tusiwadanganye vijana ATI watuchague ili keshoye tuwajengee majumba ya biashara. Tuwaeleze vijana ukweli, tuwaeleze kuwa tukishaiondoa CCM tutaweka msingi mkubwa wa kuibadili nchi na kwamba mabadiliko yatakuja hatua kwa hatua yakiwa na tija. Tuwajulishe kuwa tunahitaji muda. Nchi iliyoharibiwa kwa miaka hamsini hatutaijenga kwa siku 3 au mwaka mmoja, inahitaji muda uliopimwa na ukapimika na lazima tuwaandae vijana wafahamu jambo hilo, wasije kudhani kuwa patakuwa na “miracles”!.

Tusiwadanganye ATI tuna uwezo wa kubadili nchi KUFUMBA na KUFUMBUA. Tukishashindwa kutekeleza, lazima APPROACH yetu itakuwa ni kuwafanyisha vurugu, ili waone kuwa tunawatetea na kwamba VURUGU HIZO ndiyo zitaleta SULUHU ya matatizo yao. Hakuna mahali ambapo vurugu zimewahi kuwa suluhu ya matatizo ya wananchi.
Kuibadili nchi iliyoharibiwa na CCM kwa nusu karne inahitaji utulivu mkubwa na kuwaelimisha sana vijana, vinginevyo ni kweli tutaanza kuchimbiana makaburi.

Julius Mtatiro,
+255717536759, +255787536759,
juliusmtatiro@yahoo.com.
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top