Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

KUTOKA KWA MWANAKIJIJI:MDOGO WANGU SITTI,U-MISS BANGULILE USIKUFANYE UABIKE !


Mdogo Wangu Sitti; U-Miss Bangulile Usikupotezee Utu na Heshima Yako Zaidi...
Mdogo Wangu Sitti; U-Miss Bangulile Usikufanye Uabike!

Na. M. M. Mwanakijiji

Sitti mdogo wangu umeishi Marekani kwa muda mrefu; unajua mambo ya kuwajibika yanavyofanya kazi hasa pale ambapo mtu anajikuta amebanwa na ukweli. Madai ya kwamba kuna mahali umeongopea ili upate unachotaka ni madai mazito na hamna namna ya kukwepa kuwajibika kwake. Ukweli kwa asili yake unaweza kupuuzwa kwa muda au hata kukataliwa lakini hauwezi kugeuzwa uongo halafu ukakubaliwa. Ukweli unasimama wenyewe kama shahidi wake mwenyewe; mtu yeyote mwenye kuutafuta na akaupata anapaswa kuutii na wakati mwingine kuutii hadi mwisho.

Madai dhidi yako kimsingi kabisa ni madogo – kwa maana ya uzito wake – ila ni muhimu sana kwa sababu yanahusu taasisi ambayo mabinti na wazazi kadha wa kadha Tanzania wamekuwa wakiuangalia. Haya Mashindano ya Ulimbwende au “Umiss Bangulile” kama Sheikh wangu Kipozeo amewahi kuyaita ni mashindano siyo tu ya uzuri na maumbo (beauty and figure); ni mashindano juu ya mtu; tabia (character) na mitazamo. Yule anayevishwa taji la Umiss Bangulile (Miss Tanzania) anatakiwa kuwa ni mdada mwenye kuwakilisha mabinti wa rika yake na kuwa mfano kwa wale wa chini ya umri huo kwa mitazamo, tabia n.k Siyo mashindano ya sura tu au maumbo!

Lini umewaliza; siyo swali gumu hivyo. Wewe mwenyewe unaweza kuwa huna uhakika kwani kila mmoja anajua siku yake ya kuzaliw kwa kuambiwa; hakuna anayejua amezaliwa lini. Tunaambiwa na wazazi wetu au walezi wetu na wakati mwingine kuambiwa huku kuna kuja na ushahidi wa vyeti vya kuzaliwa. Kinachonisikitisha kwa kweli kwenye sakata lako ni jinsi gani Wazazi wako wamekuacha mpweke ujibu swali ambalo huna uwezo wa kulijibu. Baba na Mama yako wanapaswa kuwa watu wa kwanza na pekee ambao wana uwezo wa kutuambia kuwa umezaliwa lini. Tatizo ni ukimya wao na hilo wengine linatusumbua sana.

Kwamba umezaliwa mwaka 1989 au 1991 siyo hoja sana; tatizo ni kuwa lazima iwe ni kweli ili kuonesha kuwa unastahili kushiriki na kushinda mashindano haya ya Ulimbwende a.k.a UMiss Bangulile. Vielelezo mbalimbali vya huku kwa Mjomba Obama vinaonesha ulizaliwa mwaka 1989 wakati kielelezo kimoja cha hati ya kuzaliwa ambayo ni nakala (siyo halisi) inaonesha umezaliwa 1991. Wewe mwenyewe umesema umezaliwa 1991.

Sasa, kuna mahali hukusema kweli. Ama uliwadanganya kina Uncle hapa Marekani au uliwadaganya huko nyumbani. Taarifa zote mbili haziwezi kuwa kweli kwa wakati mmoja hasa kwa vile zinapingana. Ni kwa sababu hiyo naamini milango yako yote ya kutokea imefungwa isipokuwa mmoja. Kurudisha taji la Umiss Bangulile na kuomba radhi mashabiki na wapenzi wako na wale wote ambao wamekwazika.

Hautakuwa wa kwanza kati ya ma Miss duniani kurudisha taji la Umiss. Wengi tunakumbuka yaliyomkuta Vanessa Williams Mmarekani Mweusi wa kwanza kushinda taji la Miss America baada ya picha za utupu alizopiga miaka michache nyuma kuibuliwa. Alijiuzulu na kuvuliwa taji japo alifanikiwa baadaye kujijenga katika fani ya uigizaji. Kashfa siyo mwisho wa maisha. Na wapo wengine ambao nao wamewahi kuachilia mataji yao kwa sababu ya kashfa mbalimbali na hivyo isikuwie vigumu kuliachilia taji hilo kwani madhara yameshafanyika. Siamini kama utaweza kusimama kuwakilisha Tanzania katika mashindano mengine bila ya maswali haya haya kuibuliwa na labda yakaibuliwa mazito zaidi.
Naamini hata hivyo hupaswi kujiuzulu peke yako; naamini naye Mkurugenzi wa Mashindano hayo Hashim Lundenga ambaye amesababisha ama kwa uzembe, kushiriki au kwa tamaa nyingine tu kufanya suala hili liibuliwe anapaswa kujiuzulu. Tayari kumeshawahi kuwa na kashfa nyingine zilizomezwa chini kwa chini lakini hii inapaswa kuondoka nay eye ili hatimaye mashindano hayo yapate mtu anayepeswa kuyasimamia kwa uhakika na kwa weledi usio mfano.

Rudisha taji lao jijengee heshima yako tena. Usije ukajikuta katika kuutetea uongo unapoteza na utu wako.
MMM
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top