*watembelea Makao makuu ya PSPF
*wafanya mazungumzo na Mkurugenzi mkuu Bw Adam Mayingu
*wafanya mazungumzo na Mkurugenzi mkuu Bw Adam Mayingu
Mabosi wa Mabingwa wa Kombe la FA wa England, Arsenal, waliopo nchini
kwa ziara ya kikazi wameanza kutikisa, ambapo kampuni nyingi zinataka
ushirikiano na klabu hiyo.
Maofisa waliopo nchini ni pamoja na Mkurugenzi wa Maendeleo na
Ushirikiano, Sam Stone na Meneja Maendeleo na Ushirikiano, Daniel Willey
wanatarajiwa kukutana na uongozi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF)
Jumanne hii.
Tayari kampuni kubwa zaidi ya 20 zimetaka ushirika na Arsenal, na
majadiliano ya kibiashara yanatarajiwa kuanza mara moja, kuona ni katika
maeneo gani na kwa mfumo upi watashirikiana.
Katika ziara hiyo inayoratibiwa na Imani Kajula ambaye ni Ofisa
Mtendaji Mkuu wa EAG Group, benki mbalimbali zimetaka kufanya biashara
na Arsenal, lakini pia Quality Group, kampuni inayomilikiwa na Rais wa
Yanga, Yusuf Manji.
Stone amewaambia waandishi wa habari Jumatatu hii jijini Dar es
Salaam kwamba wamejizatiti na japokuwa wamekuja kibiashara, milango ipo
wazi iwapo kuna kampuni za michezo zinazotaka kushirikiana nao na kwamba
zinaweza kunufaika.
Ujumbe huo umetua nchini huku hali ya hewa kisoka kwa klabu na timu
ikiwa shwari, baada ya Arsenal kuwafunga Manchester City mabao 2-0
Jumapili hii kwenye Uwanja wa Etihad unaomilikiwa na mabingwa hao
watetezi wa England.
Mabao ya Santi Cazorla na Olivier Giroud yakichanganywa na ulinzi
mahiri wa kitimu, vilitosha kuzikonga nyoyo za washabiki wa Arsenal
ndani na nje ya England, ambapo nchini Tanzania pia washabiki wao
walionekana wakitamba mitaani, licha ya kwamba ilikuwa usiku.
Stone alisema jijini Dar Jumatatu kwamba wanaichukulia Tanzania kwa
umuhimu mkubwa, kutokana na ukubwa wake kijiografia, mvuto wa watu wake
kwenye soka na uwapo wa kampuni kubwa na zinazoweza kushirikiana na
Arsenal.
Tayari Arsenal wana uhusiano na kampuni na taasisi nchini Kenya, Uganda, Rwanda, Afrika Kusini na Nigeria.
Post a Comment