Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

SIASA ZA UONGO NA HILA ZIMESHINDWA

NINAANDIKA haya kwa sababu nimebaini wasomaji wengi wameshiba taarifa za uongo na propaganda nyepesi kuhusu kilichotokea hata kusababisha anayeitwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jecha Salim Jecha, kutokwa na akili za kawaida, na kuamua kuchukua hatua ya “peke yake” inayoendelea kuichumia nchi mgogoro wa kisiasa.

Uchaguzi 2015
Ni hatua yake ya kufuta uchaguzi mzima wa Zanzibar – Wazanzibari walimchagua Rais, Wawakilishi na Madiwani wa wadi za Zanzibar Oktoba 25.

Tena niseme wazi ninarudia kudurusu yaliyotokea baada ya kujiridhisha kuwa nisipofanya hivi, sitakuwa nimetenda haki kwa ukamilifu wake. Kwa kutotenda hivyo, nawapa ushindi wanasiasa wachache wachovu wanaotaka kupindisha ukweli kwa maslahi binafsi ya kisiasa.

Nimewahi kuapa kwa jina la mola muumba wa vyote ardhini na angani, ndani ya uhai wangu, sitavumilia ukweli kupotoshwa, kwa yale ninayoyajua kwa uhakika wake.

Lakini pia, ninapenda kusema, nimeguswa mno na majadiliano ya Wahariri katika mjumuiko wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) kuhusu kilichotokea hata Jecha akachukua hatua ile ya peke yake.

(Ni “peke yake” kwa sababu mpaka sasa hakuna ushahidi wowote uliotolewa na yeyote ndani ya Tume kwamba alitumwa na Tume ambayo maana yake ni yeye mwenyekiti, makamu wake na makamishna kufanya alichokifanya; wala Tume haikupata kujadili suala lolote tangu wananchi walipomaliza kupigakura, hata iwe walifikia kuamua kufuta uchaguzi wote nchini.

Kitendo cha Wahariri kujadiliana kupitia gurupu lao mahsusi la WhatsApp, ni chema. Tatizo ni kuona baadhi yao wanaeneza ninachoona ni upotoshaji na propaganda ambazo ndizo zinatumiwa na uongozi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar kujenga kesi dhaifu.

Angalia, Mhariri kwa kutetea ujinga, anahusisha hatua ya Jecha kufuta uchaguzi uliogharimu karibu Sh. 9 bilioni, na hatua ya Maalim Seif Shariff Hamad, anayepigania haki yake ya kuongoza Zanzibar, kutangaza mwelekeo wa kura zake za ushindi.

Huu ni upotoshaji wa kwanza uso maana. Tuseme Maalim Seif amekosea kufanya alichokifanya Oktoba 26 asubuhi, hilo litakuwa kosa lake binafsi linalopaswa kuchukuliwa kijinai.

Ni juu ya wachunguzi wa serikali, Jeshi la Polisi, kumshughulikia. Wangemhoji, wakamrekodi maelezo, wakafungua jalada la tuhuma na kuliwasilisha kwa Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) wa Zanzibar, ambaye akiona tuhuma zina msingi na ushahidi, atafungua mashitaka dhidi yake.

Hivi adhabu inayomstahilia (kama ni sahihi) Maalim Seif aliyegombea urais na “kuchaguliwa” na wananchi kwa mujibu wa matokeo yaliyokwishatangazwa na wasimamizi wa vituo majimboni, inajuzu vipi kuangushiwa wapigakura?

Iko wapi hapo haki ya wapigakura wa Zanzibar kama wanaadhibiwa wao waliopewa haki na Katiba ya Zanzibar ya 1984, kwa kosa lisilowahusu?

Kwani wao ndio waliofanya hicho anacholaumiwa mgombea kufanya? Walifanyia wapi wananchi waliopigakura? Wanasingiziwa ubaya usiowahusu. Kwa hakika watu wasio na hatia yoyote zaidi ya kutumia haki yao ya kikatiba, wanadhalilishwa isivyostahiki.


Maneno niliyoyawekea wino mzito nataka yaeleweke vizuri. Wale wanaojenga hoja ya kumlaumu Maalim Seif na kumtia makosani eti amejitangaza mshindi, wajue kwamba kila kituo cha uchaguzi kilichokuwa na wapigakura wasiozidi 350, kilihesabu kura za urais, pamoja na zile za uwakilishi na udiwani.

Na wakahesabu za Rais wa Jamhuri na Wabunge.

Msimamizi alijaza fomu za kura hizo, akawasainisha mawakala wote waliokuwa kituoni, naye akasaini. Akabandika fomu ukutani nje kwa ajili ya umma kujua. Waangalizi, kama tulivyoshuhudia waandishi wa habari, nasi tuliangalia kuthibitisha kile tulichoshuhudia wakati kura zinahesabiwa na kujumlishwa majimboni.

Katika hali kama hiyo, ni nani katangaza matokeo? Ni nani alitangulia kuyatangaza matokeo ya kura za urais? Asemaye ni Maalim Seif, huyo ana lake dhidi ya mwanasiasa huyu kipenzi cha umma.

Maalim Seif, mgombea urais, alipata fomu za majimbo yote 54 (majimbo 18 Pemba na 36 Unguja). Asipate vipi wakati sheria ya uchaguzi inaruhusu na safari hii timu yake ilisimamia kijasusi zipatikane kupitia mawakala wake vituoni? Akajumlisha kura za majimboni, akaona anatimiza idadi ya kura za kumshinda Dk. Ali Mohamed Shein. Tunaelewana?

Labda hamjui nyie, viongozi wa CCM wanatafutana uchawi, ni nani aliruhusu Maalim Seif azipate fomu za majimbo yote? Hamjui baadhi ya mawakala wa CUF walikimbizwa kiroho mbaya na mazombi (askari wasio nidhamu wa serikali) wazisalimishe fomu zisimfikie mgombea. Walichofanikiwa siku zote CCM, kimewashinda safari hii; wanalizana mjue!

Mhariri mzima anashauri kwa njia ya swali, “Maalim Seif akamatwe?” Nani amezuia hili kutendwa?

Kwanini asikamatwe kama amekosa; hata mara moja hajajiweka juu ya sheria. Anakamatika na kushitakika. Mbona ameshashitakiwa sana.

Maalim Seif amekaa gerezani pasina kuhukumiwa na mahkama. Huyu ni mpigania haki za Wazanzibari na nchi yao, hahofii mahkama wala gereza. Amepata kuyasema haya hadharani. Hajabadili kauli.

Juma Duni Haji, mwanasiasa mahiri kwa lugha ya kujengesha hisia wananchi, na kuzidodosa takwimu na tawala dhalimu Tanzania, ameshasema haya mara kadhaa. Nimeyasikia kwenye kampeni za uchaguzi uliofanyia mwezi uliopita.

Hawa wawili wamesema sana hawaogopi yote mawili – mahkama na gereza. Duni alikaa gerezani miaka mitatu mfululizo wakati huo alishatuhumiwa kuua askari mjini Wete, Mkoa wa Kaskazini Pemba, katika siku ambayo kwa hakika alikuwa mjini Unguja.

Maalim Seif alishakaa gerezani sana tu. Alisingiziwa kumshika askari shababi (kijana barubaru) na kumnyang’anya bunduki akiwa na wafuasi wake kadhaa eneo la Jang’ombe. Wenyewe wanasema wameshauawa bado kuzikwa.

Juwa usiyejua kwamba Sheria ya Uchaguzi Na. 11 ya Zanzibar ya 1984, Kifungu 88, inamtaka msimamizi wa uchaguzi jimboni “(a) haraka atamtangaza mgombea aliyepata wingi wa kura halali zilizopigwa kuwa amechaguliwa; na (b) atapeleka taarifa ya maandishi kwa mgombea aliyeshinda; na (c) atatoa taarifa ya matokeo kwa Tume, nayo itayapeleka matokeo, pamoja na idadi ya kura alizopata kila mgombea katika jimbo kutangazwa katika Gazeti Rasmi.”

Ni hawa wasimamizi walikuwa na matokeo ya kura za urais wakawasilisha Tume wakiwa wameshabandika fomu kwenye kuta za vituo majimboni. Walikuwa wameshathibitisha matokeo ya uchaguzi kwenye maeneo yao.

Hatua hiyo imefanywa pasina malalamiko ya mgombea yeyote akiwemo wa CCM. Ila wakubwa watatu wa CCM walifika Tume Oktoba 27, na barua ya malalamiko. Walisikilizwa, waangalizi wakiwepo, lakini wakatoka kapa, hakuna walichokipata.

Hapo, wakaandaa hila – eti makamishna walipigana ngumi, kura zilizidi wapigaji, nyingine ziliokotwa mitaani, eti Maalim Seif alitoka Afrika Kusini na kura bandia.

Kote hawana hoja ya kisheria. Kote wamejidhalilisha na kuumbuka. Hata mpango wao wa kuchakachua matokeo kisiwani Pemba ulishindwa baada ya kukosa wakala wa kuwasaidia kutengeneza matokeo ya kumpiku Maalim Seif.

Kilichobaki baada ya njia hizo kushindwa, ni kimoja tu – yale ya kutokabidhi serikali kwa vikaratasi. Walisema na kurudia, si kada mmoja wala wawili, wengi wao. Wakamtweza nguvu Jecha akafanya ujecha wake, leo amebakia peke yake ndani kwake, nje hakutokeki, kuchungu. Wao wasema wamsubiri atangaze siku ya uchaguzi mpya. Haweshi ubabe, na ndiyo demokrasia yao. Hawa kwa siasa chafu hawawezekani.

Chanzo: MwanaHalisi
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top