Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

UTATA WAIBUKA VYETI KIDATO CHA SITA 2015

Katibu Mtendaji wa Necta, Dk, Charles Msonde.
Baraza la Taifa la Mitihani (Necta), limeagiza kusitishwa kwa ugawaji wa vyeti vya kidato cha sita kwa wanafunzi waliohitimu mwaka 2015, huku vile vilivyokwisha gawanywa kwa watahiniwa hao vikitakiwa kurejeshwa kwenye chombo hicho.
 
Hali hiyo imeibua utata mkubwa, huku baadhi ya wadau wakiwamo maofisa elimu, wakihisi hatua hiyo ya Necta huenda inalenga kuvibadili vyeti hivyo kutoka kwenye mfumo wa wastani wa alama (GPA), kwenda kwenye ule wa jumla (division).
 
Hata hivyo, Katibu Mtendaji wa Necta, Dk, Charles Msonde, alipoulizwa na Nipashe jana alikanusha vikali madai hayo, akisema  vyeti hivyo havitabadilishwa kutoka kwenye mfumo wake bali vimesitishwa kugawanywa ili baraza lijiridhishe na baadhi ya vitu.
 
MAOFISA ELIMU, WAKUU WA SHULE
Ofisa Elimu Mkoa wa Dodoma, Juma Kaponda, alipoulizwa na Nipashe jana kama amepokea agizo hilo, alithibitisha kuwa shule zote za mkoa huo zenye kidato cha tano na sita zimepewa taarifa ya kutakiwa kurudisha vyeti hivyo Necta. 
Alisema sababu ya kuvirudisha vyeti hivyo anadhani ni kufanya mabadiliko kutoka GPA na kurudi kwenye divisheni.
 
Ofisa Elimu Mkoa wa Arusha, Nestory Mloka, alisema amepata barua ya maelekezo hayo kutoka Necta ikimuelekeza kuwataka maofisa elimu wilaya wawasiliane na wakuu wa shule za kidato cha tano na sita wasigawe vyeti vya wanafunzi waliohitimu mwaka 2015.
 
Mkuu wa Shule ya Sekondari ya St. Matthew iliyoko Kongowe, Mkuranga mkoani Pwani, Abraham Shafuri, naye alikiri kuwapo kwa agizo la Necta la kusimamisha utoaji wa vyeti hivyo kwa wahusika. 
 
Alisema aliambiwa na maofisa wa Necta kuwa vyeti hivyo vinatakiwa kurejeshwa  kwenye baraza hilo na kwamba sababu zilizotolewa ni kuwa kuna marekebisho kidogo yanabapaswa kufanyika. 
 
“Nilichoambiwa ni kwamba shule karibu zote za Dar es Salaam zimesharejesha vyeti hivyo na kwamba kwa sisi wa mkoa wa Pwani, maofisa hao watapita kuvichukua lakini hatujui ni lini watakuja,” alisema Shafuri.
 
 Katika Manispaa ya Moshi, mmoja wa wakuu wa shule za sekondari ambaye hakutaka kutajwa jina lake, aliithibitishia Nipashe kwamba wameagizwa na serikali kuvirejesha vyeti hivyo, ikielezwa kwamba vinahitaji kufanyiwa maboresho.
 
"Ni kweli tumeagizwa hilo na kesho (leo) asubuhi naletewa barua, kwa hiyo nafikiri nitakuwa katika nafasi nzuri ya kulizungumzia baada ya kuiona rasmi," alisema mkuu huyo wa shule.
 
Mmiliki mmoja wa shule ya sekondari na chuo cha ualimu binafsi, ambaye aliomba hifadhi ya jina lake, alisema ni kweli wamepata taarifa ya kutotoa vyeti hivyo na kama wamevitoa kuhakikisha vinarejeshwa.
Hata hivyo, alisema kwa taarifa alizosikia ambazo si rasmi ni kwamba vinatakiwa kubadilishwa kutoka  GPA na kuwa kwenye mfumo wa Divisheni.
 
"Lakini serikali inatakiwa kujua kwamba ikifanya hivyo, hilo ni kosa la jinai, kwani hata walivyofanya kwa matokeo ya kidato cha nne kutoka kwa mfumo wa divisheni badala ya GPA, ni kosa la jinai pia kwa kuwa wanafunzi hawakujiandaa kwa mfumo huo," alisema huku akiomba hifadhi ya jina lake na kuongeza:
 
"Unajua huu ni usumbufu mkubwa, kwani kuna wanafunzi wengine wapo Urusi na kwingineko nje ya nchi wanasoma na huko waliomba kozi zao kwa kutumia 'transcript' ambazo zinaonyesha mfumo wa GPA, sasa baadaye wakipeleka vya Divisheni si wataonekana wanadanganya. Huu ni usumbufu mkubwa hauna maana kwa sasa, ni bora kuacha mfumo uliopita ubaki kama ulivyo."
 
Mkuu wa Shule ya Sekondari Aruisha,  Christopher Malamsha, alithibitisha kupokea maagizo ya ofisa elimu wilaya ya Arusha kumweleza wazuie vyeti kidato cha sita lakini sababu hawajaambiwa.
 
MZAZI
Kwa upande wake,  Audax Rusenene, ambaye ni mzazi wa mwanafunzi aliyehitimu kidato cha sita mwaka jana kwenye Shule ya Wasichana ya Feza,  alisema uongozi wa shule hiyo umemtaka mwanaye anayesoma Chuo Kikuu cha Stelenbosch kilicho Afrika Kusini,  arejeshi cheti chake.
 
“Mtoto wangu alienda chuo Januari 17, mwaka huu, lakini nashangaa hivi karibuni kupigiwa simu na msaidizi wa mkuu wa shule aliposoma mwanangu na kutaka arudishe cheti,” alisema na kuongeza: 
 
“Nilipomwambia kwamba mtoto yupo chuo Afrika Kusini, akaniambiwa niwasiliane naye akirudishe kwa sababu hilo ni agizo la serikali.” 
 
“Hiki kitu kinasikitisha kwa sababu kama kuna mabadiliko yatafanywa kwenye cheti wakati alama alizopata ndizo zilizofanya akapata chuo unadhani itakuwaje?.”
 
Alisema mtoto wake huyo alihitimu kidato cha nne mwaka 2012 kwenye Shule ya St. Francis na kukumbwa na kufutwa kwa  matokeo yake na sasa anatakiwa tena arudishe cheti chake cha kidato cha sita.
 
NECTA YANENA
Akifafanua jambo hilo, Dk. Msonde alisema: “Baraza halijaagiza vyeti virudishwe ili vibadilishwe mfumo (GPA), baraza lilichokielekeza ni utaratibu wa kawaida wa baraza la mitihani kuangalia uhalali wa vyeti vyake, serial namba ya vyeti vyake na kujiridhisha kama vyeti hivyo vimetawanyika sawasawa.
 
“Vyeti hivi baraza limevigawa hivi karibuni na lilichofanya sasa limezuia kwanza shule zisigawe mpaka litakapotoa maelekezo mengine, msingi huo wa kuzuia uko kwenye hoja ya kuhakikisha tu kwamba linajiridhisha kwenye takwimu zake kama zimekaa sawasawa katika vyeti vilivyokwenda kila shule.”
 
“Baadhi ya vyeti kwenye mkoa wa Dar es Salaam vipo Necta, lakini kwenye mikoa mingine yote viko shuleni,” alisema Dk Msonde.
Aliongeza kuwa, “Kama mkuu wa shule alikuwa amegawa vyeti viwili, vitatu kabla havijarejeshwa baraza ni suala jingine, lakini kiujumla kinachofanywa na baraza hapa ni kuhakiki cheti hiki, kama vimekaa kama utaratibu wetu ulivyo.”
 
Alisema suala la kubadilisha kutoka kwenye GPA kwenda kwenye divisheni halipo na kwamba matokeo yaliyotangazwa kwa utaratibu wa GPA vyeti vyake vitaendelea kuwa katika mfumo wa GPA na matokeo yaliyotangazwa kwenye utaratibu wa divisheni vyeti vyake vitabaki kuwa kwenye divisheni.
 
Alisema kwa wale ambao tayari wako nje ya nchi, hakuna atakayeathirika na kama baraza likihitaji cheti chake litafanya utaratibu wa kukipata.
 
Habari hii imeandaliwa na Fredy Azzah, Dar,  Agusta Njoji, Dodoma,  Godfrey Mushi, Moshi, John Ngunge, Arusha.
CHANZO: NIPASHE
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top