Picha mbili za kwanza zinamuonesha Ofisa wa Juu wa Polisi 
(mwenye shati ya kitenge) akimsaidia Lipumba na mabodigadi wake kuvamia 
Mkutano Mkuu wa Taifa wa CUF.
 Picha ya pili na ya tatu 
zinaonesha wajumbe Mkutano Mkuu wa CUF wakihesabiwa ili kuamua ikiwa 
Lipumba ANAONDOKA au ANABAKI.
Na. Mtatiro J
 1. Akidi ilitimia pande zote, Bara na Zanzibar na mkutano ulimchagua 
Ndugu. Julius Mtatiro kwa kura takribani 500 kuwa Mwenyekiti wa Kikao, 
alifuatiwa na Ndugu. Ridhiwani wa Morogoro aliyekuwa na kura takribani 
170 na hivyo ndugu Mtatiro alipitishwa rasmi kuongoza mkutano.
 2.
 Mkutano Mkuu kwa kauli moja ulipitisha ajenda mbili: Moja ni Taarifa ya
 Barua ya Kujiuzulu kwa Prof. Lipumba na mbili ni Uchaguzi wa Kujaza 
nafasi wazi za Mwenyekiti Taifa, Makamu Mwenyekiti Taifa na Wajumbe 
wanne wa Baraza Kuu.
 3. Mkutano Mkuu ulianza ajenda ya kwanza 
chini ya Uenyekiti wa ndugu Mtatiro ambapo Katibu Mkuu wa CUF, Maalim 
Seif Sharif Hamad alipewa ruhusa ya kueleza taarifa ya kujiuzulu kwa 
Prof. Lipumba na alieleza jambo hilo kwa kina, hatua kwa hatua.
 
4. Baadhi ya wajumbe wa Mkutano Mkuu wa CUF wapatao 10 kutoka Tanzania 
Bara walitoa hoja zao kwa kutaka Kikao kimuite Prof. Lipumba ili aje 
ajieleze kuhusu kujiuzulu kwake jambo ambalo lilipingwa na wajumbe 
wengine. Mwenyekiti wa kikao aliwataka wajumbe wanaotaka Lipumba aletwe 
waweze kueleza kifungu cha katiba au kanuni kinachotaka Kiongozi 
aliyejiuzulu yeye mwenyewe aitwe kujieleza, wajumbe hao walishindwa 
kutoa mamlaka ya kikatiba au kikanuni. Wajumbe waliokataa Prof. Lipumba 
kuja mkutanoni walinukuu ibara ya 117(2) ambayo inataka taarifa ya 
kujiuzulu kwake ndiyo ipelekwe kwenye mkutano mkuu na siyo yeye 
mwenyewe. Mwenyekiti wa kikao aliujulisha mkutano kuwa Prof. Lipumba si 
mjumbe wa kikao kwa hiyo hawezi kuitwa kwa sababu yoyote ile na kwamba 
mkutano ujadili barua zake na ufanye maamuzi ya kumrudisha au 
kutomrudisha.
 5. Baadhi ya wajumbe wa mkutano mkuu wa CUF kutoka 
Tanzania Bara walikataa Mkutano Mkuu usifanye maamuzi yoyote. Wajumbe 
wengine wa Bara walitaka maamuzi yafanyike, kwa hiyo Tanzania Bara 
iligawanyika nusu kwa nusu kwenye jambo hilo. Hofu ya wajumbe wa Bara 
waliokataa maamuzi yasifanywe ilikuwa ni kuwa yakifanyika yataathiri 
mipango yao.
 6. Majira ya saa 8 mchana wakati mkutano ukiendelea 
na baadhi ya wajumbe wa bara wakiomba mkutano mkuu umuite Prof. Lipumba,
 ndipo Profesa alipojitokeza akiwa na kundi la MABAUNSA wapatao 30 
wakisindikizwa na Ofisa wa POLISI aliyekuwa na RADIO CALL (Angalia picha
 ya ukurasa wa mbele gazeti la Mtanzania). Kundi hilo liliwazidi nguvu 
walinzi wapatao 10 waliokuwa kwenye lango kuu na hivyo Prof. Lipumba 
akaingia mkutanoni kwa nguvu na kuketi upande mmoja na "genge" lake. 
Baadhi ya wajumbe wa bara wapatao 150 hivi kati ya 320 waliohudhuria 
walisimama na kushangilia ujio wa Lipumba kwa dakika kadhaa. Mwenyekiti 
wa Mkutano aliwatuliza 
 7. Mwenyekiti wa Mkutano aliwajulisha 
wajumbe kwamba kwa hatua iliyopo lazima wafanye uamuzi aidha wa 
kumrejeshea uenyekiti Lipumba au kumuondoa kabisa, kwa kupiga kura. 
Wajumbe walewale takribani 150 wa Bara waliendelea kupinga kitendo 
chochote cha kupiga kura, wakitaka mkutano mkuu umuidhinishe Lipumba 
kurudi kwenye uenyekiti "kienyeji" na bila kutumia kura.
 8. 
Mwenyekiti wa Mkutano alitoa OPTION ya pili kwamba Mkutano Mkuu uache 
ajenda ya kwanza uhamie ajenda ya pili na kufanya uchaguzi wa Makamu 
Mwenyekiti wa chama na ule wa wajumbe wanne wa baraza na kwamba Mjadala 
juu ya Lipumba uahirishwe na pia uchaguzi wa nafasi ya Mwenyekiti 
uahirishwe. Wajumbe wa bara walewale takribani 150 kati ya 320 walikataa
 OPTION hii ya pili wakasimama na kupiga makelele kuwa Lipumba arudishwe
 bila uamuzi wa kikatiba wa Ibara ya 112.
 9. Mwenyekiti wa 
Mkutano Ndg. Julius Mtatiro aliuahirisha mkutano kwa zaidi ya saa moja 
ili wajumbe wakapate chakula. Katika muda huo wa mapumziko viongozi wa 
kitaifa wa CUF waliwasiliana na viongozi wa jeshi la Polisi kuanzia 
kanda, mkoa, wilaya ili kujua ni kwa nini polisi waliokuwepo walimruhusu
 na kumsindikiza Lipumba ukumbini na kutaka kujua ni kwa nini 
wanashindwa kumuondoa kwa sababu si mjumbe. Polisi walieleza kuwa wanao 
ulinzi wa kutosha hapo hotelini na kwamba mkutano ukirejea wataimarisha 
ulinzi na kuzuia makundi yoyote yasiyo wajumbe kuvamia mkutano kama 
lilivyofanya kundi la Lipumba na watu wake. Polisi walikataa katakata 
kumuondoa Lipumba na genge lake ukumbini.
 10. Mkutano uliporejea,
 Mwenyekiti wa kikao aliwaongoza wajumbe kufanya maamuzi ikiwa LIPUMBA 
aondoke au abaki kwa mujibu wa katiba ya CUF ibara ya 117 (2). Wajumbe 
takribani 150 wa bara walisimama na kupinga. Wajumbe takribani 130 wa 
bara na wajumbe takribani 340 wa Zanzibar walipiga kura na kuamua kuwa 
Lipumba AONDOKE RASMI. Jumla ya wajumbe waliomuondoa Lipumba ni kwa kura
 zilizphesabiwa rasmi ni 476 huku waliosema ASIONDOKE wakiwa 14 tu. 
Wajumbe takribani 150 hususani kutoka Tanzania Bara walikataa kushiriki 
katika upigaji kura lakini wasingeliweza kuathiri akidi au maamuzi. 
Baada ya uamuzi huo muhimu na ukilishwaji wa ajenda ya kwanza, 
mwenyekiti wa kikao alikiahirisha kwa saa nzima.
 11. Kikao 
kiliporejea saa 1 jioni hivi, Mkutano Mkuu ulihamia kwenye ajenda ya 
pili ya Uchaguzi wa Nafasi ya Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti na Wajumbe 
wanne wa Baraza. Mwenyekiti wa kikao alimkaribisha Mwenyekiti wa 
Uchaguzi wa ndani ya chama Wakili msomi Awadh Said akisaidiwa na Wakili 
msomi Job Kralio ili waongoze shughuli uchaguzi. Wakili awadh alitoa 
taarifa ya utangulizi akawatambulisha wajumbe wa kamati yake na 
wakajipanga mbele ya wajumbe.
 12. Wakati Wakili Awadhi 
(Mwenyekiti wa Uchaguzi) akiendelea na zoezi lake, wajumbe wale 150 wa 
Tanzania bara walisimama wakijaribu kuzuia uchaguzi usifanyike. 
Mwenyekiti wa Mkutano Mkuu aliwatuliza na wakamsikiliza lakini ghafla, 
milango mikuu ya Blue Pearl ilivamiwa na kundi la vijana zaidi ya 200 
wakitokea nje, vijana hao wavamizi ambao kwa vyovyote vile lazima 
walikuwa wamekodiwa kwa ajili hiyo, waliwazidi nguvu walinzi wetu wa 
mlangoni wakaingia ukumbini.
 13. Polisi kikosi kizima waliokuwepo
 hawakufanya chochote baada ya hali hiyo, wameshuhudia makundi ya watu 
wasio wajumbe wakiingia ukumbini na wamewaacha wafanye hivyo bila 
kuwazuia. Viongozi wa Polisi waliokuwepo "walitorokea mlango wa pili" 
immediatelly baada ya kundi la wahuni kuvamia.
Kundi lile lote likawa limo ukumbini ukijumlisha na lile kundi la Lipumba na mabodigadi wake wa kukodi. Kundi jipya la wavamizi mia mbili lilianza kuleta vurumai kwa kupiga baadhi ya wajumbe wa mkutano mkuu (wajumbe kamwe hawakupigana wao kwa wao, hata mara moja, walivamiwa kutoka nje na wahuni na baadhi ya wajumbe kunyang'anywa viti na kupigwa au kutishiwa kupigwa).
Kundi lile lote likawa limo ukumbini ukijumlisha na lile kundi la Lipumba na mabodigadi wake wa kukodi. Kundi jipya la wavamizi mia mbili lilianza kuleta vurumai kwa kupiga baadhi ya wajumbe wa mkutano mkuu (wajumbe kamwe hawakupigana wao kwa wao, hata mara moja, walivamiwa kutoka nje na wahuni na baadhi ya wajumbe kunyang'anywa viti na kupigwa au kutishiwa kupigwa).
 14. Kutokana na hali hiyo majira hayo kwa mamlaka ya 
kikatiba aliyokuwa amepewa na Mkutano Mkuu, ndugu Julius Mtatiro 
aliahirisha Mkutano Mkuu wa CUF hadi itakapotangazwa vinginevyo. Baada 
ya kuuahirisha viongozi walilindwa na kuondoka mkutanoni kwa utaratibu 
na wajumbe wa mkutano mkuu wakaongezewa ulinzi wa hoteli ili wawe 
salama.
 15. Kwa maoni yangu, pamoja na kuwa Prof. Lipumba ameamua
 rasmi kuingia vitani na chama chake tena kwa malengo halisi ya AJENDA 
NA MASLAHI YAKE BINAFSI, ukweli unabakia kuwa POLISI walikuwa ni sehemu 
ya Mkakati wa kuuvuruga mkutano wa CUF. Kama Polisi wangelitoa ulinzi 
kidogo tu, mkutano ungelifanyika na uchaguzi ungelifanyika hadi mwisho. 
Lakini USALITI wa LIPUMBA akishirikiana na VYOMBO VYA DOLA unaweza kuwa 
mzizi mkuu wa hali ya jana.
 #Note 1: Leo nimeelezea kwa kirefu nini kilitokea mkutanoni jana. Kesho ntaeleza maoni yangu binafsi kwa ujumla.




Post a Comment