
Pamoja na mapungufu yake yote, siasa Marekani ina mambo kadhaa ya kupigiwa mfano. Kinachonivutia zaidi ni mijadala inyofanyika baina ya wagombea kabla ya uchaguzi. Leo, kwa mfano, tumeshuhudia pambano la tatu baina ya Obama na Romney
Mijadala ya namna hii inawapa wapiga kura fursa ya kuwasikiliza wagombea. Vile vile naiona kama namna ya kuwaheshimu wapiga kura.
Mfumo wa Marekani unatambua kuwa wapiga kura wana haki ya kuwasikia wagombea wakiongelea masuala kadha wa kadha katika kupambanishwa na wapinzani wao.
Ninakerwa ninapokumbuka mambo yalivyo kwetu Tanzania. Ninakerwa nikikumbuka jinsi CCM ilivyotoroka midahalo mwaka 2010. Ni dharau kwa wapiga kura. Tatizo ni jinsi wapiga kura wengi walivyo mbumbumbu, wasitambue kuwa hili lilikuwa dharau. Walipiga kura kama vile hawajadharauliwa.
Hebu fikiria mambo yangekuwaje ule mwaka 2010 iwapo Kikwete angepambana na Slaa katika midahalo mitatu hivi, ambayo ingeonekana katika televisheni na kusikika redioni. Lakini tulinyimwa fursa hii, kutokana na maaumzi muflisi ya CCM.
Hakuna sababu yoyote kwa nini siku zijazo tusifanye kama wa-Marekani wafanyavyo. Watangazaji makini wa redio na televisheni tunao, ambao wanaweza wakaendesha mahojiano nasi tukapata fursa nzuri ya kuwabaini wababaishaji na kuwatupilia mbali.
Chanzo:Hapa Kwetu
Post a Comment