Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

CCM,CUF WACHAFUZI WA MAONI KATIBA

Na Sarah Mossi
Wazanzibari walisahau mambo mengine, walijikita kwenye Muungano.
VIONGOZI wa CCM na CUF Zanzibar, wanadaiwa kutibua kwa makusudi zoezi la ukusanyaji maoni ya Katiba mpya lililomalizika visiwani humo juzi na kusababisha wananchi kutoaminiana na kuheshimiana.
Viongozi hao wanatuhumiwa kufanya kampeni ya kuwashawishi wafuasi wao nini cha kuzungumza wakati Tume ilipokuwa ikichukua maoni ya wananchi kwenye maeneo mbalimbali ya Zanzibar na kusababisha kutokea vurugu zilizoacha watu kadhaa wakijeruhiwa.
Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba upande wa Zanzibar, Profesa Mwesiga Baregu, aliiambia RAI kuwa viongozi wa kisiasa Zanzibar, wamefanya kampeni kwa wafuasi wao na kuwahadaa, ili waione Tume kama mkusanyaji wa kura ya maoni kuhusu Muungano.
Akizungumza na RAI katika mahojiano maalumu mara baada ya kumaliza kazi ya kukusanya maoni Zanzibar, Profesa Baregu amesema licha ya watu wengi kujitokeza kwenye mikutano iliyoandaliwa na Tume hiyo , lakini wajumbe walishangazwa kuona maoni yalikuwa ya kuegemea katika Muungano na kusahau vipengele vingine.
Profesa Baregu alisema wananchi wengi (wafuasi wa CUF) walikuwa wamejikita kwenye hoja ya Muungano wa ‘Mkataba’ na tunadhani ndio waliosababisha vurugu katika mikutano ya Tume na wale wa CCM walijitokeza na kugusia Muungano wa Serikali mbili na kuondolewa kero za Muungano.
Profesa Baregu alisema licha ya Makamishna kujaribu kuwaelekeza wananchi wanatakiwa kutoa maoni ya mabadiliko ya Katiba na siyo ya Muungano pekee, lakini kazi hiyo ilishindikana.
“Ama kwa kutojua ama vinginevyo lakini viongozi wa siasa Zanzibar wamefanya kampeni kwa watu wao waseme nini, wamefanya kama kura ya maoni kuhusu muungano, wanafikiria namba za watu kwamba tume itaamua nani kapata wingi nani kapata wachache.
“Tuliwaeleza jambo kubwa hapa ni zoezi la kuchukua maoni ya watu, si kuhesabu wangapi wamesema nini, bado ilishindikana, hawa wa mkataba walisema tu mkataba…. mkataba, bila kutoa maoni mengine, angalau hawa waliotaka serikali mbili waligusia kero ziondolewe na hapo ndipo watu wakaanza kuzomea, kushangilia na hilo likasababisha ushabiki wa kisiasa” alisema Profesa.
Profesa Baregu alisema uzoefu alioupata katika zoezi hilo, ni kutokuwapo kwa maridhiano miongoni mwa jamii ya watu wa Zanzibar na kuelekea kugawanyika kinyume na watu wanavyofikiria.
“Tumepata viashiria ambavyo hapo baadaye tutapata mgogoro ambao utaathiri hata Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania…. iweje katika Serikali ya maridhiano, lakini huyaoni hayo maridhiano yenyewe?
“Ni muhimu sasa viongozi watafute muafaka katika jamii na namna ya kuondoa uhasama wa waziwazi ambao si mzuri kwa hali ya baadaye….Kuna umuhimu wa kujenga kuaminiana kati ya watu na kuelewa wote wataishi katika Zanzibar na lazima itafutwe namna ya kuishi pamoja bila ugomvi na kuheshimiana” alisema Profesa Baregu.
Hivi karibuni wakati Tume ya Mabadiliko ya Katiba ikiwa katika hatua za mwisho kupokea maoni ya wananchi wa Zanzibar juu ya mabadiliko ya katiba mpya kulitokea vurugu kwenye maeneo mbali mbali ya Wilaya ya Mjini Unguja na kusababisha baadhi ya watu kujeruhiwa kwa kuchomwa visu.
Vurugu hizo zilizotokea katika mikutano ya kukusanya maoni, zilidaiwa kusababishwa na wanasiasa na kulazimisha Makamishna wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba kusitisha mikutano.
Hali iliyojitokeza katika mikutano hiyo ya Katiba, imeashiria kutokuwapo kwa kutovumiliana kisiasa miongoni mwa jamii ya Wazanzibari kunakochangiwa na viongozi wa vyama vya siasa vikuu visiwani humo CCM na CUF.
Julai 31, 2010, Zanzibar iliingia katika ukurasa mpya wa kisiasa barani Afrika baada ya wananchi wake kupiga kura ya maoni kubadili katiba ili kuruhusu uundwaji wa serikali za kuwagawana madaraka.
Kura hiyo iliungwa mkono na vyama vyote vikuu vya siasa visiwani humo CCM na CUF wakiwa na lengo la kumaliza mgogoro wa kisiasa uliodumu tangu ulipofanyika uchaguzi mkuu wa kwanza katika mfumo wa vyama vingi vya siasa uliofanyika 1995.
Katika uchaguzi huo ambao upande wa CCM, alisimama kuwania kiti cha Urais, Dk. Salmin Amour na kwa upande wa CUFnafasi hiyo iliwaniwa na Maalim Seif Shariff Hamad. CCM ilishinda, ingawa kwa asilimia ndogo na kuacha malalamiko kutoka CUF na kusababisha kuwapo ghasia za kisiasa visiwaqni zilizodumu hadi 2010, vyama hivyo vilipoamua kuwapo kwa kura hiyo ya maoni.
Matokeo ya kura ya maoni yalionyesha asilimia 66 ya wananchi wa Zanzibar walikubali kuwapo kwa Serikali ya Maridhiano, ambayo ingeunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa, huku asilimia 34 waliokataa kuwapo kwa serikali hiyo.
Hata hivyo, wachunguzi wa masuala ya kisiasa Zanzibar, walionyesha wasiwasi wao juu ya matokeo hayo na kubainisha kuwa asilimia ya waliokataa kuwapo kwa Serikali ya Maridhiano ni ya wale ‘wahafidhina’ wa siasa za Zanzibar wasiotaka mabadiliko yoyote.
Wachambuzi hao walikwenda mbali zaidi na kusema kundi hilo linaweza kuleta taabu siku za usoni wakati Serikali ya Umoja wa Kitaifa itakayoundwa na kuifanya isiweze kufanya kazi zake kutokana na kile walichokitaka kutofanyika

Chanzo:Mzalendo.net
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top