Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

SERIKALI YAJIKANYAGA


HATUA ya serikali kushindwa kutekeleza maazimio ya Bunge kuhusu kamati mbalimbali zilizoundwa kuichunguza Wizara ya Nishati na Madili, imeibua hisia za watuhumiwa wa ufisadi kukumbatiwa, Tanzania Daima limebaini.
Bunge kama moja ya mhimili huru, hadhi yake inakuwa imeshushwa kwa kiasi fulani endapo maazimio yake yanachukua muda mrefu bila kutekelezwa na serikali au kutofanyiwa kazi kabisa, tena kwa visingizio visivyo na tija.
Kwa nyakati tofauti katika Serikali ya Awamu ya Nne, Bunge limeunda kamati teule ama kamati ndogo chini ya kamati za kudumu za Bunge, kuchunguza masuala kadhaa, huku nyingi zikiigusa Wizara ya Nishati na Madini na idara zilizo chini yake.
Hata hivyo, licha ya kamati hizo kutumia fedha nyingi za walipa kodi kwa kusafiri na kukusanya vielelezo na kuhoji watuhumiwa, bado mapendekezo yake yamekuwa hayafanyiwi kazi kwa asilimia kubwa na serikali.
Hali hii imewasononesha wabunge wengi makini, na kuwafanya kila mara kusimama bungeni na kuhoji serikali ieleze ilivyotekeleza maazimio hayo, lakini wakati wote majibu yamekuwa ya kujirudia, yasiyo na utekelezaji wa kueleweka.
Mathalani, mwaka 2008, Bunge liliunda kamati teule kuchunguza zabuni tata ya Kampuni ya kufua umeme ya Richmond LLC (sasa Dowans) chini ya uenyekiti wa Dk. Harrison Mwakyembe.
Kamati hiyo ilileta ripoti iliyoonesha ‘madudu’ yaliyofanywa na baadhi ya watendaji na viongozi serikalini, na hivyo kusababisha mabilioni ya walipa kodi kufujwa kiaina.
Licha ya mapendekezo mengi yaliyotolewa na kamati husika, utekelezaji wake umeishia kwa viongozi wa kisiasa kujiwajibisha kwa kuachia ngazi, lakini hakuna hatua za kisheria zilizochukuliwa.
Kigugumizi hicho cha serikali katika utekelezaji wa maazimio ya Richmond pamoja na Spika wa wakati huo, Samuel Sitta, kufunga mjadala huo bila suluhu kupatikana, kimeendelea kuligharimu taifa hadi leo katia sekta ya nishati.
Mwaka jana, Spika wa Bunge aliunda kamati ndogo mbili chini ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini. Moja ilichunguza uendeshaji na uendelezaji wa sekta ndogo ya gesi hususani ushiriki, ufanisi na uadilifu wa Kampuni ya Pan African Energy Tanzania Ltd (PAT) katika mchakato wa uendelezaji wa sekta ya gesi nchini kwa maslahi ya taifa.
Kamati nyingine iliangalia utaratibu uliotumiwa na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati na Madini, David Jairo, katika kuchangisha mamilioni ya fedha kwenye idara zilizo chini ya wizara hiyo kinyume, akidai ni za kusaidia bajeti yao kupitishwa.
Licha ya kamati zote kutoa taarifa yake na mapendekezo Novemba mwaka jana, ambayo yaliazimiwa na Bunge zima kuwa serikali iyafanyie kazi, bado hakuna hatua mahususi za kisheria zimechukuliwa kwa watendaji waliozembea na kusababisha hasara hizo, badala yake viongozi kadhaa walijiuzulu tu.
Mathalani, kamati iliyochunguza sakata la Kampuni ya Pan African Energy Tanzania Ltd (PAT), iliyokuwa chini ya Mbunge wa Bukene, Seleman Zedi (CCM), ilibaini kuwapo udanganyifu unaofikia jumla ya kiasi cha dola za Kimarekani milioni 64 (sawa na sh bilioni 110) ambazo kampuni hiyo ilijirudishia isivyo halali kama gharama walizotumia kuzalisha gesi tangu mwaka 2004 hadi 2009.
Kwamba kati ya fedha hizo, PAT walikiri kwamba walijirudishia isivyo halali kiasi cha dola za Kimarekani milioni 28.1; na dola milioni 36 zilizobaki wanaandaa vielelezo vya kuthibitisha uhalali wa kujirudishia gharama hizo.
Taarifa ilisema kwa mujibu wa Shirika la Maendeleo ya Petroli nchini (TPDC) na Wizara, kufikia Septemba 30 mwaka jana, PAT walitakiwa wawe wamewasilisha vilelezo hivyo, vinginevyo wakamilishe ulipaji wa fedha zote.
“Baadhi ya vitendo vya udanganyifu wa kimahesabu uliofanywa na PAT ni pale ambapo mwekezaji huyu alipokuwa akitumia fedha za Watanzania kulipia gharama za kutafuta mafuta na gesi katika nchi za Gabon, Uganda na Nigeria,” alisema Zedi.
Kwamba alikuwa akilipwa gharama za kusafirisha gesi kutoka kwa makampuni mawili tofauti ya Songas na TPDC kwa kusafirisha kiasi hicho hicho cha gesi.
Zedi alisema hadi kamati inakamilisha taarifa hiyo, ilielezwa kwa barua yenye kumb. Na CDA.90/159/01 ya Oktoba 20, 2011 kutoka TPDC kuwa PAT walikuwa wamewasilisha vielelezo vya kiasi cha dola za Kimarekani 1,042,516.
“Katika kiasi hicho wamethibitisha kuwa dola za Kimarekani 746,153 ni gharama sahihi za mradi na kiasi kingine dola za Kimarekani 296,363 zimegundulika na wamekubali kuwa ziliingizwa kwenye gharama za mradi kimakosa na kinyume cha mkataba,” alisema.
Kwamba maofisa wakuu wa PAT waliajiriwa kama wataalamu elekezi kwa nyakati tofauti na kulipwa ujira wa shughuli wanazofanya wakati pia wanalipwa mishahara mikubwa kwa kufanya kazi zao za kawaida.
Katika kuiimarisha sekta hiyo wakati huu ambapo nchi inaingia kwenye mchakato wa uchimbaji gesi, kamati ilitoa mapendekezo kadhaa, lakini makubwa yakiwa ni mkataba huo kuvunjwa.
Pia Bunge liliazimia kuwa kamati ilijiridhisha bila shaka kwamba kwa kipindi cha mwaka 2004 hadi 2009, PAT imejirudishia isivyo halali gharama zinazofikia jumla ya dola za Kimarekani milioni 28.1 sawa sh bilioni 46.3 na kufanya serikali kukosa gawio linalofikia dola za Kimarekani milioni 20.1 zirejeshwe mara moja.
Kwamba kwa kuwa mapunjo hayo ni ya muda mrefu, marejesho yake yaambatanishwe na riba kwa viwango vya benki, pia wafanyakazi wote wa PAT waliohusika katika udanganyifu huu washtakiwe kwa mujibu wa sheria.
Hata hivyo, uchunguzi wa gazeti hili umebaini hakuna utekelezaji wa maana umefanyika katika maazimio hayo ya Bunge. Hii ni kwa mujibu wa taarifa ya serikali iliyowasilishwa bungeni Aprili mwaka huu na kukataliwa na waliokuwa wajumbe wa Kamati ya Nishati na Madini iliyovunjwa.
Na kuhusu fedha zilizochukuliwa na PAT kinyemela, serikali imekuwa na kigugumizi cha kuilazimisha kampuni hiyo izirejeshe, na badala yake imeunda timu inayojulikana kama Government Negotiations Team kufanya mazungumzo.
Tanzania Daima lilimtafuta Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, kuzungumzia utekelezaji huo wa maazimio ya Bunge, lakini alisema suala hilo halifahamu na waulizwe TPDC wenyewe.
“Mimi napenda kuzungumzia mambo ya maendeleo na waandishi naomba mnisaidie kwa hilo, hizi habari za kulipuana ebu tuziache, tuangalie mbele,” alisema.
Alipobanwa aeleze kama mamilioni ya fedha za walipa kodi zilizofujwa si habari za maendeleo, Waziri Muhongo alisema kama kuna wizi ulifanyika, vyombo vya dola vipo na TPDC waliofanya makubaliano watajibu.
Waziri Kivuli wa Nishati na Madini, John Mnyika, alisema Waziri Muhongo anakwepa kujibu maazimio ya Bunge kuhusu sakata hilo na yale ya Jairo na Richmond.
“Aliwahi kunijibu bungeni nilipohoji sakata la Jairo, akasema yeye hafanyii kazi magazeti. Huyu anataka kulidhalilisha Bunge na kutufanya wabunge kuwa tunafanya mambo ya hovyo, hatuwezi kukubali watumie udhaifu huo kama uchochoro wa kulinda ufisadi,” alisema Mnyika.
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top