MBUNGE wa Ubungo Jijini Dar es Salaam (Chadema), John Mnyika amemtaka,
Rais Jakaya Kikwete kutosaini marekebisho ya sheria mpya ya mabadiliko
katika Sheria ya Ukaguzi wa Hesabu za Umma ya 2008.
Mnyika pia anakusudia kukata rufaa juu ya uamuzi wa Spika wa Bunge, Anne
Makinda kwa kutumia vibaya kanuni za Bunge kutokana na kitendo chake
cha kuzivunja kamati tatu za Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC), Hesabu
za Serikali za Mitaa (LAAC) na Hesabu za Serikali Kuu (PAC).
Akizungumza na Mwananchi Jumapili, jana, Mnyika alisema Rais Kikwete
kabla ya kusaini marekebisho hayo ambayo yanaonyesha dalili za kuwalinda
mafisadi, ajitokeze na kuwaeleza Watanzania faida na hasara ya
mabadiliko ya sheria hiyo.
Wiki hii Serikali iliwasilisha bungeni mapendekezo ya mabadiliko katika
Sheria ya Ukaguzi wa Hesabu za Umma ya 2008, huku ikiongeza vifungu
ambavyo vinapunguza nguvu ya Bunge katika kushughulikia taarifa ya Ofisi
ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).
Marekebisho hayo yamo kwenye Muswada wa Sheria ya Mabadiliko ya Sheria,
namba tatu wa mwaka 2012 uliowasilishwa bungeni na Mwanasheria Mkuu wa
Serikali, Jaji Frederick Werema.
Marekebisho hayo yanapendekeza kubadili utaratibu mzima wa kushughulikia
taarifa hiyo, kwani yanaongeza vipengele, vinavyoliwajibisha Bunge kwa
Serikali.
Serikali imeongeza vipengele vya ziada ambavyo vinazitaka kamati za
Bunge zinapofanya uchambuzi wa ripoti ya CAG, kupeleka maazimio yake kwa
Serikali ili yatafutiwe majawabu badala ya utaratibu wa sasa wa
kupeleka hesabu zake bungeni.
Mnyika ambaye pia ni Waziri Kivuli wa Nishati na Madini alisema
marekebisho hayo hayana tija kwa taifa ambalo linapigania kuwakomboa
wananchi huku likiacha mianya ya wajanja kuendelea kutumia mali za umma
bila kuchukuliwa hatua.
“Rais ndiye mwenye uamuzi wa mwisho hivyo anatakiwa kutambua kuwa
marekebisho hayo ambayo yako mikononi mwake hapaswi kuyasaini hadi pale
atakapowaeleza ukweli wananchi nia ya mabadiliko ya sheria hiyo,”
alisema Mnyika.
Mnyika amesema amemwandikia barua Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashilila
akimtaka kumpatia mtiririko wa uamuzi wa Spika Makinda wakati
alipotangaza kuvunja kamati tatu za Bunge ili aweze kukata rufaa.
Alisema amekuwa akitaka kufanyika kwa mabadiliko ya kanuni ya Bunge ya
152 (3) inayompa mamlaka Spika kuchukua uamuzi peke yake pasipo
kushirikiana na mtu mwingine.
“Spika Makinda amezivunja kamati tatu kwa kutumia kanuni ya Bunge 152
(3), wakati huo huo licha ya kwamba amezivunja lakini bado zinatambulika
katika kaununi hiyo hiyo ya Bunge ya 114 (11). Sasa sijui Spika
ameliona hili au la,” alisema Mnyika.
Alisema atatumia sheria za kanuni za Bunge 5 (4) inayompata uhuru Mbunge
kukata rufaa kama hajaridhika na uamuzi wa Spika ili hatua zaidi
zichukuliwe.
Juzi Spika Makinda alitangaza mabadiliko ya kamati za kudumu za Bunge,
huku Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma (POAC) iliyokuwa ikiongozwa
na Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe kufutwa.
Kutokana na mabadiliko hayo, shughuli za POAC sasa zitaendelea kufanywa
na Kamati ya Hesabu za Serikali (PAC) ambayo itaendelea na jukumu lake
la msingi la kuchambua taarifa ya CAG pia kwa Serikaki Kuu.
Chanzo: Gazeti la Mwananchi
Post a Comment