MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Philip Mangula
jana aliwaonya makada wa chama hicho ambao wameanza mbio za kuusaka
urais kupitia chama hicho katika uchaguzi mkuu ujao, kwamba
hawatavumiliwa.
Mangula, ambaye ni Makamu kwa upande wa Tanzania
Bara, aliwaambia wajumbe wa Halmashauri Kuu (NEC) ya CCM kwenye semina
mjini Dodoma kuwa chama hicho hakiko tayari kuona kinagawanyika tena
vipande kutokana na makundi ya kuusaka urais wa 2015, na kwamba
watakaofanya hivyo watachukuliwa hatua za kinidhamu.
Habari kutoka ndani ya semina hiyo iliyoendeshwa
chini ya Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete zilimnukuu Mangula
akisema ili kuepuka viongozi kupita kwa rushwa au hila, ni lazima
maadili ya chama hicho yazingatiwe na vikao vyote vinavyochuja au kuteua
wagombea wa uongozi katika nafasi mbalimbali ikiwamo nafasi ya Rais.
“Ili tuweze kupata ufanisi katika chaguzi zetu,
sharti tuepuke kasoro zote zinazogusa maadili ya chama na zile za
utendaji ambazo zinawezesha watu wasiostahili kuchaguliwa kupenya kwenye
uongozi kwa rushwa au kwa hila,” alinukuliwa Mangula, ambaye pia ni
Mwenyekiti wa Kamati ya Maadili ya chama hicho.
Kauli ya Mangula imekuja wakati ambao baadhi ya
wanaCCM wanatajwa kuwa tayari wameanza maandalizi ya kuwania kwenda
Ikulu na kwamba uchaguzi mkuu wa ndani ya chama hicho uliomalizika
mwishoni mwa mwaka jana ulitumika kupanga safu ya kutimiza azma hiyo.
Miongoni mwa watu ambao wamekuwa wakitajwa kuwania
nafasi hiyo ya juu ya uongozi wa nchi kupitia CCM ni Waziri Mkuu wa
zamani, Edward Lowassa, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa
Kimataifa, Bernard Membe, Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki,
Samuel Sitta na Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli.
Spika wa zamani, Sitta mbali na kutajwa kuwa
katika kinyang’anyiro hicho, pia alinukuliwa na gazeti hili hivi
karibuni akisema kwamba anafaa kuwa Rais.
Jana Mangula akiwasilisha mada kuhusu maadili
ndani ya CCM, alinukuliwa akisema kwamba atatumia Kamati ya Maadili ya
chama hicho itakayoundwa kuhakikisha kwamba chama hicho hakipasuki
kutokana na mnyukano wa siasa za urais.
“Tumeshasema ni mwiko kwa kiongozi au mwanachama
yeyote wa CCM kuunda vikundi visivyo rasmi ndani ya chama au kushiriki
katika kampeni za uchaguzi za chinichini kinyume na ratiba ya uchaguzi
na taratibu rasmi zilizowekwa,” alisema Mangula kwenye mada yake hiyo.
Habari zaidi zilisema kuwa makamu mwenyekiti huyo alisema vikundi ambavyo vimekuwa vikianzishwa na wanaowania uongozi ukiwemo urais, ndiyo chimbuko la kukigawa chama hicho vipandevipande.
Habari zaidi zilisema kuwa makamu mwenyekiti huyo alisema vikundi ambavyo vimekuwa vikianzishwa na wanaowania uongozi ukiwemo urais, ndiyo chimbuko la kukigawa chama hicho vipandevipande.
Kanuni za uchaguzi
Mangula aliapa kwamba Kamati ya Maadili ambayo yeye anahusika nayo, itavalia njuga kusambaratisha makundi na kuhakikisha tabia hiyo inakoma.
“Moja ya mambo yanayoleta mpasuko katika chama ni makundi ambayo huundwa kinyume cha utaratibu uliowekwa na NEC. Iko miiko ya kuzingatiwa wakati wa shughuli za uteuzi na uchaguzi. Miiko hiyo imepuuzwa na baadhi ya wanachama kwa makusudi au kutokuelewa,” alisema Mangula.
NA MWANANCHI
Mangula aliapa kwamba Kamati ya Maadili ambayo yeye anahusika nayo, itavalia njuga kusambaratisha makundi na kuhakikisha tabia hiyo inakoma.
“Moja ya mambo yanayoleta mpasuko katika chama ni makundi ambayo huundwa kinyume cha utaratibu uliowekwa na NEC. Iko miiko ya kuzingatiwa wakati wa shughuli za uteuzi na uchaguzi. Miiko hiyo imepuuzwa na baadhi ya wanachama kwa makusudi au kutokuelewa,” alisema Mangula.
NA MWANANCHI
Post a Comment