Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

TCD YAJITOSA KUSULUHISHA MGOGORO WA DINI

Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD)  kinatarajia kuwakutanisha viongozi wa dini, serikali pamoja na watu mashuhuri kwa ajili ya kujadili  mstakabali wa amani nchini kuanzia Aprili 23 hadi 24, mwaka huu.
 
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa TCD, James Mbatia ambaye pia ni Mbunge alisema wameamua kufanya hivyo kutokana na kuwapo kwa tishio la kutoweka kwa amani linalosababishwa na tofauti za kidini.
 
Mwenyekiti huyo alisema kuwa tayari taasisi hiyo imeshazungumza na viongozi wa dini na serikali na wamekubali kuhudhuria mkutano huo.
 
Mbatia ambaye pia ni Mbunge wa kuteuliwa, alisema kumekuwapo na viashilia vya kutoweka kwa amani nchini kutokana na matukio kadhaa ya vurugu hususani baina ya waumini wa dini ya Kikristo na Kiislamu.
 
“Watanzania tulijengwa kuishi katika misingi ya kuwa na sauti moja, kwamba kila mtu unayemuona ni ndugu yako na hakuna aliyejitokeza akasema mimi ni wa kabila wala dini fulani. Tulijivunia katika hili hata tunapokwenda katika nchi nyingine tulionekana watu wa amani,” alisema Mbatia na kuongeza:
 
“Lakini jambo la kushangaza na kutia wasiwasi hivi sasa ni kutokana na kuzuka kwa kasi kubwa ya chokochoko na mifarakano ya hapa na pale katika nchi yetu ambayo hatukuizoea hasa zinazosababishwa na imani za kidini, mfano zile za kugombania kuchinja,” alisema.
 
Aliongeza: “Chokochoko hizi hazina tija yeyote kwa taifa na hakuna atakayenufaika nazo isipokuwa tutaangamia sote kama hatutafanya jitihada za kuzikomesha.”
 
Mbatia alisema licha ya baadhi ya watu mbalimbali wakiwamo viongozi wa dini na siasa kulizungumzia suala hilo, lakini hatua za makusudi za kuhakikisha vuguvugu hizo zinakomeshwa hazijafanyika.
 
“Tumeshuhudia viongozi mbalimbali wakiwa wanazungumzia sana suala hili la tofauti za kidini ambazo zinaendelea nchini, lakini hatujaona hatua za makusudi za kukomesha vitendo hivyo  kwa vitendo zaidi ya kuzungumza tu.  
 
“Chondechonde ninawaomba Watanzania wenzangu tusichezee amani yetu, tusikubali wala kumruhusu mtu yeyote anayetaka kuivuruga na anayejaribu kutuchonganisha tumzomee sote,” alisema.
 
“Kwa nini watu tupoteze muda mwingi katika mambo yasiyo na tija badala ya kufikilia mambo ya msingi. Kwa mfano, Mbeya watu wanabishania kuchinja kwa kuonyesha jinsi gani hatuko serious (makini) wakati dunia ni kama kijiji. Wanatushangaa sana. 
 
Tabia inayoendelea ya watu kukalia umbeya tu na kujadili  tukio moja baada ya jingine na kusahau hoja za msingi tunapotea,” alisisitiza Mbatia.
CHANZO: NIPASHE
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top