Na Fidelis Butahe, Mwananchi
Dar es Salaam. Rais Jakaya Kikwete amesema suala la kupigwa marufuku
kusambazwa kwa gazeti la The EastAfrican Tanzania, linafanyiwa kazi na
taratibu zote zikikamilika, litaruhusiwa.
Rais wa Shirikisho la Ujerumani, Joachim
Gauck, akiongozana na mwenyeji wake, Rais Jakaya Kikwete, akisalimia
wakazi wa jijini, Dar es Salaam alipowasili kwenye Viwanja vya Ikulu,
Dar es Salaam jana. Picha na Anthony Siame
Wiki mbili zilizopita gazeti hilo linalomilikiwa na Kampuni ya Nation
Media Group, lilipigwa marufuku kusambazwa nchini, ikiwa ni miaka 20
tangu kuanzishwa kwake kwa ajili ya kuandika habari za ukanda wa Afrika
Mashariki.
Uamuzi wa kulifungia gazeti hilo ulichukuliwa kjwa kile kilichoelezwa
kuwa limekuwa likisambazwa nchini bila ya kuwa na usajili, kinyume na
Kifungu cha 6 cha Sheria ya Magazeti, Namba 3 ya mwaka 1976.
Rais Kikwete alitoa kauli hiyo jana wakati akizungumza katika mkutano na
waandishi wa habari, Ikulu Dar es Salaam, akiwa pamoja na Rais wa
Ujerumani Joachim Gauck, ambaye yuko nchini kwa ziara ya siku tano.
Rais Kikwete alikuwa akijibu swali lililoulizwa na mmoja wa wanahabari
walioambatana na Rais Gauck, ambaye pamoja na mambo mengine alitaka
kujua ni lini gazeti hilo litafunguliwa na sababu za kupigwa marufuku.
Rais Kikwete alisema: “Lilikuwa na matatizo ya usajili, sasa wameanza
kufanya maombi na suala lao linashughulikiwa, taratibu zikikamilika
litaruhusiwa kusambazwa nchini.
Aliongeza: “Nchi hii ina magazeti mengi, lakini ya Serikali ni mawili
tu... moja linaandika kwa lugha ya Kiswahili na jingine Kiingereza
(Habari Leo na Daily News). Yapo magazeti kama Mwananchi, Tanzania
Daima, The Guardian, Nipashe, Majira na mengine mengi tu.”
Alisema Serikali inazingatia uhuru wa vyombo vya habari, lakini pia iko
makini kuhakikisha vyombo hivyo vinafuata sheria na taratibu
zilizowekwa.
“Barua ya Januari 21, 2015 iliagiza kusimamishwa mara moja kwa
uchapishaji na usambazaji wa gazeti hilo Tanzania hadi litakaposajiliwa
rasmi na Msajili wa Magazeti, Idara ya Habari,” alisema.
Chanzo: Mwananchi
Post a Comment