Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

MAKALA:LOWASSA,ANGUKO LA UPINZANI NCHINI NA HADITHI YA BORA SHETANI NIMJUAYE KULIKO MALAIKA NISIYEMJUA !


Na Dkt. Hamisi Kigwangalla
Raia Mwema Agosti 26, 2015.

Nimekuwa na siku nyingi kidogo sijaandika. Leo nikiwa Arusha nikitokea msibani Usangi kumzika Mzee wetu na muasisi wa TANU na CCM, Mzee Peter Kisumo, nilikutana na marafiki zangu wa UKAWA na tukataniana kidogo; na hapo nikasikia matumaini waliyokuwa nayo, si ya kushinda uchaguzi bali ya kukidhoofisha chama changu, Chama Cha Mapinduzi, mmojawapo alisema: ‘baada ya Oktoba CCM na uwanja wa siasa hautabaki sawa na leo…CCM haitokuwa imara na salama tena.’

Mazungumzo yale yalinifikirisha. Nikafanya tafakuri tunduizi. Nikaamua kuweka mawazo yangu kwenye rekodi.

Kwa hakika ushindi kwa CCM mwaka 2015 kwenye uchaguzi mkuu kwa nafasi za Urais, wabunge na madiwani uko wazi kabisa. CCM itapata ushindi wa kishindo. Kwa nini? Nitafafanua kwa ufupi tu hapa.

Sababu kubwa za kwa nini CCM itashinda mwaka huu ni zifuatazo; kwanza, CCM ni chama ambacho kimejengwa kwenye misingi na itikadi, na kina wanachama wengi zaidi wanaoamini kwenye itikadi na misingi hiyo kuliko wale wachache wanaokiuka, mfano mzuri ni wale wanaofanana na Ndg. Edward Lowassa ambaye aliondolewa kwenye kinyang’anyiro cha Urais bila maelezo ya kina, japokuwa wengi wa wachambuzi wa mambo ya kisiasa walibaki wakisema kwa kiasi kikubwa inawezekana ni historia yake ya kuhusika kwenye moja ya skendo kubwa kabisa za ufisadi kuwahi kutokea nchini, maarufu kama ‘kashfa ya Richmond’. Kashfa hii ilipelekea kujiuzulu kwake nafasi ya uongozi wa Waziri Mkuu.

Pili, CCM ndicho chama pekee chenye muundo thabiti wa kitaasisi – kutokea kwenye nyaraka mbalimbali zinazoeleweka, muundo wa utumishi, watumishi na ofisi, muundo wa vikao na ratiba zake, sera, itikadi, vifaa na majengo, na vitega uchumi vinavyoendeshwa kwa mfumo unaoeleweka, ukilinganisha na vyama vya upinzani vinavyoendeshwa kwa matukio – ni tukio moja baada ya jingine, hakuna mfumo wa muundo wa kitaasisi uliosimama na unaoeleweka. Vyama vingi vya upinzani vinajaribu kuanza harakati za kuunda mfumo na muundo wa kitaasisi lakini havijafika popote.

Tatu, CCM ni chama chenye wanachama wengi kuliko vyote; kwa mtaji wa wanachama zaidi ya milioni saba, ukiongeza na wapenzi, washabiki na watu wanaoamini tu kwenye uwepo wa dola imara inayotokana na CCM, kwa hakika ushindi kwa CCM ni dhahiri. Namba zina sifa moja kubwa, kuwa huwa hazisemi uongo.

Nne, CCM itashinda mwaka huu sababu imefanya kazi nyingi na zinaonekana. Sintozitaja kwenye makala hii.

Tano, CCM inafanya mabadiliko ya uongozi, sera, mikakati yake ya kuendesha shughuli zake na ina falsafa ya ‘kujikosoa na kukosoana’ na inakubali kujirekebisha ama kurekebishwa. Tofauti na vyama vingi vya upinzani, ambavyo toka vianzishwe, baadhi yavyo, mpaka leo hii havijawahi kufanya mabadiliko kwenye sera, muundo na hata sura za viongozi wake, na badala yake vinaongozwa na familia ama watu wa kanda ama kabila fulani. Ukitaka kubadilisha sura za viongozi utakumbana na hasira za waasisi hao wenye vyama hivyo.

Sita, ngome za CCM hazijatikiswa hata kidogo na haziwezi kuyumba ndani ya miezi hii miwili ya kampeni. Ushindi kwenye serikali za mitaa wa takribani asilimia 80 ni kipimo tosha kuwa bado CCM ni chama kilichojikita mpaka kwenye nyumba kumi za kila mtaa/kitongoji, na kwamba bado kinapendwa na kuaminiwa na watanzania walio wengi.

Saba, kitendo cha UKAWA kuwa tayari kumpokea na kumteua Ndg. Lowassa kuwa mgombea wao ni pigo kubwa kwao; kwanza ni kiongozi mbabe na asiyeshaurika, hawezi kukubali kuendeshwa na taratibu za vyama hivyo – anajiamini yeye ni ‘taasisi’, maarufu na ana timu ya kumfanyia kazi, tayari tunavyoongea amekwisha wakatisha tamaa wenzake aliowakuta huko, baada ya kuvijenga vyama vyao kwa jasho na damu kwa miaka zaidi ya 20, ameingia yeye tu na kateuliwa kuwa mgombea wao, na tayari ameanza kuzitenga timu za kampeni alizozikuta huko na mifumo ya uongozi aliyoikuta huko na kuanza kutumia makundi yake ya Urais aliyotoka nayo anakokujua.

Nane, kuna hiki kitu wataalamu wa mambo ya siasa wanaita ‘incumbency advantage’, yaani ‘faida ya kuwepo madarakani’. Hii peke yake, kisaikolojia, inaiweka CCM juu ya vyama vingine hata kabla hatujaanza kampeni.

Tisa, kwenda kwa Ndg. Lowassa na hatimaye kuteuliwa kupeperusha bendera ya UKAWA kunafanya kambi ya upinzani, iliyoungana, kwa mara ya kwanza kuwa kwenye upande wa kujitetea (defensive side) muda wote, nafasi ambayo hawajazoea kucheza kwenye mechi hizi, badala ya ile ya kushambulia (offensive), ambayo wameizoea. Pia kwenda kwake UKAWA na wao kumkubali kunajenga mazingira ya kuwafanya wapinzani waonekane ni wenye tamaa ya kushika dola kwa nguvu zote hata kama ni kwa kuchukua makapi; kwamba, wanataka kwenda kwenye pepo ya mwenyezi Mungu hata kama ni kwa kupitia kwa shetani!

Maana kumchukua mtu kama Ndg. Edward Lowassa kuwa mgombea wao, ambaye walitumia muda mwingi na nguvu zao zote kumchafua, na ambaye wanapaswa wamshukuru kwa kuwapa umaarufu na heshima nchini – kipindi wakimchafua, kunaondoa imani ya wananchi juu ya nguvu ya kimaadili (moral authority) ya wao kukemea ufisadi, na kunazua maswali ya uhalali wao kisiasa (political legitimacy) na maswali ya thamani yao kiitikadi na kimaadili (ideological values and integrity): kwamba, kama wiki tatu zilizopita alipokuwa akigombea kupitia CCM alikuwa shetani, na leo anagombea kupitia UKAWA amekuwa malaika, kwamba alikuwa shetani kwa miaka 8, na leo amegeuka malaika kwa kuingia UKAWA.

Kumi, Chama Cha Mapinduzi, kimeteua mgombea mzuri wa Urais. Ndg. John Pombe Magufuli anamuacha mbali Ndg. Edward Lowassa kwa sifa za kimaadili, mwonekano wa kiutendaji, imani ya wapiga kura kwenye uwezo wa kutekeleza ahadi atakazotoa, uwezo wa kuhutubia, uwezo wa kiutendaji, na rekodi ya mafanikio katika utendaji, uadilifu, elimu na hata uwezo wa kufanya kampeni na kujieleza.

Kumi na Moja, kwenda kwa Ndg. Edward Lowassa UKAWA kumefanya watu wanaoamini kwenye mabadiliko ya kweli kutokea nje waone kama wamesalitiwa maana Ndg. Lowassa si mwanamabadiliko, ni mtu wa mfumo wa kizamani (status-quo), lakini pia kumefanya wanasiasa walioupa upinzani nguvu na umaarufu kidogo walionao leo, ni kama hawajui la kusema wala la kufanya.

Ndg. Wilibrod Slaa – hatujui kama amejiuzulu wadhifa wake wa Katibu Mkuu wa CHADEMA na kama atarejea kwenye majukwaa kumsafisha Ndg. Lowassa ama ameamua kukaa kimya kabisa – yote ni machungu kwake, amsafishe ili avunje alichokijenga toka mwaka 2007 na astaafu kwa aibu? Na watanzania wamuone ni mtu asiyeamini kwenye chochote kile, ama anyamaze kimya, athibitishe kuwa aliyoyasema kwa kipindi chote hicho ni ya kweli, na kwamba wenzake ni walafi wa madaraka tu.

Profesa Ibrahim Lipumba, aliyeamua kujiuzuru wadhifa wake wa Mwenyekiti wa CUF kufuatia ujio wa Ndg. Lowassa amesema hakubaliani na uamuzi huu wa UKAWA.

Kwa hakika kuna makundi makubwa yaliyodumu kwenye ufuasi wa wanamageuzi hawa wakongwe kwa muda mrefu watakubaliana nao na hawatounga mkono UKAWA.

Kumi na Mbili, watanzania watachagua CCM kwa sababu, kwa wale wanamabadiliko walioamini kwenye mabadiliko kutokea nje ya mfumo hawatoona jipya linalokuja na UKAWA, wataona hakuna tofauti kati ya CCM na UKAWA na kwamba wataona bora hata ya CCM imekataa kwa vitendo, pamoja na vitisho vya ‘mafuriko ya kuigiza ya Ndg. Lowassa’, kwa kumkata jina na hatimaye kumuondoa kwenye mbio za Urais, kwa tuhuma za ufisadi uliokubuhu. CCM wamefanya hivyo bila kupepesa macho. Wametoa uongozi kwa nchi, wameonesha kuwa kuna mambo wanayoamini na wanayasimamia. Upinzani wamempokea na kumpa bendera yao apeperushe. Wapiga kura wataona hawa wanasiasa wote ni mashetani tu (kama kipimo cha wanasiasa ni ushetani), na watachagua bora shetani waliyemzoea kuliko malaika wasiyemjua na ambaye ameanza safari kuelekea kwenye dola kwa kusajili shetani mkubwa kuliko wote na kumwita ‘malaika’. UKAWA wamemomonyoka kimaadili (moral decay) zaidi ya CCM kwa kumpa bendera yao Ndg. Lowassa.

Kumi na Tatu, lugha ya CCM kwenye kampeni itakuwa rahisi sana kutokana na kuwa na mgombea wa upinzani wanayemjua vizuri, na lugha ya kuwasambaratisha wasemaji wote wa UKAWA itakuwa rahisi sana, maana CCM itakuwa na kauli zao wakimchafua Ndg. Lowassa alipokuwa CCM na watawakumbusha tu wananchi.

Kumi na Nne, uwezo wa kifedha wa Ndg. Lowassa utaathirika kwa sasa akiwa mgombea wa UKAWA kwa maana atahofia kutumia pesa zake nyingi kwenye kutafuta Urais kupitia upinzani hali ya kuwa anajua hana nafasi ya kushinda, pia marafiki zake waliokuwa wakimchangia kipindi akiwania Urais ndani ya CCM wamebaki CCM ama wanahofia kutengwa na CCM mara atakaposhindwa na hawana imani kuwa atashinda Urais kutokea nje ya CCM, na UKAWA hawana ruzuku ama vitega uchumi vya kulingana ama kuishinda CCM, hivyo vifaa vya kampeni (branding materials) ya CCM na uwezo wa kujitangaza utampoteza mgombea huyu mtata wa UKAWA mara moja kampeni zitakapoanza.

Kumi na Tano, UKAWA hawana sera ambayo itamuunganisha mgombea wao na kumuuza kwa wananchi sababu UKAWA siyo chama cha siasa, na hivyo mbali na kumsafisha mgombea wao, hawatokuwa na jipya la kutoa kwa umma ukilinganisha na CCM ambao watakuwa na ilani ya kueleweka na ambayo wataiuza kwa wananchi bila shaka.

Je, wataweza kumsafisha Ndg. Lowassa ndani ya siku 64 za kampeni na watanzania wakawaelewa? Ni maswali watakayopaswa kuyatafakari na kuyajibu, pengine wakati wanayapatia majibu, muda wa kampeni utakuwa umeishakwisha na watakuwa wameishashindwa uchaguzi.

Kwa vyovyote vile malengo ya Ndg. Lowassa, kudhoofisha CCM, hayatotimia na huu utakuwa ni mwisho wake kisiasa, na hatoanguka peke yake, ataanguka na vyama vyote vya upinzani vinavyounda UKAWA. Baada ya kushindwa kwenye uchaguzi mkuu wa Oktoba 25, siyo CCM itakayokuwa inarudi kwenye meza kujipanga upya, bali ni vyama vitakavyosambaratika
kutoka UKAWA vitakavyorudi kujiuliza vilipoangukia na kuanza upya safari ya kujijenga, na hii ni kama hata kutakuwa na mabaki ya vyama hivyo.


Mwandishi wa makala hii ni Mwanasiasa, Msomi aliyebobea kwenye afya ya jamii, uchumi na uongozi, na ni Mbunge wa Jimbo la Nzega anayemaliza muda wake.

Anapatikana kwa email hkigwangalla@gmail.com , Twitter: HKigwangalla, Facebook: www.facebook.com/TeamHamisiKigwangalla
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top