Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

TINGATINGA LA MAGUFULI LAWA TISHIO KUZOA VIGOGO TAASISI 18



Kuna taarifa kuwa hofu kubwa imetanda juu ya hatma ya vigogo wa taasisi za umma takriban 18 zilizotajwa na Rais Dk. John Magufuli, kuwa zinalalamikiwa zaidi na wananchi kwa rushwa, ubadhirifu na utoaji wa huduma duni.
 
Vyanzo mbalimbali vimeiambia Nipashe kuwa hivi sasa, ikiwa ni siku chache tu baada ya Rais Dk. Magufuli kuhutubia Bunge la 11 wakati akilizindua Ijumaa iliyopita, tayari wakuu kadhaa wa taasisi hizo wameingiwa na hofu kwa kutojua hatma yao.
 
Wakati akilihutubia Bunge, Rais Dk. Magufuli alizitaja baadhi ya taasisi za umma alizosema zinalalamikiwa zaidi na wananchi kutokana na kasoro mbalimbali za kiutendaji, na kwamba serikali yake imejipanga kuhakikisha kuwa inazishughulikia mara moja.
 
Dk. Magufuli alizitaja taasisi hizo kuwa ni pamoja na Bandari, Jeshi la Polisi na Mahakama.
 
Kadhalika, aliizungumzia kero ya rushwa ambayo hushughulikiwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), ubadhirifu katika Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) na pia malalamiko kwenye eneo la ardhi ambalo ni kinara wa chanzo cha migogoro kwa wananchi.
 
“Wakuu hivi sasa hawana amani tena… wengi hawajui kuhusu hatma yao baada ya Rais Magufuli kusema wazi kuwa kuna matatizo makubwa katika utendaji wa taasisi yetu,” chanzo kimoja kiliiambia Nipashe kwa sharti  la kutotajwa jina.
 
Kadhalika, ofisa mmoja wa cheo cha juu katika halmashauri ya wilaya, aliiambia Nipashe kuwa kauli ya Dk. Magufuli kuhusiana na dhamira yake ya kumaliza kero za wananchi wanazokumbana nazo kuhusiana na ardhi zimeibua hofu kubwa kwa maofisa wa ardhi kwenye wilaya yao (jina tunalihifadhi).
 
“Kwa kweli kila mmoja miongoni mwa hawa wakubwa wetu ameingiwa hofu… wengi wamekuwa wakifanya kazi kwa mazoea na kujiingizia fedha nyingi kupitia rushwa na pia kujimilikisha maeneo kinyume cha sheria. Magufuli anatishia hatma yao,” chanzo kingine kiliongeza.
 
ALICHOSEMA MAGUFULI 
Katika hotuba yake, Magufuli alisema kuna maeneo yaliyolalamikiwa sana na wananchi wakati wa kampeni kabla ya kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu Oktoba 25 ambao alishinda kwa asilimia 58.46 ya kura halali zilizopigwa na kuingia Ikulu.
 
Alizitaja baadhi ya kero na taasisi husika kuwa ni tatizo la rushwa. Alisema tatizo hilo limelalamikiwa na wananchi karibu katika maeneo yote yanayogusa wananchi. 
 
Magufuli aliitaja pia Tamisemi, akisema ina matatizo ya upotevu wa mapato, kushindwa kukusanya kodi, ubadhirifu, matumizi mabaya ya fedha na utekelezaji wa baadhi ya miradi chini ya viwango, wizi na uzembe.
 
Katika eneo la ardhi, Magufuli alitaja kero zake kwa wananchi kuwa ni migogoro ya wakulima na wafugaji, viwanja, kuhodhi maeneo bila kuyaendeleza, mipango miji na kujenga maeneo ya wazi.
 
Kero katika Bandari ni rushwa, wizi, ubadhirifu na urasimu; kero za Maliasili na Utalii ni kuwapo kwa ujangili ambao yaonekana wazi kuwa ni lazima idara husika inashiriki, migogoro ya mipaka kati ya vijiji na hifadhi na upotevu wa mapato.
 
Eneo lingine lenye kero zinazolalamikiwa na wananchi kwa mujibu wa Dk. Magufuli ni katika huduma za afya, akisema kuwa kuna ukosefu wa dawa, hujuma kwenye vifaa vya vipimo, msongamano wa wagonjwa na tozo zisizostahili, lugha mbaya za watumishi kwa wagonjwa, uhaba wa majengo, vitendea kazi, rasilimali watu na fedha, kushindwa kukusanya mapato yanayowahusu n.k.
 
Uhamiaji ni eneo mojawapo ambalo Rais Magufuli alilitaja kuwa ni kero kubwa kwa wananchi kwa kueleza kuwa kuna wageni wengi kutoka nje ambao wapo nchini wanafanya kazi ambazo hata mzawa angezifanya.
 
Aligusia suala la kutoa ovyo hati za uraia kwa wageni pasipo kuzingatia sheria na taratibu, utoaji wa vibali vya kuishi kwa wageni na mambo mengineyo ambayo yalikuwa yanafanywa.
 
Kadhalika, Rais Magufuli wakati akihutubia Bunge, pia alielezea suala la elimu ataipa kipaumbele zaidi kwa kutekeleza sera yake ya elimu bure kuanzia shule ya msingi hadi sekondari itakayoanza kutolewa mwakani.
 
Alieleza kuwa utoaji wa elimu bure ambayo haitakuwa na michango yoyote kwa wanafunzi.
 
“Ninaposema elimu bure, ninamaanisha elimu bure kweli kweli, sitasikia masuala ya michango, tena walimu watakaotoza michango ya ajabu ajabu watakiona,” alieleza Rais Magufuli.
 
Pia Rais Magufuli alielezea kuboresha  vifaa vya kujifunzia, kutatua matatizo ya walimu, kuboresha mazingira ya kusomea ikiwa ni pamoja na majengo, Madawati, Ukosefu wa nyumba za walimu, n.k.
 
Polisi ni sehemu mojawapo ambayo Rais Magufuli aliielezea kwa mapana zaidi kwa kueleza uovu waliokuwa wanautenda jeshi la polisi kwa kuwabambikizia kesi raia wasiokuwa na hatia.
 
Pia aliezea kuboresha madai ya askari, ukosefu wa nyumba za askari, ukosefu wa vitendea kazi vya kisasa.
 
Vile vile Rais Mgufuli aligusia utendaji wa kikosi cha zimamoto kwa kuchelewa kufika kwenye matukio, kufika kwenye matukio bila vitendea kazi kama maji, huku akihaidi kulishughulikia suala hilo hivi karibuni.
 
Pia Rais Magufuli pia alizungumzia wafanyakazi wanaofanya kazi katika Mizani kwa kuwaelezea uzembe wanaoufanya ukiwamo wa  kucheleweshwa kwa magari yanayosafiri.
 
Vilevile katika hotuba yake, alizungumzia Mahakama kwa kusema anatambua jitihada zake katika kushughulikia  mrundikano wa kesi na kuahidi kulishughulikia suala hilo kwa haraka zaidi ikiwamo malalamiko mengi juu ya ucheleweshaji wa kesi. 
 
Eneo lingine ni madini akisema taifa kutokufaidika na rasilimali hiyo huku wageni wakifaidika kwa kiwango kikubwa.
 
Masuala ya vilio vya wachimbaji wadogo wadogo kutengewa maeneo ya uchimbaji na kupatiwa mikopo, kutolipa kodi stahiki, usumbufu kulipa fidia, pia alielezea kuanza nayo kwa haraka.
 
Aidha, Rais Magufuli alizungumzia Idara ya Kilimo na Mifugo  kwa kusema uhaba wa pembejeo za mifugo na kilimo, tatizo la masoko, kukopwa mazao ya wakulima, ukosefu wa wataalam wa ugani, upungufu wa maghala, mabwawa, malambo, majosho, n.k.
 
Katika hotuba hiyo, Pia Rais Magufuli alielezea sekta ya uvuvi kwa kutaja changamoto zinazowakabili wavuvi ikiwamo vifaa duni na masoko, uvuvi haramu, uwekezaji mdogo katika sekta ya uvuvi hususan viwanda vya mazao ya uvuvi hasa katika ukanda wetu wa bahari.
 
Suala la reli, Rais Magufuli alieleza kuwa reli ya kati inahitaji kufanyiwa maboresho zaidi kwa kujenga reli nyingine ya Standard Guarge kutoka  mkoani Dar es Salaam hadi Kigoma.
 
Alieleza kuwa uchakavu wa miundombinu ya nchi, kutokuwapo kwa usafiri wa uhakika wa reli, upungufu wa bandari kavu, mizigo mingi kusafirishwa kwa barabara ni mojawapo ya matatizo yaliyomo katika sekta ya reli na yanahitaji kufanyiwa marekebisho ya haraka.
 
Rais Magufuli alizungumzia Shirika la Ndege la Taifa (ATCL) kwa kueleza kuwa shirika hilo linawafanya kazi zaidi ya 200 wanaolipwa mishahara, lakini wana ndege moja tu.
 
 Rais Magufuli pia alielezea makundi maalum kama wazee, walemavu, wanawake na watoto wanavyonyimwa haki zao.
 
Vilevile Rais Magufuli aligusia kundi la wafanyakazi kama vile wanamichezo kwa kuelezea matatizo yao ikiwamo makato ya kodi kwa wafanyakazi yakiwa makubwa.
 
“Kero hizi tutazishughulikia kwa nguvu zetu zote. Wizara, ofisi na taasisi husika zijipange ipasavyo kutatua kero hizi. Nimetaja baadhi ya kero hizi ili nanyi Waheshimiwa Wabunge mzitambue na mshirikiane na serikali na wadau wengine tuzitatue haraka,” alieleza Rais Magufuli.
 
MAONI YA WACHAMBUZI
Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Iringa (UoI), Essau Ntabindi, alisema  Rais Magufuli aliongea mambo ambayo aliyapata kutoka kwa wananchi wakati akifanya kampeni za urais hivyo vilikuwa ni vitu vyenye uhalisia.
 
Aliema Rais Magufuli alichokisema ni sahihi na wala siyo kupoteza morali kwa maofisa aliowagusa kwa kuzitaja idara zao akiwa Bungeni.
 
Kadhalika, alisema  Rais Magufuli alikuwa anawakumbusha maofisa hao na watendaji wengine wa serikali wafanye kazi na siyo kupiga porojo ambazo hazina faida katika kuinua uchumi wa nchi.
 
“Rais Magufuli alichokuwa anakisema pale Bungeni alikuwa sahihi na alikuwa anawakumbusha viongozi waliopo ofisini waendane na kauli mbiu yake ya hapa kazi tu,” anasema Ntabindi.
 
Naye Mhadhiri kutoka Chuo Kikuu Huria (Out) Idara ya Siasa na Utawala, Hamad Salim, anasema Rais Magufuli ni jukumu lake kuongelea masuala yanayogusa  taifa, na Bungeni ni sehemu mojawapo ya kuongea masuala hayo.
 
Alisema kuzitaja taasisi hizo siyo kwamba alikuwa anaziumbua au kuziaibisha, bali alikuwa anawaeleza ukweli Watanzania wafahamu uozo uliokuwa unafanywa na baadhi ya viongozi.
 
Alisema hotuba yake ilikuwa inazungumzia mwelekeo wa serikali yake itakavyofanya kazi kwa miaka mitano ijayo, hivyo ilikuwa ni lazima ataje mikakati yake.
 
“Rais Magufuli hakutaka kutumia lugha ya falsafa ambayo ingewafanya Watanzania wasimuelewe anazungumza nini na atafanya nini, aliamua kutumia lugha nyepesi ili kila mtu amuelewe,” alisema Salim.
 
Alisema Rais Magufuli alikuwa anawakumbusha viongozi atakaowateua kuwa watende kazi kwa mujibu wa sheria na kanuni na siyo kwa mazoea kama walivyokuwa wanafanya kwa viongozi wakubwa waliokwisha tangulia.
 
Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Taasisi ya Utafiti na Kuondoa Umaskini (Repoa), Profesa Samwel Wangwe, alisema Rais Magufuli alikuwa anazikumbusha taasisi hizo zifanye kazi sawasawa na kuwaonyesha Watanzania namna viongozi waliotangulia walivyokuwa wanafuja mali.
 
Alisema Jeshi la Polisi na Wizara ya Maji ni idara zinazofahamika kuwa zina changamoto kubwa katika utendaji wa kazi.
 
CHANZO: NIPASHE
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top