Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

BUNGE 'VURUGU MECHI'


KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC), inatarajiwa kukutana mjini Dodoma leo na kutoa maazimio mazito juu ya Kampuni ya Lugumi Enterprises Ltd.
Wakati hayo yakitarajiwa kujiri, baadhi ya wajumbe wa kamati hiyo wakilidokezea gazeti hili kuwa wanachotaka wao ni mkataba na si kitu kingine chochote.

Makamu Mwenyekiti wa PAC, Aeshi Hilary, hakutaka kuzungumzia suala hilo kwa undani badala yake akasema: “Kamati itakaa kesho (leo) itoe itoke na kauli moja. Lakini jiulize unaweza kusahihisa majibu bila kuona maswali?”

Tangu PAC kuibua suala la mkataba huo wa mradi wa kufunga vifaa vya utambuzi wa alama za vidole kwenye vituo vya polisi nchini, kumekuwa na vuta nikuvute kati ya mhimili huo na chombo hicho cha dola.

Utata huo uliongezeka zaidi hivi karibuni, baada ya ofisi ya Katibu wa Bunge kusema kilichoombwa na PAC ni taarifa ya utekelezaji wa mradi huo na si mkataba.

Akizungumza na Nipashe jana, Aeshi alisema: “Mimi huwa sitaki kuongea mambo nje ya kamati. Pia hili suala tulishaandikia ofisi ya Bunge ili watoe maelekezo na leo (jana) ilikuwa mwisho. Wewe kuwa mvumilivu, kesho (leo) tutakutana kamati nzima na tutatoka na msimamo mmoja.” 

Alipoulizwa kama walichotaka ofisi ya Katibu wa Bunge iagize polisi ikiwasilishe bungeni ni mkataba ulioingiwa kati ya serikali na kampuni hiyo ya Lugumi au taarifa ya utekelezaji, Aeshi alisema: “Nimeshakwambia kila kitu tutaweka wazi Jumanne (leo), lakini wewe kwa akili ya kawaida utasahihisha vipi majibu bila kujua maswali yalikuwaje?”

Kauli hiyo ya Aeshi inaweza kutafsiriwa kuwa kamati hiyo inaweza kuigeuka ofisi ya Katibu wa Bunge, ambayo hivi karibuni ilisema kilichoombwa ni taarifa ya utekelezaji wa mkataba huo na si mkataba kama ambavyo imekuwa ikiripotiwa.

Gazeti hili lilipomtafuta Naibu Katibu wa Bunge, John Joel, ili kujua kama taarifa ya utekelezaji wa mkataba huo imewasililishwa ofisini kwake, alisema alikuwa hajaipata.

“Siku bado haijaisha, lakini yawezekana labda imepelekwa kwenye ofisi ya Katibu, kwangu mimi bado sijaiona ingawa bado mimi nipo ofisini mpaka sasa hivi,” alisema Joel alipotafutwa jana saa tisa alasiri.

Taarifa iliyotolewa hivi karibuni na Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano cha Bunge, ilisema PAC haijawahi kuliandikia Jeshi la Polisi kutaka kupewa mkataba kati yake na serikali juu ya kufungwa kwa vifaa hivyo.

Taarifa hiyo ilinukuu kumbukumbu rasmi za bunge (hansard) ya mkutano wa PAC ikisema: “Kamati inamuagiza Ofisa Masuhuli kuwasilisha maelezo ya kina kuhusu utekelezaji wa mkataba baina ya Jeshi la Polisi na Kampuni ya Lugumi Enterprises kuhusu mradi wa AFIS. Maelezo hayo yawasilishwe Ofisi ya Katibu wa Bunge kabla ya Jumatatu tarehe 11 Aprili, 2016”.

Taarifa hiyo iliongeza kuwa katika agizo hilo PAC haikuwa imeandika kwa maandishi kuhusu agizo lake hilo hadi Aprili 12, mwaka huu, ilipomweleza Katibu wa Bunge kuwasilisha agizo hilo kwa maandishi ili kupata kinga chini ya Sheria ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge. Barua hiyo iliandikwa na kuwasilishwa kwa Ofisa Masuhuli ili kupatiwa maelezo hayo kabla ya jana.

Hivi karibuni gazeti hili lilizungumza na baadhi ya wabunge wa CCM na wale wa upinzani walio kwenye kamati hiyo, ambao walidokeza kuwa kinachofanya jambo hilo lionekane kuuzidi nguvu mhimili huo ni kitendo cha PAC kukosa mwenyekiti ambaye kikanuni anatoka upinzani.

“Kungekuwa na mwenyekiti ingesaidia sana. Sasa hivi huku mara kuwe na shinikizo la viongozi wa chama, sijui serikali, kwa hiyo kidogo inakuwa shida,” alisema mmoja wa wabunge.

Upinzani umesusia kamati ya PAC na ile ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), kwa kile ilichosema CCM imekuwa ikiwachangulia ni nani anatakiwa kuwa mwenyekiti wa kamati hizo.

Aprili 5, mwaka huu, Aeshi aliwaambia waandishi wa habari kuwa: “Tumewaomba (polisi) waje Aprili 11, watuletee mkataba huo tuuone kwa sababu haiwezekani tangu mwaka 2011 hadi leo kampuni hiyo iwe imefunga mashine katika vituo 14 tu wakati fedha wameshalipwa.”

Wakati mkataba huo wa Lugumi ukionekana kuhenyesha mhimili huo wa dola, Bunge la 10 lilijiwekea historia ya aina yake baada ya PAC ya wakati huo, chini ya mwenyekiti wake Zitto Kabwe, kuwaweka ndani vigogo wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), baada ya kukaidi kutoa mikataba ya gesi.

Vigogo hao ni mwenyekiti wa bodi ya shirika hilo, Michael Mwanda, na aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi Mtendaji, James Andilile.PAC ilikuwa imeomba kupatiwa mikataba 26 ya gesi kwa takriban miaka mitatu bila mafanikio.

Bunge hilo pia liliibua na kuishupalia kashfa ya uchotwaji wa zaidi ya Sh. bilioni 300 kwenye akauti ya Tegeta Escrow iliyokuwa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), hali iliyofanya mawaziri, wenyeviti wa Bunge na mwanasheria mkuu wa serikali kuachia ngazi.

CHANZO:IPP MEDIA

author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top