Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

BAJETI YA SERIKALI NA MIPANGO YA WAPINZANI



Chambi Chachage


Tunajenga nyumba moja sasa tunagombania fito za nini? Swali hilo litokanalo na msemo maarufu nchini Tanzania linaweza kutumika kuelezea ukakasi uliojitokeza kuhusu Bajeti ya Serikali. Wabunge machachari waliozuiwa kuendelea na vikao vya Bunge la Bajeti wameamua kutafuta vilinge vingine. Huko nako wapo waliozuiwa.

Wadadisi wa mambo tunaamini ni haki ya Kikatiba kwa mtu yeyote kujadili masuala yoyote yaliyo muhimu kwa Taifa. Wasiwasi wetu ni kuwa ushabiki wetu wa kisiasa kuhusu sintofahamu inayoendelea kati ya Serikali na baadhi ya wapinzani inaweza kutufanya tukose utulivu wa kuchambua ni nini hasa wanachopingana kuhusu bajeti. 

Hivyo basi, tumeamua kuchukua fursa hii kuupitia ‘Uchambuzi wa Bajeti Ya Serikali 2016/2017’ uliopangwa kutolewa kwa Umma na Kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe, katika kongamano lao lililozuiwa kufanyika Jumapili ya tarehe 12 Juni 2016. Lakini kwa kuwa tunaamini kuwa mtazamo wa kiuchumi wa Waziri wa Fedha, Dakta Philip Mpango, una ushawishi mkubwa kibajeti basi uhakiki wetu hauna budi kurejea na kulinganisha taarifa nyingine muhimu za wizara yake.

Katika uhakiki wetu, uliojikita kwenye sekta za kilimo na viwanda, hoja yetu kuu ni kwamba kuna ‘miingiliano tata’ na ‘migongano hewa’ kati ya mipango ya maendeleo ya Serikali iliyotumika kuandaa bajeti na makusudio ya uchambuzi wa wapinzani wanaojitanabahisha kama wazalendo wanaofuata ‘Ujamaa wa Kidemokrasia’.

Uchambuzi wa Kiongozi wa wazalendo hao, kwa mfano, unakubaliana na Serikali kuhusu kujenga viwanda. Tena unaipongeza “sana” bajeti yake ya sasa kwa kulenga  “kuondoa changamoto ya miundombinu kwa kiwango kikubwa sana.” Lakini unadai kwamba: “Miundombinu inaweza kujengwa lakini ikawa haina watu wa kuitumia wala bidhaa za kusafirisha kwa sababu hakuna vivutio vya kuanzisha viwanda pia.”

Pamoja na kujaribu kuihuisha misingi ya Azimio la Arusha kuhusu sekta ya Umma kupitia Azimio la Tabora, wazalendo hao hawatofautiani sana na Serikali  kuhusu nafasi nyeti/tete ya sekta binafsi. “Ikumbukwe kuwa Serikali haianzishi viwanda”, uchambuzi wao unasisitiza, “bali inajenga mazingira mazuri ya wawekezaji kuanzisha viwanda.” Hivyo, unadai kwamba bajeti hii ya Serikali “haijaweka hivyo vivutio vya kuanzisha viwanda na ime­minya uwezo wa walaji kutumia kwa kudhibiti matumizi na pia kutoza kodi nyingi zinazopunguza uwezo wa kutumia bidhaa na huduma.”

Njozi ya wazalendo hao ni kuona wananchi wengi wakiwa na ajira zenye tija. Ila wanajua “viwanda vinachangia asilimia 20 ya ajira zote rasmi nchini na kwamba theluthi mbili ya Watanzania wameajiriwa na sekta isiyo rasmi.” Hivyo, wanaona “juhudi za kuongeza uzalishaji viwandani ni muhimu sana ili kuwaondoa Watanzania wengi kutoka sekta isiyo rasmi na kuwaingiza kwenye sekta rasmi.” Ndiyo maana kiitikadi hawaoni shida kuipima Serikali kwa “kutazama hatua mbalimbali za kisera [za] kuwezesha sekta binafsi kufungua viwanda vingi zaidi nchini na kuajiri watu wengi.’

Tathmini yao inawafanya wadhani kwamba “Serikali ilipaswa kuja na Sera mahususi za kufikisha asilimia 10 au zaidi ukuaji wa uzalishaji viwandani.” Ili kufanikisha hilo wanadai “Serikali haina budi ku­kaa na wenye viwanda na kupata mwafaka wa namna bora ya kuweka sera mahususi zitazopelekea uwekezaji mkubwa wa wenye mitaji katika viwanda na kuongeza uzalishaji.” Yaani hawajaridhika na maneno haya ya Dakta Mpango: “Bajeti hii imezingatia mawazo na mapendekezo ya wadau mbali mbali wakiwemo wenye viwanda, wafanyabiashara na wengine wengi”? Wanataka ‘manahodha wa viwanda’ wawe na sauti zaidi? Mtazamo wa kiuchumi wa Kiongozi wao usiopingana dhahiri na ‘dhana ya kibepari’ ya mapinduzi ya viwanda yatokanayo na mapinduzi ya kilimo umepelekea uchambuzi wao pia udai kwamba:

“Kwa Uchumi wa Tanzania, ujenzi wa Sekta ya Viwanda hauwezi kufanikiwa bila kukua kwa sekta ya kilimo. Kilimo ndio sekta Kiongozi katika kutokomeza umasikini kwani inachangia theluthi moja ya Pato la Taifa na kuajiri theluthi mbili ya Watanzania wote. Bajeti ya kwanza ya Serikali ya Awamu ya Tano imeshindwa kufungamanisha Sekta ya Kilimo na ndoto ya maendeleo ya Viwanda. Ushahidi wa kisayansi unaotokana na Taarifa za Serikali yenyewe unaonyesha kuwa hakuna mahusiano kati ya mipango ya maendeleo ya viwanda na mipango ya maendeleo ya wananchi. (Uk. 5).

‘Dongo’ hilo ni zito hasa ukizingatia kuwa katika Hotuba yake ya Kufungua Bunge ambapo alimsifia Kiongozi huyo kwa ukomavu wa kisiasa, Rais alinena haya:

“Sura ya kwanza ya viwanda tunavyovikusudia ni vile ambavyo sehemu kubwa ya malighafi yake itatoka ndani, hususan kweye sekta za kilimo, mifugo, uvuvi, na madini – na maliasili nyingine. Viwanda vya aina hii vitatupa fursa ya kujenga mfumo wa uzalishaji ndani ya nchi uliofungamana na kushikamana. Viwanda vya aina hii vitahitaji na kutegemea malighafi toka kwa wazalishaji wa sekta nilizozitaja, na kwa kufanya hivyo wazalishaji hao watakuwa na soko la uhakika humu humu ndani ya nchi.” 

Eneo mojawapo ambalo Bajeti kuu imejaribu kuzingatia alichosema Rais ni hili lilipo katika hotuba ya Dakta Mpango:

Kutoza Ushuru wa Forodha wa asilimia 10 badala ya asilimia 0 kwenye mafuta ghafi ya kula (crude edible oil) yanayotambulika katika HS Code 1511.10.00 kwa mwaka mmoja. Hatua hii inalenga katika kuhamasisha kilimo cha mbegu za mafuta hapa nchini na kukuza viwanda vya kutengeneza mafuta ya kula. Aidha, Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji imeandaa mkakati maalum wa kuendeleza viwanda vya kuzalisha mafuta yanayotokana na mbegu zinazozalishwa hapa nchini na kutumia fursa [ya] soko kubwa lililopo katika Jumuiya ya Afrika Mashariki ambapo Tanzania inayo nafasi ya kuweza kuongeza uzalishaji wa mbegu za mafuta (Uk. 87).

Mpango wa Maendeleo Wa Miaka Mitano unapopelekea sasa kinachodaiwa kuwa ni asilimia 1 tu ya Bajeti ya Maendeleo iende kwenye kilimo, je, ni kwa sababu ‘vipanga’ waliouandaa hawaelewi muingiliano wake na viwanda? Je, ni kwa sababu huko serikalini kuna ‘vilaza’ wa uchumi wa “viwanda vya kusindika mazao ya kilimo (agroprocessing industries)” ambavyo uchambuzi wa wazalendo hao unavipigia chapuo?

Serikali ‘sikivu’ ya Rais Magufuli inajua fika inachotaka kukifanya kiuchumi hata kama kuna dalili zinazoonesha kwamba haielewi kikamilifu inakoelekea na athari zake kwa undani. Kama wadadisi tulivyowahi kugusia hapo awali kuhusu ‘Dakta Mpango na Hatma ya Kifedha, Kibajeti na Kiuchumi’, njozi yake imejikita katika ujenzi wa mkusanyiko wa viwanda vilivyojikita katika kile ambacho ‘wachumi wa kiliberali’ wanakiona ni fursa ambazo uchumi wa nchi/jamii fulani unazo kuzidi washindani wake.
 
Ukiirejea taratibu ‘Taarifa ya Hali ya Uchumi 2015 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2016/17’ aliyoiwasilisha Bungeni tarehe 8 Juni 216, kwa mfano, utakutana na mkakati wa “kuanzisha kongane za viwanda (Industrial Clusters) za kuongeza thamani ya mazao ya kilimo, mifugo.” Hilo limejikita katika dhana ya ‘Minyororo ya kuongeza Thamani (Value Chains)’. Na ndiyo maana hotuba yake ya ‘Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa Mwaka 2016/17’ inasema:

“Serikali hadi sasa imeipatia Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania mtaji wa shilingi bilioni 60. Aidha, katika hatua za awali, benki imeainisha minyororo 14 ya thamani ya mazao ya kilimo katika sekta ndogo ndogo nane itakayopewa kipaumbele katika kutoa mikopo kwa kuanzia. Sekta hizo ni za uzalishaji wa nafaka; mifugo; ufugaji wa samaki, kilimo cha matunda, maua, mbogamboga, na viungo; mazao ya viwanda hasa miwa na korosho; mbegu za uzalishaji mafuta ya kula; na mazao ya misitu hasa ufugaji wa nyuki na mazao yake… kwa mwaka 2016/17, Benki imepanga kuendelea kutoa mikopo kwa angalau minyororo 14 ya thamani (agricultural value chains) itakayofanyiwa tathmini yakinifu kama iliyoanishwa kwenye mpango kazi wa kwanza wa 2016-2020” (Uk 27 & 53).

Suala la kilimo kwenye bajeti na mipango ya Serikali linazidi kutazamwa kwa jicho la kibiashara/kiwekezaji. Ndiyo maana katika hotuba hiyo hiyo Dakta Mpango anatujulisha kwamba madhumuni makuu “ya kuanzishwa benki hii ni kusaidia upatikanaji, utoshelezi na usalama wa chakula endelevu nchini na kusaidia katika kuleta mapinduzi ya kilimo kutoka kilimo cha kujikimu kwenda kilimo cha biashara ili kuchangia kwenye ukuaji wa uchumi na kupunguza umaskini.” Picha hii inaakisi maneno haya yaliyopo katika ‘Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2016/17’:

Mradi [wa Kuboresha Mazingira ya Uwekezaji na Biashara] unalenga kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara nchini. Katika mwaka 2016/17 zimetengwa shilingi bilioni 1.227 fedha za ndani kwa ajili ya: kuendelea kutafuta fursa nafuu za biashara na masoko kwa bidhaa za kilimo na viwandani kupitia majadiliano baina ya nchi na nchi, kikanda na kimataifa” (Uk. 92).
 Usuli huo unaweza kutusaidia kuelewa ni kwa nini Dakta Mpango alisema haya Bungeni: “Bajeti hii pia inalenga kujenga mazingira mazuri ya kufanya biashara na kuwekeza ili kuvutia ushiriki wa wawekezaji wa ndani na nje katika kuendeleza viwanda na kilimo.” Hakika mpango wa Serikali ya Magufuli siyo kujenga lile Taifa la wakulima na wafanyakazi. Ni wa kujenga hili Taifa la wafanyabiashara na wawekezaji.

Viwanda vilikuwa viwe vya wafanyakazi na kilimo kiwe cha wakulima enzi hizo za Ujamaa. Ila enzi hizi za Uliberali viwanda vinatakiwa kuwa vya wawekezaji na kilimo kuwa cha wafanyabiashara. Kama hatuamini hebu tutafakari haya maneno ya Dakta Mpango wakati anawasilisha bajeti Bungeni: “Mheshimiwa Spika, azma kuu ya Serikali ni kuimarisha sekta ya kilimo, mifugo na uvuvi kwa mtazamo wa kibiashara, kukuza viwanda na kuongeza thamani ya mazao yatokanayo na sekta hii.”

Dakta Mpango anaonekana amechoshwa sana na tija ndogo na kipato kidogo katika kilimo. Sasa anatoa wito kwamba watu watumie “nguvu” na “ubunifu” wao “katika kilimo cha mazao ya thamani kubwa.” Ndiyo maana anataka “mapinduzi ya kilimo kutoka kilimo cha kijungujiko (subsistence farming) kwenda kilimo cha kibiashara.”

Je, mapinduzi hayo yanawezekana bila kuondoa idadi kubwa ya wakulima kwenye ardhi/mashamba yao ili kuwapisha wenzao wachache wanaoonekana kuwa wabunifu zaidi na wenye mtazamo wa kibiashara/kijasiriamali? Kama ni kweli kilimo kinaajiri zaidi ya asilimia 70 nchini kama Dakta Mpango anavyodai, je, lengo hasa la mipango na bajeti ya Serikali ni kuhakikisha watu wote hawa wanabakia kwenye sekta hiyo?

Cha kushangaza ni kwamba swali hili la msingi katika stadi za maendeleo ya uchumi  haliguswi au linapotezewa tu. Kwa mfano, Kiongozi wa ACT-Wazalendo anasema: “Kwa sisi wachumi tunatambua kuwa ili kupunguza umasikini wa Tanzania kwa zaidi ya nusu ilihitajika sekta ya Kilimo kukua kwa kati ya asilimia 8 na 10 kwa mwaka. Kwa ukuaji huu tulionao sasa, maana yake itachukua miaka mingi sana watanzania kuondoka kwenye dimbwi la umasikini. Baadhi ya mazao yanayotarajiwa kuzalisha malighafi za viwanda uzalishaji wake umeporomoka kwa kiwango cha kutisha.”

Rai hiyo ya Wazalendo haiiambii Serikali inawezaje kukuza sekta kwa ‘mwendokasi’ huo bila hata kuwa na mbadala kwa wakulima watakoachwa. Inachoambulia kupewa ni mapendekezo yanayolenga “kumwezesha mkulima kubakia na sehemu kubwa ya mapato yake na kuvutia wananchi wengi kujishu­ghulisha na uzalishaji katika kilimo.” 

Ombi letu wadadisi ni kujibiwa hili tu: Tanzania ya viwanda ni Tanzania ya kilimo?
 
CHANZO:UDADISI 
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top