Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

JK APIGA KITANZI WAGOMBEA URAIS

 Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi,Rais Jakaya Kikwete.
.................
*Awapa mtihani mzito Lowassa, Sitta, Membe
*Kutemwa kwa January Makamba swali gumu
*Uteuzi wa Nchimbi, Lukuvi una sababu nzito

Mwenyekiti wa Taifa wa Chama Cha Mapinduzi, (CCM) Rais Jakaya Kikwete, amewapa mtihani wanasiasa wanaoonyesha nia ya kugombea urais 2015 kwa tiketi ya chama hicho, baada ya kukamilisha kazi ya kupanga safu ya viongozi wa chama chake ambayo itaratibu na kusimamia upatikanaji wa mrithi wake.

Ukweli huo umedhihirishwa na uteuzi alioufanya wa wajumbe wa Kamati Kuu wa CCM aliowatangaza juzi usiku baada ya kupigiwa kura na wajumbe wa Halmashauri ya Kuu ya Taifa (NEC) mjini Dodoma, huku akiwaacha kando baadhi ya wanasiasa wenye majina makubwa.

Miongoni mwa wanasiasa hao ambao majina yao yamekuwa yakitajwa kuingia katika mchuano wa urais wakati huo na ambao Kikwete hakupendekeza majina yao katika orodha ya kugombea ujumbe wa Kamati Kuu ni waziri mkuu wa zamani, Edward Lowassa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe

Wengine ni Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, Waziri wa Uchukuzi, Dk. Harrison Mwakyembe na Waziri wa Ujenzi, John Magufuli ambaye alikuwa akitarajiwa kuteuliwa kuwa Mjumbe wa NEC kabla ya jina lake kupendekezwa katika mchuano wa Kamati Kuu.

Hatua ya Rais Kikwete kuwaacha baadhi ya wanasiasa hao inatajwa na baadhi ya wadadisi wa siasa za CCM walio ndani ya NEC na nje kuwa iliyokuwa ikilenga kuvunja msukumo wa nguvu za makundi ambazo zimekuwa zikikitesa chama hicho kwa muda mrefu.

Mawazo ya namna hii ndani ya chama hicho, yanatiwa chachu kwa kiwango kikubwa na kauli ambayo Rais Kikwete mwenyewe aliitoa muda mfupi baada ya kuwatangaza wajumbe wapya wa Kamati Kuu usiku huo huo wa juzi.

Taarifa za ndani ya NEC zimemkariri Kikwete akiwaasa wana CCM wenye nia ya kugombea urais kuendesha harakati zao katika misingi ambayo haitakiacha chama hicho kikiwa ni majeruhi wa kuparanganyika kwa umoja na mshikamano wake.

Kauli hiyo ya Kikwete ambayo ilitafsiriwa na baadhi ya wajumbe wa NEC kuwa iliyokuwa ikisahihisha au kuikosoa ile iliyotolewa hivi karibuni na makamu wake wa mwenyekiti, Philip Mangula kwa kiwango kikubwa ilirejesha ari ya wanasiasa na wapambe wao kuendelea na mipango yao ya urais.

Mbali ya hilo, hatua ya Kikwete kumrejesha Nchimbi ndani ya CC huku akiliacha kando jina la mwanasisa mwingine kijana, January Makamba imetajwa na wafuatiliaji wa siasa za ndani ya chama hicho kuwa iliyokuwa ikilenga kufungua ukurasa mpya wa siasa za kuelekea katika urais wa mwaka 2015.

Jina la January ambaye ni mtoto wa Katibu Mkuu wa zamani wa CCM, Yussuf Makamba limekuwa likitajwa kwa muda mrefu kuwa moja ya wanasiasa waliokuwa wakipewa nafasi kubwa ya kurejeshwa katika CC baada ya kuondoka mwishoni mwa mwaka jana kutokana na kuvunjwa kwa sekretarieti ya zamani.

January amekuwa akitajwa na baadhi ya wana CCM kwamba alikuwa akipewa nafasi kubwa ya kurejeshwa ndani ya Kamati Kuu kutokana na namna alivyoshikiri kwa kiwango kikubwa kujenga umoja na mshikamano miongoni mwa makundi ya mahasimu wa kisiasa wakati akiwa Katibu wa Idara ya Siasa na Ushirikiano wa Kimataifa.

Hata hivyo, kama ilivyo kwa Lowassa, mwanasiasa huyo kijana (January) amekuwa akitajwa kuwa katika misigano ya chini chini ya kisiasa na wanasiasa wengine kadhaa wanaotajwa kuwa karibu na rais au familia yake, kama alivyo Membe.

Kurejea kwa Nchimbi katika Kamati Kuu akiwa nje kwa vipindi viwili mfululizo kama ilivyo kwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Siasa na Uhusiano), Stephen Wassira kunatajwa kuwa mkakati binafsi wa rais kuwaweka karibu watu ambao amekuwa nao kisiasa kwa miaka mingi.

Nchimbi na Wassira ndiyo wanasiasa pekee wa kundi lililosambaratika la mtandao ambao wameendelea kuwa na mahusiano ya karibu ya kikazi na Rais Kikwete ndani ya CCM na serikalini tangu Februari mwaka 2008 wakati Lowassa alipojiuzulu uwaziri mkuu.

Ukiwaacha wanasiasa hao wawili, mwanasiasa mwingine watatu ambao ameendelea kufanya kazi kwa karibu na Kikwete ni Membe ambaye japo ameendelea kushikilia wadhifa wa Waziri wa Mambo ya Nje ya Ushirikiano wa Kimataifa kwa muda mrefu amekuwa nje ya Kamati Kuu.

Ingawa ukaribu na uaminifu binafsi wa Nchimbi kwa Rais Kikwete unaweza ukawa sifa iliyomrudisha ndani ya CC, wadadisi wa siasa wanasema historia ya mwanasiasa huyo ndani ya chama hicho tangu akiwa kiongozi wa juu wa Umoja wa Vijana wa CCM, ni sehemu ya mambo ambayo yanamfanya awe na sifa za kufikia hapo alipo leo.

Sifa kama hizo za Nchimbi zinatajwa pia kuwa miongoni mwa sababu ambazo zilisababisha Rais Kikwete alazimike kulirejesha jina la William Lukuvi ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge) katika timu ya wanasiasa wanaounda Kamati Kuu.

Tathmini ya Mtanzania Jumatano kwa wajumbe 14 waliochaguliwa kuunda Kamati Kuu inaonyesha kuwa wengi ni makada ambao hawana makundi ndani ya chama na pia wenye misimamo thabiti isiyoyumbushwa na kelele za kisiasa wala mwelekeo wa upepo wa kisiasa.

Tathmini hiyo ambayo imemuangalia mjumbe mmoja mmoja, ikianza na wajumbe saba kutoka Tanzania Bara imeonyesha kuwa mgombea urais wa CCM anaweza kuwa mtu ambaye hatarajiwi na wengi lakini kwa kutumia uzoefu wa kisiasa wa wajumbe wa Kamati Kuu, CCM kinaweza kumbeba kumnadi kwa watanzania na kuibuka na ushindi.

Jambo jingine linaloonyesha mwanzo mpya wa safari ya CCM kuelekea uchaguzi mkuu wa 2015 kikiongozwa na CC mpya ni sura za wajumbe wenye uchu wa kupambana na wanasiasa wa vyama vya upinzani ambao wamekuwa wakikisumbua chama hicho katika majukwaa ya kisiasa kwa kipindi kirefu sasa.

Wa kwanza anayetajwa kuwa na sifa ya kupambana na wapinzani ni Wassira ambaye historia yake ya kuzunguka katika vyama vya upinzani imemjengea uzoefu wa namna vyama hivyo vinavyoendesha shughuli na hivyo kuwa na uwezo wa kukabiliana na makada wake katika siasa za majukwaani.

Kwa mujibu wa upepo wa kisiasa ulivyo hivi sasa ambao umekuwa ukivuma vibaya kwa upande wa CCM, haina shaka kuwa kuteuliwa kwa Wassira ambaye ni Mbunge wa Bunda, kumetokana na kile kinachoonekana kuwa ni utiifu na uaminifu wake kwa Kikwete binafsi.

Sifa yake hiyo ya kuonekana kuwa mpambanaji dhidi ya wanasiasa wa kambi ya upinzani ndiyo ilimsaidia kupata ushindi mkubwa katika uchaguzi wa wajumbe wa NEC licha ya kukabiliwa na tishio kubwa la kupokwa nafasi yake ya ubunge kutoka kwa makada wa ndani ya chama chake.

Sifa hizo za Wassira zinafananishwa na zile za Nchimbi na Lukuvi ambao ukaribu na utiifu wao wa kikazi kwa CCM na kwa rais unawaweka katika kundi la wanasiasa wanaoonekana kuwa na sifa za ziada za kukipigania chama hicho.

Hata hivyo, baadhi ya wadadisi wamekuwa wakimuangalia Lukuvi kuwa mwanasiasa ambaye mara zote amekuwa akiangalia zaidi maslahi yake binafsi licha ya kuwa na historia inayofanana na wanasiasa wa aina ya Nchimbi ya kukulia ndani ya chama akianzia harakati zake UVCCM.

Moja ya mifano inayotajwa sana kuhusu mwanasiasa huyo, ni ule wa kuelekea mwaka 2005 wakati alipokuwa akihusishwa kuwa katika kundi lililokuwa likimuunga mkono kwa karibualiyekuwa Waziri Mkuu wa wakati huo, Frederick Sumaye kabla ya kubadilika kadri Kikwete alivyoonekana kuelekea kushinda uteuzi ndani ya CCM.

Kama ilivyo kwa wajumbe wapya wa Kamati Kuu, kuingia kwa Adam Kimbisa ambaye ni Mbunge wa Bunge wa Afrika Mashariki na Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa wa Dodoma katika CC kunahusishwa na sababu kama hizo hizo.

Kimbisa anatajwa kuwa karibu sana kisiasa na kikazi na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana ambaye katika miaka ya hivi karibuni wote walipata kuwa viongozi wa Chama cha Msalaba Mwekundu.

Ni jambo lililo wazi kuwa kuteuliwa kwake kumetokana na kutotajwa kujihusisha moja kwa moja na siasa za makundi pamoja na jina lake kuhusishwa na mgombea mmoja maarufu wa urais ambaye ameachwa nje ya Kamati Kuu.

Pengine jina jipya katika Kamati Kuu ya CCM ni la Profesa Anna Tibaijuka, Mbunge wa Muleba Kusini na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi ambaye kuteuliwa kwake kumeonekana kuwashtua wanasiasa wengi na wadadisi wa masuala ya siasa nchini.

Licha ya kuwa mgeni katika siasa za CCM, Tibaijuka anaonekana kuwa mwanasiasa mwenye nguvu hasa kutoka mikoa ya Kanda ya Ziwa na msomi mwenye fikra yakinifu na zisizofungamana na upande wowote.

Prof. Tibaijuka ambaye aghalab ameepuka sana kuwa mwanasiasa wa majukwaani, amejijengea heshima ndani ya CCM kwa kutokuwa mtu wa ndiyo mzee na mtu mwenye mawazo yanayojitegemea.

Tangu aalipoanza kushiriki moja kwa moja siasa za hapa nyumbani hajaonyesha kuwa na kundi ndani ya chama jambo ambalo haina shaka ndilo lililomvutia rais Kikwete kumuweka katika timu yake kwa imani kuwa atatoa msaada mkubwa wa chama kutoyumbishwa na siasa za makundi na hasa wakati wa kuelekea uchaguzi.

Kwa Pindi Chana, mwanamama mwingine aliyeingia katika CC mfululizo katika vipindi zaidi ya vitatu, anaonekana kuwa tofauti kidogo na Prof. Tibaijuka kutokana na msimamo wake kutofahamika bayana pamoja na kubeba taswira ya kuwa mwanamama kipenzi cha viongozi wa juu wa chama hicho.

Pindi anatajwa kuwa miongoni mwa wanasiasa wachache wanawake ambao makuzi yao ya kisiasa yamepita katika mikono ya Nchimbi wakati alipokuwa Mwenyekiti wa Taifa wa UVCCM.

Jina jingine geni katika siasa za chama hicho nap engine mtu anayeonekana kuwa tanuru jipya la fikra ndani ya Kamati Kuu ni la Meya wa Manispaa ya Ilala, Jerry Salaa anayewakilisha kundi kubwa la vijana ndani ya CCM.

Silaa licha ya kuwa mgeni katika siasa hiki ni kipindi chake cha pili kuwa mjumbe wa NEC ambaye amepata mafanikio ya kisiasa kutokana na tabia yake ya kuangalia eneo ambalo haliwezi kuathiri maslahi yake binafsi.

Siasa zake zina mkondo wa kimagharibi na wanacCCM wenzake Jijini Dar es Salaam wamempa jina la mwanasiasa mjanja kutokana na namna anavyoendesha maisha yake ya kisiasa.


author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top