Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) |
NA RAHMA SULEIMAN
Nyumba tisa zimeteketezwa kwa moto katika kisiwa cha Tumbatu Kaskazini
Unguja muda mfupi baada ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) kutangaza
ushindi wa urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mgombea wa Chama
Cha Mapinduzi (CCM), Dk. John Magufuli.
Baada ya kutangazwa kwa matokeo hayo, baadhi ya wafuasi na wanachama wa
CCM kisiwani hapo walianza kushangilia ushindi huo. Hata hivyo, wakati
wakiendelea kushangilia ushindi huo huku wakilidhihaki kundi lingine
hali iliyosababisha warushiane mawe na mwishowe kuchomeana nyumba hizo.
Akizungumza na Nipashe, mmoja wa wananchi wa kisiwa hicho, Juma Ali,
alisema kuwa wafuasi wa CCM waliokuwa wakisherehekea ushindi walikuwa
wakiwazomea wafuasi wa wanaoaminika kuwa ni wa chama kingine na kuanza
kupigana.
Alisema ugomvi huo ulizusha taharuki hadi kufikia wafuasi hao wa pande
mbili kuanza kurushiana mawe hadi kuchomeana moto nyumba zao za makaazi
yao.
“Kwa kweli hali ilikuwa mbaya katika kisiwa hiki cha Tumbatu hasa kijiji
cha Tumbatu Gomani ambacho kina wafuasi wengi wa CCM na kijiji cha
Tumbatu Chwaka ambacho kina wafuasi wengi wa chama kingine,” alisema.
Alifafanua kuwa nyumba zilizochomwa moto ni za Gomani na Chwaka.
Kamishana wa Jeshi la Polisi Zanzibar, Hamdani Omar Makame, alisema
jumla ya nyumba tisa katika kisiwa hicho zimechomwa moto na chanzo cha
ugomvi huo ni matokeo ya mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania kupitia CCM.
Alisema tayari polisi kwa kushirikiana na vikosi vya SMZ, vimeshatuliza
ghasia hizo kisiwani humo na pia wanaendelea kufanya uchunguzi ili
kubaini waliohusika na vitendo hivyo vya uvunjifu wa amani.
CHANZO: NIPASHE
Post a Comment