Vyama sita vya siasa vimemtaka Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar
(ZEC) Jecha Salum Jecha kujiuzulu kwa kukiuka katiba ya uchaguzi na
kutaka kuiingiza nchi katika machafuko.
Wajumbe wa vyama sita vinavyomtaka
Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar kujiuzulu; vyama hivyo ni
Demokrasia Makini, SAU, CHAUMA, NRA, Jahazi Asilia, na DP wakizungumza
na waandishi wa habari jana katika ukumbi wa hoteli ya Grand Palace
iliyopo Malindi Mji Mkongwe wa Zanzibar
Vyama hivyo ni pamoja na Demokrasia Makini, SAU, CHAUMA, NRA, Jahazi
Asilia, na DP ambao wamezungumza na waandishi wa habari jana katika
ukumbi wa hoteli ya Grand Palace iliyopo Malindi Mji Mkongwe wa
Zanzibar.
Akizungumza na katika mkutano huo Mgombea wa Urais wa Zanzibar kwa
tiketi ya CHAUMA, Abdallah Kombo Khamis alisema wao kama wana siasa na
ni wazanzibari hawapo tayari kuona demokrasia inavizwa wakakaa bila ya
kutoa tamko lolote.
“Kwa vyovyote vile iwavyo, hatutakubali uvizwaji wa demokrasia wa aina
yoyote, kwamba kwa kuwa matokeo tulioyoyataja kutokwenda sambamba na
matarajio ya CCM, mwenyekiti wa ZEC amekubali kutumika kukinusuru chama
cha CCM ambacho yeye ni mwanachama aliyewahi kuwania ubunge kupitia
chama hicho” alisema Mgombea huyo.
Wamesema sababu alizozotoa Mwneyekiti wa tume ambazo zimepelekea kufutwa
kwa uchaguzi huo zilikuwemo ndani ya uwezo wa tume yake kuzifanyia
marekebisho hata kabla hazijaathiri zoezi la uchaguzi wote katika hatua
ya mwisho.
Alisema Mwenyekiti huyo ameshindwa kuchukua hatua mwafaka muda uliofaa
katika mambo yaliokuwa ndani ya mamlaka yake unatia mashaka juu ya
ukweli wa hoja zake.
“Zaidi ya yote ametoa maelezo jumla jumla hakuainisha ni eneo lipi hasa
lililohusika ili na wadau wengine wakajiridhisha na maelezo yake, hili
linatia shaka” alisema.
Mgombea huyo ambaye aliambatana na wagombea wenzake wa vyama vilivyounda
umoja huo kwa ajili ya kutoa yamko lao la kupingana na Mwenyekiti wa
Tume mbali ya kulaani tukio la Mwneyekiti lakini pia wanaona uamuzi
wake huo utaathiri matokeo ya uchaguzi wa Muungano.
“Huku demokrasia ikipindwa katika kiwango hicho, mitaani wananchi
wamekuwa wakipata mateso ya kupigwa na kuumizwa vibaya pasipo na sababu
kunakofanywa na vikosi vya ulinzi, vitendo hivi ni uvunjifu mkubwa wa
haki za binaadam na haki za watu hivyo tunaiomba serikali ichukua hatua
kusitisha mara moja mateso kwa raia zake” aliongea kwa uchungu Khamis.
Walisema khofu yao uchaguzi utakaofutwa na kurejeshwa tena hali ya
wananchi itakuwa tete zaidi nap engine kupelekea mauaji kama yaliowahi
kutokea katika chaguzi zilizopita.
“Sisi tukiwa miongoni mwa wagombea urais wa Zanzibar hatujaridhika na
maamuzi pweke ya Jecha na hivyo tunaitaka ZEC ikae katika kikao halali
cha tume iyoe tamko ya kufuta kauli ya Mwenyekiti wao na kueleza
umaliziaji wa hatua iliyobaki ya majumuisho na matangazo ya uchaguzi wa
nafasi ya urais wa Zanzibar ili aliyeshinda apewe haki yake katika njia
ya kidemokrasia ili nchi yetu idumu hali ya Amani na utulivu” aliongeza.
Mgombea huyo alisema suala la uchaguzi lina gharama kubwa ambapo
Zanzibar imetumia shilingi bilioni 7.5 kwa ajili ya uchaguzi hivyo
kuijeresha tena Zanzibar ndani ya uchaguzi ni kuingia tena kwenye
gharama kuliangamiza taifa.
“Tunaziomba jumuiya za kimataifa na taasisi nyengine kusaidia kulimaliza
tatizo la uchaguzi huu kwa kuhakikisha kuwa aliyeshinda anapewa haki
yake ili Amani iendelee kudumu Zanzibar” alisema Khamis.
Aidha mgombea huo aliitaka tume ya uchaguzi Zanzibar kuendelea na
mchakato na kutangaza matokeo ya uchaguzi huo kwa mujibu wa fomu
zilizokusanywa katika vituo vya kupigia kura.
Pia mgombea huyo aliiomba tume ya kimataifa na mashirika ya maendeleo
kuingilia kati suala hilo kwa kutumia waangalizi wa jumuiya mbali mbali
zilizoshiriki katika uchaguzi huu ambapo wao wanaweza kupata taarifa
kamili na za uhakika.
Katika kutoa wito wamewataka wazanzibari wote bila ya kujali itikadi za
kisiasa kuwa tayari kupigania haki zao na kuhakikisha demokrasia
inachukua nafasi yake kwa lengo la kuimarisha na kukuza ustawi wa
Zanzibar na watu wake.
Chanzo: zanzibariyetu.wordpress.com
Post a Comment