Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

UKAWA WAKOMBA HALMASHAURI 19


Vyama vinavyounda UKAWA.
 
Muungano wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) unaelekea kuimarika zaidi katika ngazi ya udiwani baada ya kujihakikishia kuongoza halmashauri takriban 19 hadi kufikia jana.
 
 
Hadi kufikia jana, tayari muungano huo unaoundwa na vyama vya NCCR-Mageuzi, NLD,  Chama cha Wananchi (CUF) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ulishapata madiwani wengi na hivyo kujihakikishia utawala katika halmashauri za wilaya, miji, manispaa na jiji katika mikoa ya Kilimanjaro, Tanga, Mtwara, Mbeya, Lindi, Kagera na Arusha.
 
 
MTWARA 
Kwa mujibu wa matokeo yaliyotangazwa hadi sasa, CUF na Chadema tayari zimejihakikishia utawala katika Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Mjini baada ya kutwaa jumla ya kata 11 dhidi ya 7 za Chama Cha Mapinduzi (CCM). Kati ya hizo, CUF imeshinda kata 8 na Chadema kata 3.   Awali, CCM ndiyo waliokuwa wakiongoza halmashauri hiyo. 
 
 
Kadhalika, CUF pia imetwaa utawala wa Halmashauri ya Wilaya ya Tandahimba baada ya kushinda katika kata 20 kati ya 31 zilizopo, Chadema wakipata kata moja na nyingine 10 zikiangukia CCM. Aidha, CUF wameshinda pia ubunge katika majimbo hayo mawili ya Mtwara Mjini na Tandahimba. 
 
 
ARUSHA
Katika mkoa wa Arusha, matokeo yanaonyesha kuwa hadi sasa Chadema wanaongoza katika halmashauri za wilaya za Monduli, Jiji la Arusha, Arumeru  Mashariki na Arumeru Magharibi.
 
 
Halmashauri ya Jiji la Arusha, Chadema imeshashinda katika kata 24 na CCM kuambulia kata moja.
 
 
Arumeru Mashariki, Chadema imepata kata 25 na CCM kata sita, Arumeru Magharibi Chadema kata 21 na CCM sita huku Monduli Chadema ikipata kata 15 na CCM kata 5. Na kote huko, Chadema imetwaa pia viti vya ubunge.
 
 
TANGA
Licha ya kutwaa ubunge wa Jiji la Tanga, CUF pia imetwaa utawala wa Jiji hilo baada ya kushinda katika kata 11 dhidi ya CCM iliyoambulia kata 5. 
 
 
MBEYA 
Katika mkoa wa Mbeya, tayari Chadema ina  uhakika wa kuongoza Halmashauri ya Jiji la Mbeya na pia Halmashauri ya Mji wa Tunduma wilayani Momba.
 
 
Matokeo yanaonyesha kuwa katika Halmashauri ya Jiji la Mbeya lenye kata 36, Chadema imepata kata 26 huku CCM ikipata kata tisa na kata moja uchaguzi ukiahirishwa kufuatia kifo cha mgombea wa CCM wakati wa kampeni.
 
 
Kabla ya uchaguzi wa mwaka huu, Halmashauri ya Jiji la Mbeya ilikuwa ikiongozwa na CCM iliyokuwa na madiwani 22 huku Chadema ikiwa na madiwani 12 na wengine wawili wakiwa wa NCCR Mageuzi.
 
 
Katika Jimbo la Tunduma, Chadema imeshinda kata 14 huku CCM ikiambulia kata moja kati ya 15 zilizopo.
 
 
KAGERA
Chadema na washirika wake Ukawa wamefanikiwa kutwaa Manispaa ya Bukoba baada ya Chadema kushinda katika kata 7, NCCR moja na CUF kata moja huku CCM ikipata kata 5
 
 
 
IRINGA
Katika Halmashauri ya Manispaa ya Iringa, Chadema ilishapata kata 18 hadi kufikia jana mchana na CCM kupata kata 4, hivyo kujihakikishia utawala katika halmashauri hiyo.
 
KILIMANJARO 
Kwa mujibu wa matokeo hayo, Chadema iliyovuna wabunge sita na NCCR-Mageuzi yenye mbunge moja katika mkoa wa Kilimanjaro, sasa zitaunda Halmashauri tano za Wilaya ambazo ni Moshi Mjini, Hai, Siha, Rombo, Moshi Vijijini na Vunjo; wakati CCM ikiwa imeambulia Halmashauri mbili za Mwanga na Same.
 
Majimbo hayo na idadi ya Kata ambazo Chadema na NCCR-Mageuzi zitaunda Halmashauri zake ni Moshi Mjini, Chadema imeshinda Kata 19 kati ya 21 na CCM imepata Kata mbili za Bondeni na Kilimanjaro, wakati jimbo la Hai, Chadema imeshinda Kata 16 kati ya 17, ambapo Kata moja ya Bomang’ombe ndio pekee haijafanya uchaguzi kutokana na mgombea wa CCM kufariki dunia wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu.
 
Aidha, Chadema iliyoshinda Kata 27 kati ya 28 za Wilaya ya Rombo,ndiyo itakayounda Halmashauri ya Wilaya hiyo, huku NCCR-Mageuzi iliyoshinda Kata nane, kati ya 16 na Chadema iliyoshinda viti 15 vya udiwani katika jimbo la Moshi Vijijini, sasa zitaunda Halmashauri moja ya Wilaya ya Moshi. Katika jimbo la Moshi Vijijini CCM imeshinda Kata moja.
 
LINDI
Katika mkoa wa Lindi, CUF imefanikiwa kupata uongozi wa halmshauri za wilaya za Kilwa ambako imetwaa kata 8 kati ya 10 za Kilwa Kusini na pia halmashauri ya Wilaya ya Liwale ambako imepata kata 14 huku CCM ikipata kata 6. 
 
MARA 
Chadema imetwaa kata 4, sawa na CCM, huku ikitwaa utawala Tarime Vijijini baada ya kushinda katika kata 16 dhidi ya 10 za CCM.
 
*Imeandikwa na Thobias Mwanakatwe, Godfrey Mushi, Juma Mohamed, Emmanuel Lengwa na Daniel Mkate
 
CHANZO: NIPASHE
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top