Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

KAFULILA:BILA UPINZANI IMARA CCM ISINGEMPITISHA DK.MAGUFULI 2015


David Kafulila alipokuwa bungeni.
...........................
Tangu ulipoanzishwa mfumo wa vyama vingi hapa nchini mwaka 1992, kumekuwa na mambo mengi hususani katika siasa za Tanzania.
 
Miongoni mwa mambo hayo ni pamoja na vyama vya upinzani kuweka mbele mapambano dhidi ya ufisadi ndani ya serikali kuanzia awamu ya pili uongozi wa nchi chini ya Rais mstaafu Ali Hassan Mwinyi.
 
Katika kipindi hicho chote wapinzani waliendelea na mapambano hayo na kuyafanya ajenda ya kudumu kwa serikali ya awamu ya tatu ya Rais mstaafu Benjamin Mkapa na awamu ya nne ya Rais mstaafu Jakaya Kikwete.
 
Ni mapambano mazuri ambayo yalisaidia kuikumbusha serikali hizo dhidi ya ufisadi na matumizi mabaya ya fedha za umma hapa nchini.
 
Sasa tupo katika uongozi wa awamu ya tano ya Rais John Magufuli ambaye amekuja na kauli mbiu ya 'kutumbua majipu' ikiwa ni namna ya kipekee ya kupambana na ufisadi.
 
Anafanya hivyo baada ya kukiri kwamba alikuta uozo mkubwa ndani ya serikali na kwamba ni kazi kubwa kutumbua majipu na anahitaji Watanzania wamuombee kwa Mungu.
 
Ametangaza kujitoa sadaka ili kuikomboa nchi hii dhidi ya vitendo viovu vya ufisadi.
Moja ya wapinzani ambao wamekuwa mstari wa mbele kupambana na ufisadi hadharani ni mwanasiasa kijana, David Kafulila.
 
Kafulila ambaye alikuwa Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR-Mageuzi) kati ya 2010 hadi 2015, anasema juhudi za Rais Magufuli zinapaswa kuungwa mkono na watu wote.
 
Mwanasiasa huyo akizungumza katika mahojiono maalum anasema, wazalendo wote wanapaswa kumuunga mkono kwa sababu mapambano haya yanaleta nidhamu ya utendaji serikalini.
 
Anasema kwa muda mrefu serikali zote zilikuwa katika hali mbaya katika nidhamu ya utendaji ambao ulitokana na kuwapo mfumo mbovu.
 
 Kikubwa anachokisema Kafulila ni kujenga mfumo imara ambao utasimamia nidhamu ya matumizi ya fedha za umma hata kama Rais Magufuli atamaliza kipindi chake na kuondoka.
 
"Rais anatakiwa ajenge mfumo unaotisha ili hata  asipokuwapo kwa sababu yoyote ile nchi ibakie na nidhamu ya utendaji kazi na hofu ya ufisadi.
 
Kafulila anasema panapokuwa  na mfumo mzuri wa utendaji  kazi hata kiongozi mwingine anapokuja lazima atabanwa ili afanye hiki kinachofanywa na Rais Magufuli kwa sasa.
 
Hata hivyo, Kafulila anasema  Rais Magufuli anapaswa kutambua kuwa hofu ya sasa ni ya muda mfupi kwani anaogopwa yeye na sio mfumo.
 
Anasema kuwa njia pekee ya kuhakikisha hilo linatendeka ni pamoja na kuwapo kwa katiba mpya itakayojenga mifumo thabiti katika utendaji kazi.
 
“Zaidi anapaswa kuruhusu demokrasia hasa ya Bunge ili limsaidie kutumbua majipu kwani peke yake hawezi,” anasema Kafulila.
 
SAKATA LA UFISADI  WA KASHFA YA ESCROW 
Kafulila ambaye alijinyakulia umaarufu bungeni baada ya kuibua tuhuma nzito akiwahusisha mawaziri wawili kuhusika katika uchotwaji wa fedha zaidi ya bilioni 200 katika akaunti ya Tegeta Escrow iliyokuwa inamilikiwa kwa pamoja kati ya Shirika la Umeme (Tanesco) na kampuni ya kufua umeme ya  IPTL.
 
Kuhusu sakata la Escrow anasema anachokiona kwa Rais Magufuli bado anaivutia pumzi.
 
”Simuoni  akiigusa ingawa sioni akiicha iendelee,” anasema Kafulila.
Anasema anachokifanya kwa sasa ni kuhangaika na kesi yake ya kupinga ushindi alioupata mgombea wa CCM katika jimbo la Kigoma Kusini mwaka jana.
 
Anakiri kwamba alikuwa mwiba mkali kwa serikali ya Kikwete na kwamba bado anawaza kuendelea na juhudi hizo za kupinga ufisadi hadharani.
 
Mwanasiasa huyo kijana anasema  kinachofanywa na Rais Magufuli hususani kuwafukuza wezi wa fedha za umma kwa sasa mtu anaweza kudhani Ikulu haikuwa na Rais miaka mitano iliyopita.
 
Akizungumzia uchaguzi wa mwaka jana, Kafulila anasema ulikuwa na ushindani mkali ambao haujawahi kutokeo katika chaguzi zote zilizowahi kufanyika nchini.
Kafulila anasema ushindani huo ulikuwa ni jaribu  kwa mfumo kuona kama upo imara  kusimamia uchaguzi wa ushindani kuanzia ngazi ya Udiwani, Ubunge na Urais.
 
“Jambo moja kubwa nililoliona ni udhaifu wa mfumo hasa kuanzia kwa Tume ya Taifa ya  Uchaguzi (NEC),  kunahitajika mabadiliko ya kikatiba kwa sababu kwa kiasi kikubwa hii ni Tume ya serikali na siyo ya umma,” anasema Kafulila.
 
Anasema mfumo unaifanya iwe hivyo kwamba wasimamizi wote wa uchaguzi kwenye majimbo ambako kunaamua nani awe mbunge na diwani na hata Rais ni watendaji kata na wakurugenzi ambao hakika ni sehemu ya Tamisemi ambao ni serikali.
 
“Sheria inasema wasimamizi hao wa uchaguzi ndiyo wenye kauli za mwisho katika kumtangaza mshindi, na baada ya hapo labda mtu aende mahakamani,"  anasema Kafulila.
 
Anatoa mfano kwamba kama NEC ingekuwa kwa ajili ya wananchi ingeweza kutatua migogoro mingi ya uchaguzi na kuimaliza na isingeenda mahakamani.
 
Kafulila anatoa mfano kuwa kuna wagombea wanalalamika kwamba alitangazwa mshindi ambaye hakushinda  na fomu za matokeo zinaonyesha hivyo na kwamba jambo kama hilo lingepaswa  kuishia kwa Tume kwa mfumo wa rufaa na kurekebisha kasoro kama hizo.
 
Anasema masuala ya kufikishana mahakamani yangebaki yale ambayo yanayohitaji sayansi kubwa kutambua haki ni ya nani.
 
Kafulila alishauri kuwa serikali iondolewe kwenye mfumo wa Tume ili iajiri watu wake watakaowajibika kwa yenyewe na siyo kuwa na watumishi wanaowajibika kwa serikali.
 
NAFASI YA VYAMA VYA UPINZANI KWA SASA.
Akizungumzia nafasi ya upinzani kwa sasa anasema kuwa bado upinzani una nafasi kubwa hasa ukizingatia kuwa Rais Magufuli ameeleza yupo tayari kujiuzulu urais kama akishindwa kupambana na ufisadi.
 
Anasema hoja ya ufisadi ni ya upinzani kwa miaka mingi, hivyo nafasi ya upinzani bado ipo hususani kumuelekeza Rais yalipo majipu.
 
“Jambo la msingi ni Rais asimamie kwa dhati kauli yake kuwa yeye ni rais wa wote  bila kujali itikadi za  siasa,  dini,  rangi wala ukanda na kikabila kwani itamsaidia kujenga uwajibikaji,” anasema.
 
Aliongezea kuwa “Rais aone upinzani ndiyo ustawi wa taifa lake, kwani hata yeye,  asingepewa nafasi ya kugombea kupitia CCM kama CCM isingehofu upinzani. 
 
Alionekana kama mtu anayeweza kukabili wimbi la mabadiliko ili kuinusuru CCM ndio sababu akapewa siyo kwamba wenye CCM walimpenda,” anasema Kafulila.
 
Kuhusu serikali ya sasa ya  CCM  kama imekidhi kiu ya upinzani kwa kile walichokuwa wanakililia kwa miaka mingi, Kafulila anasema kuwa bado ni mapema kusema haya.
 
“Bado hata mwaka haujamalizika siasa zinaendelea tena kwa kasi, hata serikali ifanye nini upinzani utazidi kukua kwani unaweza kubadili mbinu ndiyo maana nchi zenye maisha bora duniani kama Finland bado kuna upinzani mkali,” anasema Kafulila.
 
MAISHA YAKE KISIASA BAADA YA KUSHINDWA UBUNGE
Kafulila anasema yeye bado ni mwanachama halali wa NCCR-Mageuzi na pia ni Katibu mwenezi Taifa.
 
“Sijui habari za kuhama NCCR msingi wake ni nini,  kwa sasa nipo mahakamani nashughulika na kesi ya ubunge wangu hilo ndilo jambo kubwa naweza kusema hayo mengine sina nafasi kuyazungumzia,” anasema Kafulila.
CHANZO: NIPASHE

author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top