Featured

    Featured Posts

    Social Icons

Loading...

Maskini Baba Diamond Platnumz, Azidiwa Ghafla

Maskini wee! Baba wa staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’, Abdul Juma ‘Baba D’ anaumwa sana! Ndivyo Risasi Mchanganyiko linavyoweza kukuhabarisha baada ya mzazi huyo kuzidiwa ghafla na kukimbizwa hospitalini kutibiwa kwa msaada kutokana na kukosa fedha, twende hatua kwa hatua.

NI JUMAPILI ILIYOPITA
Tukio hilo la kusikitisha la baba mzazi wa msanii ambaye anatajwa kuwa na ukwasi wa kutosha Bongo, lilijiri Jumapili iliyopita ambapo kwa msaada wa Dk. Fadhili Emily wa Kituo cha Tiba cha Fadhaget Sanitarium kilichopo Mbezi Beach-Africana, Dar, baba Diamond alifikishwa kutoka nyumbani kwake Magomeni-Kagera hadi hospitalini hapo na kupatiwa matibabu.

CHANZO CHAVUJISHA
Awali, Risasi Mchanganyiko lilipokea taarifa za mzee Abdul kuzidiwa nyumbani kwake lakini ikaelezwa kwamba, hakuwa na msaada wowote hadi majirani walipopata mawasiliano ya daktari huyo na kumuomba amsaidie.

“Jamani baba D (baba Diamond) yupo hoi hapa nyumbani kwake Magomeni. Miguu inamuuma, anashindwa kutembea na ukizingatia hana kipato, anashindwa pia kwenda hospitali. Na bahati mbaya kwa muda mrefu hata majirani wamekuwa wakimsaidia lakini bado hajapata tiba sahihi.”

AUNGANISHWA NA DK. FADHILI
“Leo (Jumapili) kuna jirani yake mmoja hapa ndiyo amepata wazo baada ya kusoma Gazeti la Risasi Jumamosi (ndugu na hili), amepata namba za Dk. Fadhili katika makala anazoandika gazetini kuhusu afya. Akampigia na kumuomba msaada na bahati nzuri dokta huyo ameguswa na tatizo la mzazi huyu, amemtumia nauli ya teksi ili akimbizwe  hospitalini kwake, sasa hivi ndiyo wanaelekea huko,” kilisema chanzo hicho.

MAKACHERO WAUNGA TELA
Licha ya kuwa muda huo ulikuwa umeyoyoma (saa 1 usiku), makachero wetu waliingia mzigoni kuelekea moja kwa moja Mbezi kwenye hospitali hiyo na kumkuta baba D akiwa anaingia mapokezi katika kliniki hiyo.


ASAIDIWA NA WAHUDUMU
Akiwa mapokezi, makachero wetu walimshuhudia baba Diamond akisaidiwa na vijana wawili ambao ni wahudumu wa hospitali hiyo, walimkalisha kwenye kochi kisha wakaanza kumpa huduma ya dharura ambapo walimpima presha na kumuita Dk. Fadhili atazame miguu yake.

KUHUSU MIGUU
Dk. Fadhili alipofika, alimvua soksi baba huyo na kuikagua vizuri miguu hiyo kabla ya kuingia naye ndani katika chumba maalumu cha vipimo na matibabu.

VIPIMO VINGINE
Ilibainika kuwa, miongoni mwa vipimo alivyopimwa baba D ni pamoja na kile cha Quantum Magnetic Analyzer ‘QMA’ ambacho kazi yake ni kutambua magonjwa mbalimbali ndani ya mwili wa binadamu. Hata hivyo, Risasi Mchanganyiko halikufanikiwa kujua kipimo hicho kilitambua nini!

BABA DIAMOND AFUNGUKA
Baada ya kupimwa na kupatiwa dawa za kutumia, baba Diamond aliliambia gazeti hili kuwa, anamshukuru daktari huyo kwani ameweza kugundua tatizo linalomsumbua na kwamba anaamini dawa alizopewa zitamsaidia.
“Kwa kweli ni Mungu tu, hali yangu ni mbaya, miguu inanisumbua kwa zaidi ya miaka nane sasa. Inauma, imevimba na inabadilika rangi kuwa myeupe. Inakuwa kama inatoka mabakamabaka. Kiuchumi siko vizuri kabisa.”

NGOZI IMEATHIRIKA
“Dk. Fadhili amenipima, amebaini ngozi yangu imeathirika vibaya. Amenitajia tatizo langu kitaalamu na amenipa dawa za kutumia, lakini pia amenielekeza mazoezi maalum ambayo natakiwa kuyafanya,” alisema baba Diamond huku uso wake ukijaa simanzi.


AMWAGA SHUKRANI
Baba Diamond alipoulizwa kama alimueleza mwanaye Diamond kuhusu suala hilo wakati alipozidiwa, alisema hakuona na haoni sababu ya kumwambia kwani analijua na hapendi kuendeleza malumbano na mwanaye lakini anamshukuru Dk. Fadhili kwa kujitolea kumsaidia bila malipo yoyote.


“Sipendi kuendeleza malumbano, ninachokiangalia kwa sasa ni miguu yangu. Nitamshukuru Mungu zaidi nitakapopona kabisa maana nimeshahangaika nayo sana. Kipekee, kutoka moyoni nimshukuru Dk. Fadhili kwa kusikia kilio changu na kunisaidia bure.
“Sikutegemea, mtu unaumwa, anakwambia anakutumia fedha ya teksi uende hospitalini kwake akakutibu bure. Ni upendo wa hali ya juu na Mungu amzidishie, pale alipotoa apabariki na apate zaidi,” alisema baba Diamond.


DIAMOND ANASEMAJE?
Gazeti hili lilifanya jitihada za kutaka kumsikia Diamond anazungumziaje suala hilo la ugonjwa hadi kufikia mzazi wake kusaidiwa na mtu baki, simu yake haikuwa hewani lakini hata alipotumiwa ujumbe mfupi wa maandishi kupitia Mtandao wa WhatsApp ulioonesha ameusoma, bado hakujibu chochote.

TUMEFIKAJE HAPA?
Baba Diamond amekuwa akisumbuliwa na ugonjwa huo wa miguu ambapo awali, mzazi huyo alisema anasumbuliwa na kansa ya ngozi lakini hata hivyo, mwanaye Diamond amekuwa mzito kumsaidia kutokana na kile kinachodaiwa kuwa ni mwanaume huyo kumtelekeza mama Diamond, Sanura Kassim ‘Sandra’ yeye akiwa mdogo.

MAJIBU YA DK. FADHILI
Juzi Jumatatu, Risasi Mchanganyiko lilimpigia simu daktari huyo na kumuuliza kuhusu tatizo la baba Dimaond na namna alivyolishughulikia, ambapo alijibu:

“Ha! Jamani, ugonjwa wa mtu ni siri kati yake na daktari, labda kama ataona sawa aseme yeye mwenyewe.”
author

This post was written by: Author Name

Your description comes here!

Get Free Email Updates to your Inbox!

Post a Comment

CodeNirvana
Chediel . Powered by Blogger.
© Copyright Rundugai Blog
Back To Top